2013-11-09 11:04:05

Utume na maisha ya familia pamoja na changamoto zake katika ulimwengu mamboleo!


Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia anasema kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ameonesha kipaumbele cha pekee kwa Familia katika utume kama Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa kuitisha Sinodi Maalum kwa ajili ya familia itakayoadhimishwa Mwezi Oktoba 2014. RealAudioMP3

Huu utakuwa ni wakati muafaka kwa Mama Kanisa kuweza kufanya tafakari ya kina kuhusu dhamana ya familia, fursa zilizopo na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Nia hii ya Baba Mtakatifu Francisko ni kielelezo cha upendo wa dhati kwa Familia ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake.

Askofu mkuu Paglia anasema kwamba, Mkutano wa ishirini na moja wa Baraza la Kipapa la Familia,imekuwa ni nafasi kwa wajumbe kuanza kunoa mawazo yao, kama sehemu ya mchakato wa maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia. Lengo ni kuliwezesha Kanisa kuendelea kutoa mchango wake katika masuala ya ndoa, familia na zawadi ya uhai.

Familia zinakabiliwa na changamoto kubwa ambazo zinahitaji kupatiwa ufumbuzi wa kina kwa kuibua mikakati ya kichungaji kwa ajili ya utume na maisha ya familia katika ulimwengu mamboleo. Kuna umuhimu wa kujenga msingi wa utamaduni wa ndoa na familia unaofumbatwa katika uelewa wa kitaalimungu na unaogusa mabadiliko msingi yanayoendelea kujitokeza katika maisha ya watu; kwa kuzingatia utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Ni mwaliko kwa wanandoa kutumia nguvu zao zote katika kujenga na kuimarisha misingi na tunu bora za maisha ya ndoa na familia, kwa kutambua kwamba, mwanaume na mwanamke wanategemeana na kukamilishana katika dhamana na utume wa ndoa kama Sakramenti. Askofu mkuu Paglia anasema, Roho wa Bwana anatekeleza kazi zake hata nje ya mipaka, maisha na utume wa Kanisa, kumbe kuna uwezekano mkubwa wa kuwa na utamaduni mpya wa maisha ya ndoa na familia hata katika ulimwengu wa utandawazi, ambako tunu msingi za maisha ya kifamilia zinakabiliana na vitisho!

Wanawake katika mchakato huu wana nafasi ya pekee kwani wao ndio wadau wakuu wanaotegemeza familia nyingi duniani, kama walezi na walimu wa tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili. Wanawake wenye imani, hekima na busara wanajenga mahusiano ya dhati ndani ya familia zao. Bila ya kuwashirikisha wanawake kwa kina na mapana mchakato wa Mama Kanisa kuibua mikakati mipya ya kichungaji kwa ajili ya maisha na utume wa Familia itakwama. Wanawake ni waathirika wakubwa katika maisha ya ndoa na familia.

Pale ndoa zinapovunjika, wanawake wanalazimika kubeba mzigo wote wa familia kwa malezi na makuzi ya watoto wao. Ni wanawake wanaokesha usiku na mchana wakiwahudumia watoto, wazee na wagonjwa katika familia, kumbe kuna haja ya kuwatambua na kuwashirikisha zaidi na zaidi katika maisha na utume wa Kanisa kwa ajili ya familia.

Askofu mkuu Vincenzo Paglia anasema, kuna haja kwa wanaume na wanawake kuwa na utambulisho makini kwani wanategemeana, kila jinsia ikiwa na nafasi yake katika kazi ya uumbaji. Kanisa halina budi kutoa mwelekeo wenye mvuto na mashiko kuhusu utambulisho wa wanawake na wanaume, kwa kutambua kwamba, linawajibu wa kurithisha imani, maadili na utu wema kwa waamini na Jamii kwa ujumla wake. Bila familia thabiti ni vigumu kuweza kurithisha tunu msingi za maisha kwa vijana wa kizazi kipya. Kutokana na ukweli huu, Uinjilishaji mpya unajikita katika tunu msingi za maisha ya kifamilia.

Mama Kanisa anapotafakari kuhusu utamaduni na mikakati bora ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya familia, kuna umuhimu wa kuwashirikisha waamini walei, kwani hawa ndio wanaoguswa kwa namna ya pekee na mipasuko, kinzani na changamoto mbali mbali za maisha ya kifamilia katika ulimwengu mamboleo. Familia zinaposambaratika, Jamii iko mashakani. Myumbo wa uchumi kimataifa na athari zake ni mambo ambayo yanaendelea kuathiri familia nyingi duniani kwa kukosa uhakika wa maisha na huduma msingi. Familia zikiyumba, Jamii nyingi zinaweza kuteleza na kuanguka!

Ni wajibu wa waamini walei kuhakikisha kwamba, kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao wanaenzi na kuzitegemeza familia zao. Utume huu unaweza kutekelezwa kwa umakini mkubwa kwa njia ya vyama vya kitume vilivyo enea ndani ya Kanisa. Askofu mkuu Paglia anasema, kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa na kimaadili, kuna haja kwa Mama Kanisa kuwekeza zaidi na zaidi katika vyama vya kitume kwa ajili ya malezi na majiundo endelevu ya familia, ili viweze kutekeleza dhamana hii nyeti kwa kuwaimaarisha wanandoa katika maisha na utume wao. Wanandoa wawe na ujasiri wa kufanya toba na wongofu wa ndani kwa makosa na mapungufu yao ya kibinadamu, wakiwa tayari kuanza upya safari ya ujenzi wa Familia kama Kanisa dogo la nyumbani, shule ya haki, upendo na ukarimu.

Ushauri uliotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, Viongozi wakuu wa Kanisa na Nyaraka mbali mbali za Mabaraza ya Maaskofu ni nyenzo msingi zinazoweza kulisaidia Kanisa Katoliki kuanzisha mchakato wa mikakati ya shughuli za kichungaji kwa familia katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Waamini wanasubiri anasema Askofu mkuu Vincenzo Paglia kusikia Kanisa likifafanua kwa kina na mapana kuhusu: Haki msingi za Familia, Haki ya Kazi na Mapumziko, pamoja na Zawadi ya Uhai. Kuna changamoto nyingi zinazopaswa kufanyiwa kazi katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo; changamoto ambazo kwa hakika zinahitaji hekima na busara ili kufanya upembuzi yakinifu wa maisha na utume wa ndoa na familia; Injili ya Maisha dhidi ya Utamaduni wa Kifo!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.