2013-11-18 10:50:07

Onjeshaneni tone la furaha, matumaini na machungu ya maisha kwa kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu!


Jumuiya ya Kimataifa inaanza kugundua tena umuhimu wa kujenga na kudumisha mshikamano wa dhati miongoni wa Jamii mbali mbali kama njia ya kupambana na majanga ya maisha, ili kwa pamoja kama Jumuiya waweze kuonjeshana tena tone la furaha, matumaini na machungu ili kwa pamoja waweze kukumbatia zawadi ya maisha! Binadamu anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza na viongozi wa kisiasa na kidini, kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima yake na kamwe asiwe ni kichokoo cha udadisi wa tafiti za kisayansi.

Majadiliano ya kidini miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali yanawachangamotisha wadau kuhakikisha kwamba, wanaheshimu dini na mafundisho tanzu ya kila dini; kutobeza dini za watu wengine pamoja na kuthamini tofauti mbali mbali zinazojitokeza miongoni mwa Jamii, kwani huu ni utajiri mkubwa na wala si tishio kwa amani, usalama na ustawi wa Jamii husika.

Huu ni mchango wa Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini wakati alipokuwa anachangia kwenye Semina iliyoandaliwa na Kituo cha Majadiliano ya Kidini na Kitamaduni cha Mfalme Abdullah Bin Aziz, kwa kifupi KAICIID huko Vienna, Austria, tarehe 18 Novemba 2013 kwa kuongozwa na kauli mbiu "Sura ya mwingine".

Anasema, majadiliano ya kidini yanaweza kusaidia mchakato wa kumpatia Mwenyezi Mungu kipaumbele cha kwanza katika maisha ya watu; kujenga na kudumisha mshikamano wa kidugu pamoja na kuwa nari ya kutenda kwa ujasiri. Majadiliano ya kidini yasaidie kusafisha dhamiri na kuwa tayari kupokea mawazo mapya kutoka kwa wengine sanjari na kukubali changamoto zinazotolewa katika masuala ya imani, kwa ajili ya mafao ya wengi.

Waamini wajifunze kuheshimiana na kuthaminiana kwani wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.