2013-11-08 08:54:49

Baba Mtakatifu Francisko asikiliza na kujibu kilio cha wananchi wa Kenya!


Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum, hivi karibuni alizindua Hospitali inayomilikiwa na kuendeshwa na Shirika la Masista wa Katekesi wanaotekeleza utume wao Jimboni Eldoret, nchini Kenya.

Sherehe hizi zimehudhuriwa na Askofu mkuu Charles Daniel Bavo, Balozi wa Vatican nchini Kenya pamoja na viongozi wa Kanisa kutoka Jimboni Eldoreti. Hizi ni juhudi za Baba Mtakatifu Francisko kuhakikisha kwamba, Kanisa linasikiliza kilio cha maskini na kujitahidi kujibu kwa njia ya matendo ya huruma kama kielelezo cha imani tendaji.

Katika mahojiano na Gazeti la L'Osservatore Romano linalomilikiwa na kuendeshwa na Vatican, Monsinyo Segundo Tejado Munoz, Katibu mkuu msaidizi wa Cor Unum anasema, Baraza hili ni kielelezo cha mshikamano wa upendo unaooneshwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa watu wanaokabiliana na majanga mbali mbali ya maisha, pamoja na kusaidia mchakato wa kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la umaskini, ujinga na maradhi.

Huduma ya upendo wa Baba Mtakatifu inachangiwa na Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Kanisa Katoliki limeendelea kuwa ni mdau mkubwa katika maboresho ya huduma ya afya ya jamii kwa miaka mingi. Hii ni sehemu ya Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima kama alivyowahi kusema Papa Paulo wa sita.

Huduma ya afya inayotolewa na Kanisa Katoliki Barani Afrika inajikita zaidi vijijini, huduma kwa mama na mtoto, wazee na hasa waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi. Hii ndiyo picha inayojionesha pia Jimboni Eldoreti, nchini Kenya. Hospitali ya Trinity Mission Hospital iliyoko Jimboni humo pamoja na mambo mengine inapania kutoa huduma kwa Jamii ya wafugaji ambayo inakabiliana na changamoto nyingi za huduma za Kijamii.

Mradi wa Hospitali hii ni cheche za matumaini kwa wananchi wa Eldoreti kama kielelezo cha mshikamano na maskini katika mapambano dhidi ya magonjwa bila ugabuzi. Cor Unum inasema, Bara la Afrika bado linaendelea kuhifadhi tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kitamaduni zinazoweza kuhamasisha mchakato wa Uinjilishaji mpya sehemu mbali mbali za dunia. Barani Afrika familia inayoundwa kati ya Bwana na Bibi bado inapewa kipaumbele cha kwanza, ikilinganishwa na "majanga" yanayoendelea kujitokeza Barani Ulaya na Amerika.

Afrika bado inaendelea kujikita katika utamaduni wa maisha, licha ya utamaduni wa kifo unaoanza kujipenyeza kwa njia ya sera za utoaji mimba kama sharti la kupokea misaada ya maendeleo ili kupambana na umaskini. Baba Mtakatifu Francisko ana matumaini makubwa kwa Kanisa Barani Afrika na kwamba, litaendelea kuchungia kwa hali na mali katika maendeleo na ustawi wa Kanisa la kiulimwengu licha ya changamoto zilizoko mbele yake.

Misimamo mikali ya kidini na vitendo vya kigaidi ni kati ya mambo ambayo yanapaswa kusimamiwa kidete ili kuhakikisha kwamba, haki msingi za binadamu zinalindwa na kuheshimiwa; watu wanaweza kutekeleza uhuru wa kuabudu bila woga wala wasi wasi wa kuvamiwa. Mashambulizi ya kidaidi yanaendelea kujenga hofu na wasi wasi miongoni mwa wananchi wengi Barani Afrika.

Mauaji ya kinyama yaliyofanyika Westegate, mjini Nairobi na kupelekea zaidi ya watu 60 kupoteza maisha ni jambo la kusikitisha sana. Madhulumu ya kidini bado yanaendelea pia kujionesha nchini Somalia na Tanzania, nchi ambayo kwa miaka mingi ilifurahia amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa, kwa sasa misingi hii inaanza kusambaratika taratibu kadiri siku zinavyokwenda!

Cor Unum inayapongeza Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki yanayotekeleza dhamana na wajibu wake katika kambi za wakimbizi zilizoenea sehemu mbali mbali za Afrika, lakini kwa namna ya pekee nchini Kenya. Kambi ya Wakimbizi ya Dadaab, iliyokuwa na uwezo wa kutoa hifadhi kwa wakimbizi 90, 000 kwa sasa inahifadhi watu zaidi ya 450,000. Hii ni kambi kubwa ya wakimbizi kuliko zote duniani. Kambi hii inakabiliwa na changamoto nyingi zinazopaswa kufanyiwa kazi na Jumuiya ya Kimataifa kwa kushirikiana na wadau mbali mbali.

Ukame wa kudumu Kaskazini mwa Kenya ni changamoto nyingine katika kuwahudumia wakimbizi. hali ya usalama kwa wafanyakazi wa Mashirika ya Misaada Kitaifa na Kimataifa si shwari sana kwani kila wakati wanakabiliana na kifo mbele yao! Kanisa Katoliki nchini Kenya linatekeleza wajibu wake barabara katika medani za kidiplomasia na utoaji wa misaada ya kiutu katika mchakato wa kutafuta suluhu ya kudumu na kwa ajili ya mafao ya wengi!







All the contents on this site are copyrighted ©.