Tanzania yakabidhiwa taarifa kuhusu ugonjwa wa mnyauko wa minazi
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa Serikali
yake imedhamiria kukabiliana na maradhi ya mazao likiwamo zao la mnazi ambalo linakabiliwa
na tatizo la mnyauko. Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa ni muhimu kwa Serikali kuchukua
hatua za kukabiliana na tatizo la minazi kwa sababu watu wengi katika baadhi ya maeneo
ambayo uchumi wake unategemea zao la mnazi wanakabiliwa na hatari ya kweli kweli ya
kuathirika kwa maisha yao.
Rais Kikwete ametoa uhakikisho huo Jumamosi, Novemba
16, 2013, wakati alipokutana na Waziri wa Maendeleo ya Minazi na Maendeleo ya Shamba
la Janatha wa Sri Lanka, Mheshimiwa Jagath Pushpakumara na ujumbe wake mjini Colombo.
Waziri huyo aliandamana na Mwenyekiti wa Taasisi ya Utafiti ya Minazi ya Sri Lanka.
Rais
Kikwete yuko nchini Sri Lanka kuhudhuria Mkutano wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya
ya Madola (CHOGM) unaomalizika leo, Jumapili, Novemba 17, 2013. Mkutano huo wa siku
tatu, ulianza Ijumaa, Novemba 15, 2013. Mheshimiwa Pushpakumara na ujumbe wake walikuwa
wanamwelezea na kumkabidhi Rais Kikwete Ripoti ya Magonjwa ya Minazi iliyoandaliwa
na wataalam wa minazi wa Sri Lanka ambao walitembelea Tanzania Julai mwaka huu.
Wataalam
hao walitembea Tanzania na kufanya utafiti kuhusu ugonjwa unaolikabili zao la minazi
kufuatia ahadi ya Rais Mahinda Rajapaksa aliyoitoa kwa Rais Kikwete wakati alipofanya
ziara rasmi ya Tanzania Juni 27, 2013, na baadaye kushiriki katika Mkutano wa Smart
Partnership Juni mwaka huu.
Rais Rajapaksa alitoa ahadi hiyo baada ya kuelezwa
na Rais Kikwete kuhusu zao la kukauka kwa minazi nchini. Minazi ni zao muhimu sana
katika uchumi wa Sri Lanka na ni zao tegemeo kwa wananchi wa Taifa-Kisiwa hilo kilichoko
kusini mashariki mwa India katika Bahari ya Hindi. Wataalamu waliofuatana na Waziri
huyo wamemwambia Rais Kikwete kuwa ugonjwa unaolikabili zao hilo la minazi ambao pia
unashambulia minazi katika eneo la Caribbean hauna tiba kwa sababu mpaka sasa hakuna
taasisi yoyote ya utafiti imegundua dawa hiyo.
Wataalam hao ambao walikaa Tanzania
kwa wiki moja, zikiwamo siku mbili katika Zanzibar, wanasema kuwa zao hilo la mnazi,
kama ilivyo katika nchi nyingine zinazolima zao hilo, lina uwezo mkubwa wa kusaidia
uchumi kupitia viwanda vidogo vidogo. Wakati wakiwa Tanzania, wataalam hao wa Sri
Lanka walifanya uchunguzi na utafiti kwa karibu na wataalam wa Taasisi ya Utafiti
ya Kilimo ya Mikocheni (MARI).
Rais Kikwete azungumza kwa ajili ya viongozi
wenzake Sri Lanka
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho
Kikwete amesema kuwa maoni ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola kuhusu ajenda ya
maendeleo baada ya mwaka 2015 yatakuwa mchango mkubwa kuhusu nini kifanyike baada
ya kumalizika kwa kipindi cha Malengo ya Maendeleo ya Milenia (MDG).
Aidha,
Rais Kikwete ameipongeza nchi ya Sri Lanka kwa kuandaa vizuri na kwa mpangilio mzuri
Mkutano wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Madola (CHOGM) uliomalizika mchana
wa leo, Jumapili, Novemba 17, 2013.
Rais Kikwete ameyasema hayo na kutoa pongezi
hizo Jumamosi, Novemba 16, 2013, wakati alipotoa Salamu za Shukrani kwa niaba ya viongozi
wote waliohudhuria Mkutano huo kwenye Chakula cha Usiku rasmi kilichoandaliwa na Rais
wa Sri Lanka, Mheshimiwa Mahinda Rajapaksa kwenye Ikulu ya Temple Trees ya nchi hiyo.
Akizungumza
kwa niaba ya viongozi wenzake, Rais Kikwete amesema: “Mada ya mwaka huu ya mkutano
wetu wa CHOGM ya Maendeleo ya Pamoja kupitia Ukuaji wa Pamoja imekuja kwa wakati unaofaa.
Kwa taasisi kama ya kwetu ambayo inawakilisha watu bilioni mbili kujadili suala hilo
hasa kwa kutilia maanani mjadala unaoendelea kuhusu ajenda ya maendeleo baada ya mwaka
2015 ni jambo la busara sana.”
Mkutano wa CHOGM ambao ulianza Ijumaa, Novemba
15, 2013, umemalizika Jumapili tarehe 17 Novemba 2013 kwenye Kituo cha Mikutano cha
Kumbukumbu ya Bandaranaike mjini Colombo, Sri Lanka.
Akizungumzia mkutano huo,
Rais Kikwete amesema: “Tunakupongeza Mheshimiwa Rais kwa maandalizi mazuri ya Mkutano
huo. Tunajua siyo kazi rahisi kuandaa Mkutano wa ukubwa huu. Lakini kwa uongozi wako
wa busara na uongozi wako, kwa kusaidiana na Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola, kila
kitu kimekwenda vizuri.” Ameongeza Rais Kikwete: “Kwa niaba ya viongozi wenzangu waliokusanyika
hapa jioni ya leo, napenda kukutakia wewe, Mheshimiwa Rais, kila la heri katika uendeshaji
wa taasisi yetu hii.”