Jeshi la Polisi nchini Tanzania linapenda kuutaarifu umma kwamba aliyekuwa Mkurugenzi
wa Upelelezi wa makosa ya jinai (DCI) Robert Manumba amefikia umri wa kustaafu kisheria
ambao ni miaka sitini (60) katika utendani wake wa kazi.
Aidha, katika utumishi
wake ndani ya Jeshi la Polisi amefanya kazi katika nyadhifa mbalimbali zikiwemo Chumba
cha kupokea mashtaka kuanzia mwaka (1976 – 1977), mwendesha mashtaka wilaya ya Kibondo
na Kasulu mkoani Kigoma, 1977 – 1984), Mkufunzi katika chuo cha polisi Dar es salaam,
(1984 – 1987), Mkuu wa Upelelezi wilaya ya Magomeni na Kinondoni na Naibu Mkuu wa
upelelezi wa mkoa wa Dar es salaam (1987 – 1993),
Pia, amewahi kuwa Mkuu
wa upelelezi wa mkoa wa Arusha, ( 1993 – 1995), Mkufunzi mkuu wa Chuo Cha Polisi
Moshi ( 1995 – 1996), Mkuu wa kitengo cha Fraud makao makuu ya upelelezi, (1996 –
1997), Mkuu wa kitengo cha usalama wa nchi, intelijensia na madawa ya kulevya makao
makuu ya upelelezi (1997 – 2001) na kuwa msaidizi wa mkurugenzi wa upelelezi wa makosa
ya jinai nchini (2001 – 2006). Kuanzia mwaka 2006 hadi anastaafu, alikua Mkurugenzi
wa upelelezi wa makosa ya jinai nchini Tanzania
Aidha, Mkuu wa Jeshi la Polisi
nchini (IGP) Said Mwema, amemshukuru na kumpongeza (DCI) Manumba anayestaafu kwa kulitumikia
taifa katika nyadhifa mbalimbali ndani ya Jeshi la Polisi kwa weledi na uwaminifu
mkubwa wakati wote alipokuwa mtumishi ndani ya Jeshi la Polisi. Pia, amemtaka kuendelea
kuwa msaada kwa Jeshi la Polisi kwa kutoa ushirikiano wa namna yoyote ile unaoweza
kusaidia kupunguza uhalifu hapa nchini kwasababu suala la usalama ni taaluma kama
zilivyo taaluma zingine, na taaluma hiyo wanayo watu wachache.
Hata hivyo,
wakati taratibu wa uteuzi wa mkurugenzi wa upulelezi ukiendelea, mkuu wa ufuatiliaji
na tathimini CID makao makuu, kamishina Isaya Mungulu, atakua akikaimu nafasi hiyo.
Wakati
huo huo, wanaharakati za haki msingi za binadamu wanasema, DCI Manumba anang'atuka
madarakani wakati bado watu wanaendelea kuwaza na kuwazua juu ya kushamiri kwa vitendo
vya ukatili kwa viongozi wa kidini na serikali kama ilivyojionesha hivi karibuni.
Watu wanasubiri kusikia wahusika wametiwa nguvuni na kufikishwa kwenye vyombo vya
usalama!