Waamini kutoa heshima kwa masalia ya Mtakatifu Petro mjini Vatican wakati wa kufunga
Mwaka wa Imani
Askofu mkuu Rino Fisichella, Rais wa Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Uinjilishaji
Mpya anasema, katika Maadhimisho ya Kufunga Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa
na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa Maadhimisho ya Sherehe
ya Kristo Mfalme, kwa mara ya kwanza katika historia ya Kanisa, waamini watapata fursa
kutoa heshima yao kwa masalia yanayosadikiwa kuwa ni ya Mtakatifu Petro, Mwamba wa
Imani.
Huu ni mwaliko wa kuendelea kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya
imani na kuendelea kumwabudu, daima waamini wakitambua kwamba, Uinjilishaji mpya unafanyika
kwa njia ya kupiga magoti, yaani kwa njia ya sala inayomwilishwa katika matendo na
ushuhuda wa maisha ya Kikristo. Waamini wanapaswa kujenga na kudumisha ari na moyo
wa sala kama njia ya kujenga uhusiano wa dhati na Mwenyezi Mungu. Bila uhusiano huu,
utume wowote unaofanywa na Mama Kanisa unakuwa ni kama kazi nyingine yoyote ya mshahara.
Waamini
wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, wanajenga na kuimarisha maisha
ya kiroho kama njia ya kuchuchumilia utakatifu wa maisha, mwaliko kwa kila mwamini.
Sala na kazi ni mambo msingi katika maisha ya Kikristo; mambo yanayopaswa kuendelezwa
hata baada ya kufunga rasmi Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Tarehe 21 Novemba 2013,
Baba Mtakatifu amechagua Monasteri moja iliyoko mjini Roma ili kwenda na kusali huko
kwa faragha. Utakuwa ni muda wa kuabudu, ili kuweza kufahamu mambo msingi katika maisha,
ili hatimaye, kuweza kuyakumbatia.
Askofu mkuu Fisichella anasema, Sala inapaswa
kupewa kipaumbele cha kwanza katika maisha na utume wa Kanisa. Waamini wajenge utamaduni
wa kutoka na kwenda katika "Jangwa" la maisha yao ili kutafakari matendo makuu ya
Mungu katika maisha yao; kwa kukuza na kuimarisha upendo kwa Mungu na jirani. Yesu
katika maisha yake hapa duniani, alipenda kujitenga kwa ajili ya sala. Mama Kanisa
kabla ya kujitosa kwa ajili ya Uinjilishaji hana budi kujikita kwanza katika maisha
ya sala na tafakari ya kina.
Baba Mtakatifu Francisko atawatembelea na kusali
na Wamonaki wa Camaldoli, Jumuiya ambamo wanaishi pia Watawa kutoka Tanzania. Anataka
kukazia umuhimu wa Tafakari ya Neno la Mungu, huduma kwa maskini na watu wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii, ili kuwaonjesha wengine ukarimu wa kile kidogo kinachotoka katika
undani wa moyo na maisha ya waamini. Waamini waitafakari sura ya Kristo kwa kuguswa
na mateso pamoja na mahangaiko ya maskini na wagonjwa.
Kwa matukio haya, Mama
Kanisa anajiandaa kwa namna ya pekee kabisa kufunga Maadhimisho ya Mwaka wa Imani,
kwa kutoa heshima kwa masalia ya Mtakatifu Petro, Mwamba wa Imani, aliyeyamimina maisha
yake kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Mwaka wa Imani uwachangamotishe waamini kuwa
na ari na mwamko mpya katika imani tendaji inayoshuhudiwa kwa maisha adili na matakatifu.
Hii ni hija inayopaswa kuendelezwa na waamini bila ya kuchoka wala kukata tamaa, kwa
kutafakari uso wa Yesu Msulubiwa!