2013-11-13 07:48:15

Mashirika ya Misaada ya Kanisa, Majimbo, Parokia na watu binafsi waanza kuchangia wananchi wa Ufilippini


Baba Mtakatifu Francisko amepokea kwa masikitiko na majonzi makuu taarifa za mahangaiko ya wananchi wengi wa Ufilippini kutokana na kukumbwa na tufani ambayo imesababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao.
Baba Mtakatifu katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuchangia kwa hali na mali juhudi za kuokoa maisha ya mamillioni ya watu waliofikwa na janga hili kutokana na kukumbwa na tufani cha Haiyan kilichotokea nchini Ufilippini, hivi karibuni. Kutokana na mwaliko huu wa Baba Mtakatifu, Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki, Majimbo, Parokia na watu binafsi kutoka sehemu mbali mbali za dunia wameanza kuchangia juhudi za kuokoa maisha ya watu walioathirika na tufani.
Shirika la Kipapa kwa ajili ya misaada kwa Kanisa hitaji limetoa kiasi cha Euro 1000,000 kama sehemu ya mchango wake kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Ufilippini wakati huu wanapokabiliana na janga hili kwa wananchi wao. Umoja wa Mataifa unakaidiria kwamba, zaidi ya watu millioni 11 wameathirika kutokana na tufani hii, watu zaidi ya 673,000 hawana makazi baada ya nyumba zao kubomolewa kutokana na upepo na mvua kali. Maaskofu wanasema, waathirika ni wengi zaidi ya taarifa zinavyoonesha na kwamba, ni vigumu kwa Serikali kuweza kukidhi mahitaji ya wananchi wake kwa sasa.
Waathirika kwa sasa wanapata hifadhi kwenye nyumba za Ibada, shule na viwanja vya michezo, kwani nyumba na majengo mengi yameathirika vibaya kiasi kwamba, hayafai tena kwa matumizi ya binadamu. Shirika la Kipapa kwa ajili ya Makanisa hitaji linasema kwamba, kwa sasa msaada uliotolewa unalenga kukabiliana na dharura iliyojitokeza, lakini kwa siku za usoni, watajipanga ili kuanza ujenzi wa miundo mbinu ya Kanisa katika shughuli za kiuchungaji kwa maeneo yaliyoathirika kwa tufani ya Haiyan.







All the contents on this site are copyrighted ©.