2013-11-09 15:30:24

UNITALSI ni kielelezo makini cha ushuhuda wa imani tendaji katika matendo ya huruma kwa wagonjwa!


Miaka 110 iliyopita, ulikuwa ni mwanzo wa hija ya imani, matendo ya huruma na majiundo makini katika maisha na utume wa Kanisa miongoni mwa wagonjwa. UNITALSI, ambao ni Umoja wa Kitaifa wa Wasafirishaji wa wagonjwa Lourdes na kwenye Madhabahu ya Kimataifa ni juhudi zilizoanzishwa na kunako mwaka 1903 na Giovanni Battista Tomassi, wakati alipokuwa anakaribia kukata tamaa ya maisha kutokana na kuandamwa mno na magonjwa, aliamua kufanya hija ya maisha ya kiroho mjini Lourdes, Ufaransa, hapo ndipo alipoonja matendo makuu ya Mungu katika maisha yake.

Kwa maombezi ya Bikira Maria wa Lourdes akaongoka na hivyo kufanikiwa kuguswa na kweli za maisha ya Kikristo. Aliporudi nchini Italia, akaandika Katiba ya UNITALSI na huo ndio ukawa ni mwanzo wa UNITALSI kuanza kuenea kwa kasi ya ajabu nchini Italia. Hiki ni kielelezo makini cha ushuhuda wa imani tendaji katika matendo ya huruma yanayojionesha katika Parokia na Majimbo mengi nchini Italia.

Ni maneno ya Kardinali Tarcisio Bertone, Camerlengo wa Kanisa Katoliki, katika Ibada ya Misa Takatifu iliyoadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumamosi, tarehe 9 Novemba 2013, kama sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 110 tangu UNITALSI ilipoanzishwa.

Tangu wakati huo, wadau mbali mbali wameshiriki kikamilifu katika maandalizi pamoja na kuwasindikiza wagonjwa si tu katika Madhabahu ya Kimataifa, bali hata katika hija ya maisha yao ya kila siku. Kanisa lina kila sababu ya kumshukuru Bikira Maria msaada wa wagonjwa kwa mafanikio makubwa yaliyokwisha kupatikana katika kipindi cha miaka 110 iliyopita.

Kardinali Bertone anasema kwamba, kumwongokea Mungu ni mwanzo wa maisha mapya na kwamba, waamini wanapaswa kutambua kuwa miili yao ni Hekalu la Roho Mtakatifu, kama ilivyokuwa kwa Yesu, ishara wazi ya uwezo wa Mungu kati ya watu wake. Wagonjwa ni sehemu ya Fum bo la Mwili wa Kristo. Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, katika Ibada ya kuabudu Ekaristi Takatifu, waamini kwa jicho la imani wanayaona Madonda Matakatifu ya Yesu kwa njia ya ndugu zake wagonjwa, wanaopaswa kusikilizwa na wafuasi wa Kristo.

Kardinali Bertone anasema, miaka 110 imekuwa ni ushuhuda wa wadau mbali mbali katika azma ya kusikiliza kwa makini wagonjwa, kwa kutambua kwamba, maisha ni fumbo linalohitaji uwajibikaji wa dhati, huruma, upendo na uvumilivu kutoka kwa kila mtu. Lakini jambo hili si rahisi kwa watu wengi, ndiyo maana kunahitajika ujasiri unaofumbatwa katika msingi wa imani, ili kuweza kupokea kwa matumaini magonjwa katika maisha, kwa kumuiga Kristo aliyeteseka, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Kardinali Bertone amewakumbusha wagonja na wahudumu wao kwamba, ushiriki wao mkamilifu katika Ibada ya Misa Takatifu ni mchakao wa kujimwilisha katika Fumbo la mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Hii ni Sadaka endelevu ya Kristo Msalabani aliyeshinda dhambi na mauti kwa nguvu ya upendo wake wa Kimungu. Shule ya Ekaristi Takatifu inawafunda waamini kupenda na kuthamini zawadi ya uhai hata katika hali ya magonjwa na kifo!

Kardinali Tarcisio Bertone, Camerlengo wa Kanisa Katoliki anahitimisha mahubiri katika Maadhimisho ya Miaka 110 ya UNITALSI kwa kuwataka wagonjwa kumkimbilia Bikira Maria ili aweze kuwaombea kwa Kristo ili waweze kubeba pamoja na Kristo Msalaba wa mateso na mahangaiko yao.







All the contents on this site are copyrighted ©.