Wakristo wanaalikwa kujenga ushirika kamili na Kristo kwa njia ya Sakramenti, karama
na mapendo ili kuishi wito wao vyema!
Baba Mtakatifu Francisko katika Katekesi yake iliyopita, alitafakari kuhusu ushirika
wa watakatifu, kama kielelezo cha mshikamano na watakatifu. Akiwa kwenye Uwanja wa
Kanisa kuu la Mtakatifu Petro uliokuwa umefurika na umati wa watu, Jumatano tarehe
6 Novemba 2013 amegusia ushirika katika mambo ya kiroho yaani: ushirika katika imani,
ushirika wa Sakramenti, ushirika wa karama pamoja na ushirika wa mapendo kama unavyofafanuliwa
na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki.
Baba Mtakatifu anasema, ushirika wa
Sakramenti ni kielelezo makini cha mshikamano miongoni mwa waamini kinachowasaidia
kukutana na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia na kwa njia yake, wanawezeshwa kukutana
na ndugu zao katika imani. Kwa njia ya Sakramenti za Kanisa yaani Ubatizo, Kipaimara
na Ekaristi Takatifu mwamini anashirikishwa kwa Kristo pamoja na Jumuiya ya waamini,
kwani Kanisa linatengeneza Sakramenti na Sakramenti zinaliunda Kanisa na hivyo kuwaunda
Watu wa Mungu kwa kuimarisha utambulisho wao.
Kila wakati waamini wanapokutana
na Yesu kwa njia ya Sakramenti Yeye mwenyewe anawakirimia wokovu na kuwatuma kuwashirikisha
wengine wokovu huo ambao wamebahatika kuuona, kuugusa, kukutana nao na kuupokea kwani
hiki ni kielelezo cha upendo. Sakramenti zinawahamasisha waamini kuwa ni Wamissionari
wanaotumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu katika medani mbali mbali za maisha, ili
kuwashirikisha watu mpango wa ukombozi kutoka kwa Mwenyezi Mungu anaopania kuwashirikisha
wote. Sakramenti zinawaimarisha waamini katika imani na furaha ili kuweza kuyashangaa
matendo makuu ya Mungu pamoja na kusimama kidete kupinga miungu ya dunia hii.
Baba
Mtakatifu anasema kwamba, ushirika wa karama ni zawadi ya Roho ya Mtakatifu katika
maisha ya kiroho kwa ajili ya ujenzi wa Kanisa na mafao ya Watu wa Mungu, mwaliko
na changamoto ya kuishi kwa uaminifu karama hizi za Roho Mtakatifu kwa ajili ya huduma
kwa Jumuiya husika. Karama hizi ni muhimu sana katika mchakato wa utakatifu na utume
wa Kanisa. Kila mwamini anaalikwa kuheshimu karama zake na zile za wengine kwa ajili
ya mafao na ustawi wa Kanisa.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, ushirika wa mapendo
ni muhimu sana katika maisha ya Jumuiya ya Kikristo na kwamba, ni njia ya kukua katika
upendo, kwa kushiriki katika furaha, mateso na mahangaiko ya wengine pamoja na kuthubutu
kusaidia kubebea mizigo ya maisha ya maskini na wanyonge ndani ya Jamii. Mshikamano
huu ni kiini cha cha umoja miongoni mwa Wakristo. Ni sakramenti na kielelezo cha upendo
wa Mungu kwa ajili ya wote kwa kuguswa na furaha na mahangaiko ya jirani.
Baba
Mtakatifu anasema, kwa bahati mbaya, waamini wanajikuta wakiwa baridi pamoja na kutoguswa
na mahangaiko ya wengine badala ya kuwashirikisha upendo wa kidugu, wanatema cheche
za machungu na masikitiko, ubaridi na ubinafsi. Baba Mtakatifu anawaambia waamini
na watu wenye mapenzi mema kwamba, Yesu anawaalika kujenga ushirika kamili pamoja
naye kwa njia ya Sakramenti, Karama na Mapendo, ili kuishi mintarafu wito wa maisha
ya Kikristo.
Baba Mtakatifu alipata fursa ya kuzungumza na mahujaji kutoka
sehemu mbali mbali za dunia ambao tangu alfajiri na mapema walianza kujaza pole pole
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Ametumia fursa hii kuwashukuru
wote kwa matendo makuu yanayojionesha kwa njia ya uwepo wao mjini Vatican. Amewapongeza
Mapadre kutoka Uingereza wanaofanya Jubilee ya maisha na wito wa Kipadre. Anawaalika
waamini kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake katika medani mbali
mbali za maisha.
Baba Mtakatifu anaendelea kuwakumbusha waamini kwamba, Mwezi
Novemba, Mama Kanisa anawakumbuka na kuwaombea waamini marehemu ili waweze kuonja
huruma na upendo wa Mungu. Waamini wanahimizwa kutembelea na kusafisha makaburi.
Msalaba
wa Kristo ni alama na kielelezo cha upendo, huruma, upatanisho na matumaini. Anawataka
waamini kuendelea kujichotea matumaini na nguvu wanayohitaji katika utekelezaji wa
dhamana yao ya kitume miongoni mwa ndugu zao katika Kristo. Amewatakia wote baraka
zake za kitume!