2013-11-05 09:11:31

Maaskofu Katoliki Tanzania waridhia MWUCE kuanza mchakato wa kuwa ni Chuo Kikuu Kamili!


Hotuba ya mkuu wa chuo kwenye mahafali ya 6 ya Chuo Kikuu Kishiriki cha Ualimu Mwenge (Chuo cha Mt. Augustino cha Tanzania), iliyotolewa na Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania.

Mhashamu Askofu Isaac Amani – Askofu Jimbo Katoliki Moshi na Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu – Mwenge,
Mheshimiwa Padre Daktari Pius Mgeni – Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mt. Augustino Tanzania,
Waheshimiwa Wajumbe wa Bodi ya Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu – Mwenge,
Mheshimiwa Padre Daktari Philbert Vumilia – Mkuu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu – Mwenge,
Waheshimiwa Wakuu wa Vyuo na wageni mbali mbali mliopo hapa,
Waheshimiwa Wahadhiri wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu – Mwenge,
Waheshimiwa Wanachuo mnaohitimu leo,
Waheshimiwa wanachuo mnaobaki,
Wafanya kazi wote wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu – Mwenge,
Mabibi na Mabwana,

Utangulizi
Tumeanza sherehe za leo kwa ibada ya Misa Takatifu tukimshukuru Mungu kwa fadhila na baraka zake kwa wahitimu wetu wa mwaka huu. Tunapoingia katika sehemu hii ya pili ya adhimisho la siku ya leo napenda kuchukua nafasi hii kwanza kabisa kuwakaribisha Mababa Askofu na wageni wote katika mahafali haya ya leo. Karibuni sana.
Katika ghafla hii ya kuwatunukia wahitimu vyeti vyao kwa pamoja tunakuja kuwapongeza kwa jitihada na uvumilivu wao hata kufikia katika kilele cha azma yao ya kufuzu katika masomo. Mwanadamu mtu mzima anapopangilia maisha yake anakuwa na lengo na linapokamilika hana budi kufurahi. Ikiwa lengo ni kubwa pia mahitaji ya kulifikia au kulitekeleza nayo yanakuwa makubwa na kwa kadiri hiyo mtu atahitajika kuwa makini katika kuliendelea lengo lenyewe. Katika juhudi za kufikia malengo changamoto hazikosekani na hata vipingamizi.

Mara nyingi vipingamizi vya kuendelea vinatokana na wahusika wenyewe kutozingatia mafunzo na matokeo yake kushindiwa njiani. Leo tunaadhimisha ushindi siyo kushindwa na kwa sababu hiyo ni siku ya kuwashangilia wahitimu wetu. Chuo cha Mwenge kinaona fahari kuwatunukisha vyeti wahitimu mia nne sabini na sita ambao kwa mwaka mmoja, miwili au mitatu wamejitahidi kufuata mafunzo na hivyo kukidhi viwango vya ufaulu vinavyotarajiwa. Chuo cha Mwenge daima kimewania kutayarisha wataalamu wenye maadili mema, wenye kujituma na walio na moyo wa kujenga Taifa la Tanzania.

Maadili ni chachu ambayo inapatikana kwa upungufu sana katika nchi yetu kwa sasa. Kelele nyingi zinazosema “Ufisadi, wizi wa mali za umma, n.k.” ni dalili tosha za maadili kushuka. Lengo la Chuo chetu ni kuchochea na kujenga maadili mema yaliyo ndani ya mioyo ya mwanadamu ili mwanadamu aweze kuishi maisha manyofu na ya kujali jamii kwa ujumla wake na majirani kwa upeke peke katika maisha ya kila siku. Nchi inashikwa na simanzi kwa sababu ya ubinafsi ambao unapelekea kupenda mali kuliko kujenga jamii inayojaliana na kupendana.

Tabia na maisha ya Kiafrika yalifunza na kusisitiza sana maisha ya pamoja na kusaidiana lakini mwelekeo wa walio wengi leo ni kupata mali kwa haraka na bila kujali yanavyopatikana. Hali hiyo inaleta fujo katika maisha ya jamii na hadi kupelekea kutoaminiana na mwisho kupigana ndugu na ndugu na jirani na jirani mwenzake. Hayo ni kati ya mambo ambayo tunatazamia kwamba wasomi wetu wakiwemo wahitimu wetu wa leo wataenda kuyapiga vita ili maisha ya Mtanzania yawe ya kujali, kutumikia kwa upendo na kufanya kazi kwa weledi kulingana na mbinu na taratibu zilizopo.

MWUCE na Elimu
Kwa wale wageni ambao hawaifahamu MWUCE niseme tu kwa ufupi kwamba ilikuwa azma ya Baraza la Maaskofu katika Kikao chake cha 1994 kwamba Chuo Kikuu cha Mt. Augustino Tanzania kianzishwe Mwanza na kiwe na vyuo vishiriki vitatu yaani: Bugando kwa ajili ya mafunzo ya udaktari, MWUCE kwa ajili ya Elimu na Ruaha kwa ajili ya sheria na Kompyuta. Hayo yamefanyika kwa utaratibu huo na kuongeza vyuo vingine nane hadi sasa. Mwenge tangu awali imejishughulisha na kutayarisha walimu wa masomo ya Sayansi na inafahamika hivyo. Tunayo pia masomo ya Sanaa na masomo mengine ambayo yameanzishwa kwani wajibu wa chuo kikuu ni kufundisha masomo mbali mbali lakini kila chuo kina eneo maalumu kinapojikita.

MWUCE imeendelea kuimarisha eneo la utayarishaji wa waalimu jambo ambalo ni moja ya mahitaji makubwa Kitaifa. Nchi inapohangaika na tatizo la ufaulu mdogo wa wanafunzi katika shule za msingi na sekondari Chuo cha Mwenge kinaguswa sana na jambo hilo kwani mchango wake kwa jamii hutokana na idadi ya wanachuo wanaohitimu na kwenda kufundisha mashuleni.

Ninatambua kwamba tangu kuwepo kwa Chuo cha Mwenge kimekuwa kinaendesha warsha za kusaidia walimu wa sekondari kuimarisha taaluma zao za ualimu. Mwaka huu nimesikia kwamba licha ya kuendesha warsha hiyo chuoni kama ilivyo utaratibu wa kawaida pia Chuo kikishirikiana na wadau wengine kimeamua kusogeza huduma hiyo karibu na walimu na wanafunzi na hata kupanua eneo kwenye sekondari 40 katika Wilaya 7 za Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara. Haya yote ni katika jitihada za kuchangia katika kukuza elimu nchini.

Aidha MWUCE imeendelea kuimarisha Programu yake ya ualimu kwa kuanzisha shahada ya Uzamili ambapo wanachuo kumi na mmoja watahitimu siku hii ya leo. Huu ni mchango wa Kanisa katika kuimarisha elimu nchini na hatutasimamia hapo bali utaratibu ni kuongeza idadi ya wanafunzi wanaojiunga na Chuo mwaka hadi mwaka ili tuwe na wataalamu wengi zaidi katika Taifa letu.
Jambo ambalo daima jamii inatarajia kutoka MWUCE na ndicho ninachoamini kinafanyika, ni wakufunzi kuimarisha ufundishaji ili wahitimu watoke wakiwa wameiva vizuri. Wanafunzi huomba kujiunga na chuo ili kusudi waje kusoma lakini lengo kuu la mbeleni ni kupata ajira. Ajira ya mhitimu itakuwa na umaana kwake na kwa jamii kama mwajiriwa huyu atakuwa na nyenzo za kutimiza kazi yake vizuri. Hapo awali nimezungumzia kuhusu maadili mema lakini mhitimu anahitaji pia awe amesoma na kuelimika vizuri kuweza kukidhi mahitaji ya ajira. Hivyo ni wajibu wa wahadhiri na wanachuo kuwania kufanya kazi kwa pamoja kwa nia ya kumtayarisha mtaalamu mahiri wa baadaye. Kama mwanachuo kazania kile unachokisoma ili uwe mtaalamu hodari. MWUCE ipo ikuongoze na kukufundisha siyo kwa elimu ya kitabuni peke yake bali pamoja na mafunzo kwa vitendo.

Mafunzo kwa vitendo kwa upande wa MWUCE yamepewa kipaumbele sana ili kusudi wanachuo wakiwa mafunzoni waanze kujijengea ujuzi wa kazi wanayoisomea. Kwa wale wa ualimu najua kwamba wanaenda kufanya ufundishaji “Teaching Practice” – zoezi hili mahali pengi limechukuliwa kama utaratibu wa kawaida wa kumpatia mwanachuo alama baada ya ukaguzi wa mazoezi yanayofanywa na wahadhiri wa Chuo. Kwa upande wa MWUCE zoezi hili ni la muhimu sana na hivyo linapewa uzito maalumu.

Ninajua kwamba Mwenge imeanzisha utaratibu siyo tu wa wahadhiri kuwatembelea wanachuo kwenye shule wanakofanyia mazoezi bali pia wamechaguliwa waalimu wa sekondari walio wazoefu wa kutembea na wanachuo walioko mazoezini wakiwashauri katika hiyo safari yao. Utaratibu huo unalenga kuwajengea wanachuo uwezo na utaalamu ambao utawasaidia kufundisha kwa umakini na umahiri waingia kwenye ajira. Tafadhali zingatieni hayo mliyoyapata kusudi hayo mliyoyasoma yasaidie jamii.

Pia kwa masomo mengine yasiyo ya ualimu mnakuwa na mazoezi kwenye maeneo mbali mbali ili kujipatia utaalamu na kuimarisha ujuzi. Zingatieni hayo ili mnapomaliza hayo mliyojifunza yawe nyenzo ya kufanya kwa ufanisi katika ajira yenu.

Changamoto
Uendeshaji wa vyuo vya elimu ya juu unazo changamoto nyingi na hasa katika kipindi hiki. Baraza linatambua changamoto hizo zikiwemo:
    Ufaulu mdogo wa wanafunzi wanaomaliza kidato cha sita na hivyo kufanya idadi ya wanafunzi wanakidhi viwango vya kujiunga na vyuo kuwa ndogo
    Mikopo kwa ajili elimu ya juu kutopatikana kwa ajili ya wanachuo wa programu zote kunafanya wanafunzi wengine kushindwa kujiunga na chuo
    Gharama za uendeshaji wa vyuo vikuu kuwa kubwa
    Uwepo wa wanachuo vyuoni wasiotilia mkazo masomo badala yake kufuata maisha ya anasa na starehe na hivyo kutofaulu vizuri kwenye masomo yao

Hayo ne mengine mengi yamekuwa ni changamoto kwenye vyuo na pia kwa wanafunzi vyuoni. Yale ambayo Mwenye Chuo ana uwezo nayo ataendelea kuyashughulikia ikiwa ni pamoja na kuuhimiza uongozi wa MWUCE kuongeza programu za Certificate na Diploma ili vijana wengi waweze kujiunga na Chuo chetu. Aidha tutaendelea kuwasiliana na serikali yetu kuhusiana na uwezekano wa mikopo kutolewa kwa wanafunzi wote wanaopokelewa vyuoni. Kwa upande wa wanachuo napenda kuweka msisitizo kwamba nia ya Kanisa ni kutayarisha wataalamu walio na maadili mema. Pendeni kuwa na tabia njema ambazo zitakubalika kwenye jamii.

Maamuzi ya Baraza la Maaskofu kuhusu MWUCE
Chuo cha Mwenge kimeanza kutoa mafunzo ya shahada mwaka 2005/06 hivyo sasa kiko kwenye mahafali ya sita. Kwa hiyo miaka saba Chuo kimekua hadi kufikia hatua tunayoiona sasa. Idadi ya wanachuo imeongezeka kutoka wanafunzi 58 (31 shahada na 27 stashahada) mwaka 2005/06 hadi 1,960 mwaka 2012/13. Katika kukua huko pia idadi ya wahadhiri, majengo na vifaa vya kujifunzia na kufundishia vimeongezeka kulingana na idadi ya wanachuo. Hayo yote yanaonesha kukua kwa Chuo. Kutokana na maendeleo hayo na kulingana na kukua kwa Chuo Kikuu cha Mt. Augustino Tanzania (kwa sasa kina vyuo vishiriki na vituo (Centres) 12) Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania limeona ni muda mwafaka wa Chuo Kiuu Kishiriki cha Mwenge (MWUCE) kianze mchakato wa kuwa Chuo Kikuu kamili. Tayari Mkuu wa Chuo Padre Philbert Vumilia alishapata barua ya maelekezo na kwa sababu hiyo nawaalika muombee utaratibu huu ufanikiwe.

Nia ya kuazimia Chuo hiki kiwe Chuo Kikuu kamili ni kusudi kiendelee kuimarisha yale ambayo tumeshayaona kuwa na mazuri na ya kuijenga jamii ya Tanzania. Hivyo matarajio ya Baraza ni kwamba Elimu itaendelea kuimarishwa na wahitimu wa Chuo hiki waende kuwa MWANGA kama kauli mbiu ya Chuo hiki inavyodai. Baraza la Maaskofu Tanzania liko tayari kusaidia kwa kila njia kuhakikisha kwamba Chuo chetu kinaendelea kutoa elimu bora ya kuwafaa watanzania.

Nawaasa tena wahadhiri na wanachuo mnaobaki muendelee kujiimarisha ili Chuo kiweze kufikia malengo yake ambayo ni kufundisha, kutafiti na kutoa huduma kwa jamii. Daima simamieni kile kitakachojenga jamii kwa uzalendo na nia njema. Maadili mema pamoja na kuaminiana kutawale maisha yenu ili kila mnachokifanya kilete maendeleo kwa watu.

Kwa wahitimu wetu, nawapongeza tena kwa hatua mliyofikia mkijua kwamba hatua moja huvuta hatua nyingine. Nendeni mkahudumie mkiwa mabalozi wazuri wa MWUCE. Kile mlichokisoma hapa mkakiishi na kukishirikisha kwa wengine. Nanawatakia wingi wa baraka katika maisha yenu.

Mwisho, napenda kuwashukuru jumuiya yote ya MWUCE kwa shughuli zote wanazozifanya kukifanya Chuo chetu kiendelee kukua. Ahsanteni sana. Nawatakieni wingi wa baraka katika huduma zenu mkijua kwamba Baraza la Maaskofu liko nanyi.

Ahsanteni sana, Mungu awabariki.
Mhashamu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa
Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Mt. Augustino Tanzania








All the contents on this site are copyrighted ©.