2013-11-11 10:48:41

Hakuna nchi iliyopata kucharuka katika maendeleo kwa kutumia koroboi ama karabai!


Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania amesema kuwa Serikali yake inaelekeza nguvu nyingi na kasi mpya katika umeme kwa sababu hakuna nchi iliyopata kuendelea kwa kutumia koroboi ama karabai. Aidha, Rais Kikwete ametaka vyombo vinavyohusika na kusambaza na kuunganisha umeme katika vijiji mbali mbali nchini kuongeza kasi ya kufanya kazi kwa sababu ni lazima vijiji 1,600 vipate umeme katika muda mfupi.

Rais Kikwete ameyasema hayo Jumapili, Novemba 10, 2013 wakati alipozungumza na wananchi katika eneo la Buseresere/Katoro, mpakani mwa wilaya za Geita na Chato, Mkoa wa Geita ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake katika Mkoa wa Geita ambako amekuwepo kwa siku tatu. Buseresere na Katoro ni miji iliyoungana lakini Buseresere iko Wilaya ya Chato na Katoro iko Wilaya ya Geita.

Rais Kikwete alikuwa anazungumza na mamia kwa mamia ya wananchi kabla ya kuzindua mradi mkubwa wa kusambaza umeme katika vijiji vya wilaya nne za Mkoa wa Geita na moja ya Mkoa wa Shinyanga. Umeme unasambazwa katika vijiji 14 vikiwamo 10 vya Wilaya ya Geita. Umeme huo ni sehemu ya miradi mikubwa ya miundombinu ya umeme, barabara, maji na Uwanja wa Ndege wa Mafia inayogharimiwa na Shirika la Maendeleo ya Milenia (MCC) la Marekani kupitia Shirika la Maendeleo ya Milenia Tanzania (MCA-T).

Mradi huo wa kusambaza umeme katika vijiji vya wilaya za Geita, Chato na Nyang’hwale Mkoani Geita na Msalala (Shinyanga) umegharimu dola za Marekani 21, 477, 181 (sawa na Sh. Bilioni 36.3) na utanufaisha wateja 3,500 katika maeneo hayo. Akizungumza katika sherehe hiyo, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali yake imeamua kuelekeza nguvu nyingi katika kusambaza umeme vijijini kwa sababu umeme ndiyo maendeleo. “Hakuna nchi iliyopata kuendelea duniani kwa kutumia koroboi ama karabai. Nchi zote zilizoendelea zimefanya hivyo kwa kutumia umeme na kuwekeza ipasavyo katika sekta hiyo ya umeme.”

Akijibu malalamiko ya wananchi kuwa usambaza wa umeme huo unachelewa pamoja na kwamba wamelipia kuunganishiwa umeme, Rais Kikwete ameziekeleza taasisi zinazohusika na kazi ya kusambaza na kuunganisha umeme. “Mmesikia wenyewe malalamiko ya wananchi kwamba kasi ya kuunganisha umeme siyo kubwa. Napenda tuongeze kasi kwa sababu tunayo kazi kubwa ya kusambaza umeme katika vijiji 1,600 vya nchi yetu katika muda mfupi ujao. Hivyo, tuongeze kasi ili tuweze kuikamilisha kazi hiyo mapema iwezekanavyo.”

Rais Kikwete pia amewaambia wananchi kuwa ili kuwawezesha wananchi kupata huduma ya umeme kwa urahisi, Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imepunguza ada za kuunganisha umeme kutoka sh. 450,000 hadi 170,000.

Mapema Jumamosi, Rais Kikwete amezindua Mradi wa Maji wa Masumbwe katika kijiji cha Shinyanga A, wilaya mpya ambazo ziliundwa na Rais Kikwete mwaka jana. Mradi huo uliogharimu Sh. Milioni 341 ni moja ya miradi ya maji katika vijiji 10 kila mkoa inayogharimiwa na Benki ya Dunia (WB).

Rais Kikwete pia amezindua Wodi ya Wazazi katika kituo cha afya cha Kijiji cha Iboya, Kata ya Mbogwe. Mradi huo umegharimu Sh. Milioni 57 na ujenzi wa wodi hiyo ni maandalizi ya kukifanya kituo hicho cha afya hospitali mpya ya wilaya mpya ya Mbogwe.

Naye Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Wilaya ya Bukombe, Mkoa wa Geita wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Profesa Kulikoyela Kanalwanda Kahigi amemsifu na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuendesha nchi vizuri na kuhangaika sana kuwaletea wananchi maendeleo. Aidha, Profesa Kahigi amemsifu Rais Kikwete kwa kuendesha nchi kwa makini na kwa kusikiliza pande zote na kuwa mwenye moyo wa kusaidia wananchi. Profesa Kahigi ametoa sifa na pongezi hizo Jumamosi, Novemba 9, 2013 wakati alipozungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye eneo la Stendi ya Mabasi mjini Ushirombo, Wilaya ya Bukombe.

Katika mkutano huo uliohutubiwa na Rais Kikwete akiwa kwenye siku yake ya pili ya ziara ya Mkoa wa Geita, Profesa Kahigi amewaambia mamia kwa mamia ya wananchi: “Namfahamu Rais Kikwete tokea tulipokuwa pamoja Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Ni mtu mwenye moyo na roho ya kibinadamu sana. Na pia napenda kumpongeza sana kwa kufanya kazi akisikiliza watu wengine na pande zote za kisiasa za nchi yetu,” amesema Profesa Kahigi na kuongeza: “Nawaomba viongozi ambao anawateua wawe na moyo kama wa kwake. Ni jambo la furaha vile vile kwamba Serikali ya Rais Kikwete inatuletea umeme katika wilaya yetu ambayo miaka na miaka hatuna umeme. Hili halina mjadala ni jambo la pongezi sana kwako Mheshimiwa Rais kutoka kwa wana-Bukombe.”

“Ni kweli zipo changamoto na kwa kweli tutaendelea kuzisema lakini jambo jingine zuri ni kwamba hata leo asubuhi tumeweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa barabara ya Uyovu-Bwanga kwa kiwango cha lami. Mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Rais wetu amefanya kazi nzuri sana kuwalete wananchi wetu maendeleo.”

Mapema, Jumamosi Rais Kikwete amezindua Shule ya Msingi ya Nga’nzo iliyoko Ushirombo, shule ambayo imedhaminiwa na ushirika wa wachimbaji wadogo wa dhahabu wa eneo hilo la Nga’nzo na kujengwa na mwekezaji wa ndani, Ndugu Emmanuel Gungu Silanga ambaye pia ni mwana-ushirika huo. Shule hiyo imejengwa baada ya shule ya zamani katika eneo hilo kuwa imetishiwa na wachimbaji dhahabu wadogo ambao walikuwa wanachimba katika eneo la shule ambako kwanza walikuwa wanachimba usiku lakini baadaye wakapat ujasiri wa kuchimba hata nyakati za mchana.

Shule hiyo imejengwa kwa gharama ya Sh. Milioni 460 na Rais Kikwete amewachangia wanaushirika wa wachimbaji wadogo katika eneo hilo Sh. Milioni mbili.


Rais Kikwete Jumamosi, Novemba 9, 2013, ameweka jiwe la msingi kwa ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara nyingine muhimu ikiwa ni barabara ya pili kuwekewa jiwe la msingi katika siku mbili za mwanzo za ziara ya Rais Kikwete mkoani Geita. Baada ya kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Barabara ya Bwanga-Biharamulo , Ijumaa, Novemba 8, 2013, kwenye siku ya kwanza ya ziara yake, Rais Kikwete ameweka jiwe la msingi la ujenzi kwa kiwango cha lami la Barabara ya Iyovu-Bwanga.

Barabara ya Bwanga-Biharamulo ambayo sherehe za uwekaji jiwe lake ulifanyika kwenye Kijiji cha Buziku, Tarafa ya Bwanga, ina kilomita 67 na ni barabara nyingine ambayo inaunganisha mikoa ya Kagera na Geita. Barabara hiyo inayojengwa na kampuni ya Sinohydro ya China inagharimu Sh. Bilioni 54.76 na inatarajiwa kuwa imekamilika Februari mwaka 2015.

Sherehe za uwekaji jiwe la msingi kwenye Bararaba ya Iyovu-Bwanga zimefanyika kwenye Kijiji cha Iyovu, Kata ya Runzewe na kuhudhuriwa na mamia kwa mami ya wananchi. Barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 45 inajengwa kwa kiasi cha Sh. Bilioni 43.36 na inatarajiwa kumalizika Agosti, mwakani, 2014.








All the contents on this site are copyrighted ©.