2013-11-16 09:33:34

Balozi wa Vatican nchini Tanzania awataka waamini kuendelea kuwa ni chumvi na mwanga wa mataifa!


Yafuatayo ni mahubiri yaliyotolewa na Askofu mkuu Francisco Montecillo Padilla, Balozi wa Vatican nchini Tanzania wakati wa Ibada ya kufunga Mwaka wa Imani nchini Tanzania, hapo tarehe 10 Novemba 2013, Parokiani Bagamoyo, Jimbo Katoliki la Morogoro. Ibada ambayo ilihudhuriwa na umati mkubwa wa Familia ya Mungu nchini Tanzania. RealAudioMP3

Mwadhama
Ndugu zangu Maaskofu Wakuu na Maaskofu
Wapendwa Mapadri, watawa, viongozi wa serikali
Wapendwa waamini.

Tunapo adhimisha Misa hii ya kufunga rasmi Mwaka wa Imani kitaifa, ningependa nianze na maneno ya Kristo anayesema: “Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani” (Yn 12:46).

Mwanga huu ulikuja duniani miaka elfu mbili iliyopita. Mwanga huu ndiyo tabia ya Ufalme wa Mungu, ulio anzishwa na Kristo Mfalme. Alikuja kusimika Ufalme hapa duniani, ufalme ambao si mamlaka ya dola bali Ufalme wa Imani unao dhihirika katika upendo na heshima.

Sisi ni sehemu ya ufalme huu. Sisi pia tumepokea mwanga huu, imani hii mioyoni mwetu iliyoletwa na wamisionari shupavu. Kwa namna ya pekee nawashukuru Mapadri wa Shirika la Roho Mtakatifu kwa majitoleo na sadaka zao katika kuleta mwanga huu, imani hii ambayo ilianzia Zanzibar na kuingia Bara kupitia Bagamoyo. Hii ndiyo sababu tunaadhimisha Misa hii mahali hapa.

Watu waliifurahia imani hii, waliufurahia mwanga huu. Lakini hapo katikati, imani ikahusishwa na giza. Watu wengi wakaacha kuihusisha imani na Kristo wakaihusisha na wanadamu, hivi kwamba kiini cha imani kikawa si Kristo tena bali watu. Huu ukageuka kuwa mwanga binafsi, ulioweza labda kuufurahisha moyo na kumfariji mtu binafsi lakini si tena mwanga unaoweza kupendekezwa kwa wengine kama mwanga halisi na ambao watu wanaweza kuushiriki na kuona njia. Unapopotea mwanga huu mkubwa ambao ni Yesu Kristo, kila kitu kinatatanisha. Inakuwa ni vigumu kupambanua wema na uovu, au njia inayotuongoza kwenye lengo letu na zile njia zisizo tufikisha popote. Ufalme wa Mungu uliojengwa duniani umepitia katika hali ya kumfanya Mungu asionekane na watu kuishi katika “jangwa” la kiroho.

Katika miaka ya hivi karibuni, tumeshuhudia jinsi ambavyo maisha au dunia bila Mungu jinsi ilivyo. Sasa tunaiona hali hiyo kila siku katika maisha yetu. Utupu umeongezeka. Kwa watu wengi tatizo kati ya imani na maisha limeongezeka. Lipo hitaji la lazima sasa kuhakikisha kwamba imani inakuwa tena mwanga, yaani Yesu Kristo mwenyewe, anayeweza kuangaza kila hali ya maisha ya mwanadamu.

Ndiyo maana Mwaka wa Imani ulianzishwa na Papa Benedikto na kuendelezwa na Papa Fransisko kwa lengo la kupambana na tatizo la kupotea kwa imani ili kujitahidi kuirudisha imani mahala pake: yaani imani kwa Kristo na siyo imani kwa ubinafsi wa mtu. Imani ya kweli inazaliwa katika kukutana na Mungu aliyehai ambaye anatualika na kuufunua upendo wake, upendo ambao tunaweza kujifunza ili utulinde na utusaidie kujenga maisha ya watu. Wakigeuzwa na upendo huu, watu wa Ufalme wa Mungu hapa duniani wanapata muono mpya, macho mapya yanayo wafanya kutambua kuwa imani inabeba ahadi kubwa ya maisha mema na kwamba dira ya maisha yajayo inafunguka mbele ya kila mmoja.


Mwaka wa Imani umewafanya kugundua na kuuiona sura ya Kristo. Na mtu anapoiona sura ya Kristo, basi upendo unaumbwa katika moyo wake na kumgeuza kuwa mtu anaye hamasisha upendo katika jamii ya leo. Kwa hiyo imani hii mpyainazaa upendo na kwa upendo huu mtu anakuwa mwanga wa ulimwengu. Kwa nini leo hii kuna chuki sana katika jamii? Kwa sababu hakuna mwanga na upendo. Kwa kuadhimisha mwaka wa imani mtu anakuwa mwanga unaofuatwa na wengine kwa kuendeleza kazi za Kristo, kazi za upendo, msamaha, maridhiano na amani. Kwa ufupi, Mwaka wa Imani umewaalika kuwa mashahidi wa kweli wa Kristo kwa wengine. Haiwezekani tena baada ya maadhimisho haya ukabaki kuwa mtu uliyejitenga, unaye tumainia nafsi yako na ubinafsi wako kama msingi wa matendo yako

Watu huishi daima katika uhusiano. Unatoka kwa wengine, wewe ni wa wengine na maisha yako lazima yatajirishwe kwa kukutana na wengine. Mioyo yenu itajazwa na imani hii, itajazwa na nafsi ya Kristo ili kwamba pasiwepo tena nafasi ya chuki, wivu, ubinafsi. Unakuwa mmisionari wa kweli wa Yesu Kristo, ukidumisha amani, msamaha na maridhiano, ambazo ni sifa za Ufalme wa Mungu duniani, ufalme ambao dunia inautamani sana leo hii.


Ndiyo, baada ya mwaka wa imani, mnapewa utume wa kuwa mwanga na chumvi ya ulimwengu. Na katika kutekeleza utume huu, matatizo yatakuwa mengi kwa sababu mtakutana na mbwa mwitu walio tayari kuwa rarua wale wanaopeleka ujumbe wa Yesu Kristo. Ndugu zangu, hiyo ndiyo hali yetu: sisi ni wamisionari waliotumwa kama kondoo kati ya mbwa mwitu ili kutangaza ujumbe wa upendo, msamaha, maridhiano na amani katika dunia iliyojaa vurugu. Wamisionari siyo wale tu walioacha familia na nchi zao kwenda kutangaza injili. Sisi sote, kadiri ya hali zetu za maisha, kwa ubatizo wetu na kwa imani tuliyoipokea ni wamisionari na ni wajibu wetu kutimiza wito wetu wa kuwa watatkatifu katika maisha na kupanda duniani injili ya upendo na amani.


Mtu anawezaje kuwa nuru na chumvi ya dunia? Baada ya maadhimisho haya ya mwaka wa imani, kila mmoja wetu anapaswa kujichunguza na kutafakari kama yametokea mabadiliko yoyote moyoni mwake; kama amegundua utume wa maisha yetu wa kujenga Ufalme wa Mungu hapa duniani. Jamii ambamo upendo, kuheshimiana na haki vinatawala. Mwaka wa imani unadai wale wote walio na wajibu wa kisiasa, kiuchumi na katika masuala ya jamii kuwa na ujuzi juu ya mafundisho ya jamii ya Kanisa, ambayo yanaweza kuwapatia misingi ya kutenda kulingana na Injili. Watu hawa wanatakiwa kuwa mashuhuda wa kikristo na wataamika pale tu watakapo fanya kazi zao kwa uaminifu na weledi; pale tu watakapokuwa na imani itakayo waongoza kutenda kwa upendo na kuwahudumia watu wote, hasa masikini.

Imani hii inapaswa kutuwezesha, kwanza kabisa, kuheshimu mazingira na kutambua sarufi iliyoandikwa kwa mkono wa Mungu kuwa ni mahali pa kuishi ambapo kila mmoja anapaswa kupalinda na kupatunza. Imani hii itawawezesha watu kutafuta namna za maendeleo ambazo msingi wake siyo tu matumizi na faida bali yale yaliyo mema na ya haki katika jamii. Imani hii itatufundisha kuunda mifumo ya uongozi iliyo ya haki kwa kuunda dhamiri za wale wanaoongoza kutambua kuwa mamlaka hutoka kwa Mungu na yapo kwa ajili ya kuhudumia manufaa ya wote. Imani hii itatupatia fursa ya kusamehe, jambo ambalo mara nyingi linahitaji muda, jitihada, uvumilivu na uthabiti. Msamaha unawezekana pale mtu anapogundua kwamba wema unashika mahali pa kwanza na una nguvu kupita uovu na kwamba neon la Mungu lina nguvu kuliko mtu anavyoweza kulikataa.

Katika jamii yetu leo, tunahitaji wakatoliki ambao ni mfano wa fadhila zinazo hubiriwa katika Injili, maisha ya ushuhuda wa upendo, maridhiano na amani. Kama bado hatuweza kuzalisha wakatoliki wa namna hii au kama tunaona kila wanacho amini hakipatani na kile wanachoishi, hapo tujue kwamba bado tuna kazi ya kufanya ili kupata watu waadilifu na wenye imani. Ni wajibu wetu kuwaonesha watu tena uzuri, wema na ukweli wa sura ya Kristo ambao ndani yake kila mwanadamu anaalikwa kutambua kielelezo cha kweli cha kufuata. Kwa hiyo hii ndiyo changamoto yetu kubwa baada ya mwaka wa imani: kuwaelekeza watu wa leo kwa Kristo, kumtambulisha kama kipimo cha kweli cha ukomavu na ukamilifu wa mwanadamu.


Katika Bara la Afrika, hali halisi inadai uwezo wa kujumuisha makuzi ya kiakili ya imani na uzoefu wa maisha ya kukutana na Kristo aliye hai na anayetenda katika jumuiya ya kikanisa. Mapadri na Maaskofu mnapaswa kusisitiza ukweli kwamba kuwa mkristo si matokeo ya maamuzi ya kimaadili bali kukutana na nafsi ya Kristo. Waamini wanapaswa kufundishwa kuwa daima umoja ni bora kuliko mafarakano na palipo na mafarakano ya watu na maslahi, si vema kupuuzia. Ni muhimu kukabiliana na hayo kwa lengo la kutafuta ufumbuzi na kusonga mbele katika kufikia umoja na maridhiano.


Ni wajibu wetu kama viongozi kuitunza imani hii ndani ya watu wetu. Imani na upendo vinapodhoofika, misingi ya ubinadamu nayo inatiwa hatarini. Ndiyo, kama tutaondoa imani kwa Mungu katika miji yetu, kuaminiana kutatoweka. Watu watabaki wameungana katika hofu na uthabiti utapotea. Sote tunapaswa kuwa mwanga kwa wale walio bado gizani, wale wasiofahamu bado hali za wanadamu na matukio. Imani yenu leo itakuwa taa ya kuongoza hatua zenu katika usiku maisha na katika safari yenu ya upendo, msamaha, maridhiano na amani.


Ninawaalika tuimarishwe kwa maneno ya Kristo: Msiogope, niko pamoja nanyi mpaka ukamilifu wa dahari. Katika wakati wa shida na majaribu, zawadi hii bora ya imani leo iwaongoze kwenye matumaini, matumaini yanayoangalia mbele katika ufahamu kwamba ni katika nafsi ya Yesu Kristo pekee ndimo nafsi zetu na Kanisa letu na jamii yetu inamoweza kupata misingi imara nay a kudumu. Ni katika muungano wa imani na upendo, matumaini yanatuongoza katika safari ya kuelekea siku zijazo kwa hakika na kufutilia mbali kudanganywa na mali za dunia. Msihurusu kuibiwa matumaini haya ambayo yanawatia ujasiri wa kusonga mbele hata katika hali ngumu.

Mwaka wa Imani ni mwanzo tu. Tutaendelea na safari ili kutajirisha maisha yetu kwa nafsi ya Yesu Kristo. Huyu ndiye atakaye tufanya kuwa vyombo vya mabadiliko kwa jamii. Tuombe mwaka huu wa imani uwe tukio lenye kuzaa matunda kwa kila mmoja wetu kukuza uhusiano wake na Munguna wengine. Mwaka huu uwaimarishe muweze kujenga utamaduni wa upendo kwa kutoa msamaha, kusaidia maridhiano na amani.


Ninaomba ili tuweze kusambaza tunu hizi bora kwa jamii na ulimwengu upate kuwa mahali pazuri kuishi kulingana na mfumo wa Ufalme wa Mungu uliojengwa na Kristo kwa ajili yetu, ambamo wote tunakuwa kielelzo cha fadhila za msamaha, maridhiano na amani sasa na hata milele.

Tumsifu Yesu Kristo. Amina.








All the contents on this site are copyrighted ©.