2013-11-14 10:27:34

Kanisa katika huduma kwa wazee wagonjwa wa mishipa ya fahamu!


Zaidi ya wajumbe 400 kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanatarajiwa kushiriki katika mkutano wa ishirini na nane wa kimataifa ulioandaliwa na Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi wa sekta ya afya; mkutano unaoongozwa na kauli mbiu "Kanisa katika huduma kwa wazee wagonjwa: tiba kwa wagonjwa walioathirika na magonjwa ya mishipa ya fahamu.

Huu ni mkutano utakaowashirikisha wataalam wa magonjwa ya mishipa ya fahamu, watunga sera za tiba ya magonjwa ya mishipa ya fahamu katika karne ya ishirini na moja. Tafiti na tiba mbali mbali ambazo zimekwishapatikana hadi sasa na matumaini kwa siku za usoni. Wajumbe watapata fursa ya kupembua kwa kina na mapana magonjwa ya mishipa ya fahamu yanayowashambulia wazee na mahali muafaka pa kupatia tiba.

Wataangalia mbinu mkakati wa kuzuia magonjwa ya mishipa ya fahamu kwa wazee. Viongozi wa Kanisa watashirikisha mang'amuzi ya kitaalimungu na kichungaji na huduma zinazotolewa na Mama Kanisa katika sekta ya afya. Mkutano huu utafunguliwa kwa Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Alhamisi tarehe 21 Novemba 2013 na kuhitimishwa tarehe 23 Novemba 2013 kwa sala na tafakari.

Baadaye wajumbe hawa watakutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko ambaye anaendelea kuonesha upendeleo wa pekee kwa wagonjwa kwani hawa ni rasilimali muhimu katika maisha na utume wa Kanisa na kamwe wasisukumizwe pembezoni mwa Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.