2013-11-04 14:51:03

Mshikamano wa kidugu na ushuhuda kwa Roho Mtakatifu ni mwelekeo mpya katika maisha na utume wa Makanisa!


Wajumbe wa mkutano mkuu wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, Jumatatu tarehe 4 Novemba 2013 wamekazia umuhimu wa kuonesha mshikamano wa kidugu katika maisha na katika utekelezaji wa utume na dhamana ya Kanisa katika Uinjilishaji; kwa kuangalia kwa pamoja changamoto zinazojitokeza katika Uinjilishaji katika ulimwengu mamboleo.

Wajumbe hao kimsingi wamekubaliana na hati ya mkutano iliyoandaliwa na Kamati Utume na Uinjilishaji ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika kikao chake cha Mwezi Septemba, 2012 kilichofanyika nchini Ugiriki. Hati hii pamoja na mambo mengine inatoa mwelekeo wa Kibiblia, Sala na Nyimbo zinazoweza kutumika katika kuhamasisha mchakato wa Uinjilishaji unaofanywa na nchini wanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni.

Wajumbe wanakazia umuhimu wa kushirikiana kwa pamoja kama ndugu kama kielelezo cha umoja katika Roho Mtakatifu pamoja na kuhakikisha kwamba, Kanisa linawajali na kuwahudumia wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kimsingi wajumbe wanayataka Makanisa kushikamana kama njia ya kutolea ushuhuda amini katika maisha na utume wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo.







All the contents on this site are copyrighted ©.