2013-11-16 11:28:04

Jubilee ya Miaka 50 tangu Mashahidi wa Uganda kutangazwa kuwa Watakatifu, Papa Francisko anaalikwa na Maaskofu wa Uganda!


Baraza la Maaskofu Katoliki Uganda, limetoa mwaliko kwa Baba Mtakatifu Francisko, kutembelea nchini Uganda, kama sehemu ya kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Mashahidi wa Uganda walipotangazwa na Mama Kanisa kuwa ni watakatifu, kielelezo na mfano wa kuigwa katika imani na maisha adilifu.

Kilele cha Maadhimisho haya ambayo nchini Uganda yamekwenda sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kitakuwa hapo tarehe 18 Oktoba 2014, wakati ambapo Madhabahu ya Namgongo yatakapofurika kwa umati wa mahujaji kutoka ndani na nje ya Uganda. Mashahidi wa Uganda walitangazwa kuwa Watakatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican hapo tarehe 18 Oktoba 1964.

Nia ya Baraza la Maaskofu Katoliki Uganda, ilibainishwa na Askofu mkuu Cyprian Lwanga wa Jimbo kuu la Kampala alipokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko, hapo tarehe 21 Septemba 2013 mjini Vatican. Ikiwa kama Baba Mtakatifu Francisko ataridhia hija hii ya kichungaji, pengine itakuwa ni hija ya kwanza kwa Baba Mtakatifu kulitembelea Bara la Afrika tangu alipochaguliwa.

Mwenge maalum wa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Mashahidi wa Uganda walipotangazwa kuwa watakatifu unaendelea kuzunguka katika Parokia 54 zinazounda Jimbo kuu la Kampala, kama kikolezo cha ushuhuda wa imani tendaji katika kuikiri, adhimisha, mwilisha na kusali imani ambayo ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, lakini inamwajibisha mwamini kuitolea ushuhuda, ili Kristo aendelee kuwa ni Mwanga wa Mataifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.