2013-11-06 07:42:37

Kuelekea Bagamoyo! Simameni kidete kutangaza na kumshuhudia Kristo kwa maneno na matendo! Msikatishwe tamaa!


Askofu mkuu Paul Ruzoka, Mwenyekiti wa Tume ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano na Radio Vatican anasema, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani nchini Tanzania yamekumbana na changamoto na kinzani za kidini hasa Zanzibar ambako kimsingi ni Mlango wa Imani kwa Waamini wa Kanisa Katoliki Afrika Mashariki. RealAudioMP3

Uvunjifu wa misingi ya haki, amani na utulivu ni dosari kwa watu wote wenye mapenzi mema na kwamba, vitendo hivi vimesababisha hofu na mashaka kwa Wakristo Visiwani Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kwani vitendo hivi vinagusa haki msingi juu ya uhuru wa kidini. Vitendo hivi vinapaswa kudhibitiwa na vyombo vinavyohusika na wahalifu wapelekwe mbele ya sheria, ili sheria iweze kushika mkondo wake. Wananchi wajenge utamaduni wa kuheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana kama sehemu ya mchakato wa kujenga na kudumisha amani, utulivu, upendo na mshikamano wa kidugu.

Askofu mkuu Ruzoka anasema, pamoja na changamoto zote hizi, Wakristo wanapaswa kumakubali, kumpokea na kumshuhudia Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kwa maneno na matendo yao adili. Damu ya Wakristo inayomwagika Visiwani Zanzibar na Tanzania kwa ujumla ni kielelezo cha ukomavu wa imani na itazaa matunda kwa wakati wake.

Askofu mkuu Ruzoka anasema, wavunja sheria, amani na utulivu miongoni mwa jamii wasionewe soni! Wakamatwe na kufikishwa mbele ya sheria ili amani na utulivu viweze kurejea tena. Serikali ina wajibu wa kuhakikisha kwamba, inasimamia kwa ukamilifu haki msingi za binadamu na kwamba, kila mtu anahitaji amani na utulivu katika kutekeleza mikakati ya maisha. Kumbe, wenye dhamana hii wasifanye mchezo, Tanzania inaweza kujikuta inatumbukia kwenye "majanga".







All the contents on this site are copyrighted ©.