2013-11-04 14:23:55

Madonda matakatifu ya Yesu ni kielelezo cha huruma na tumaini la maisha ya uzima wa milele!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 4 Novemba 2013 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea Marehemu Makardinali na Maaskofu waliofariki dunia katika kipindi cha Mwaka 2013, kutoka sehemu mbali mbali za dunia hasa katika Mwezi Novemba, uliotengwa na Mama Kanisa kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea Marehemu, ili waweze kupata tuzo waliloahidiwa watumishi wema na waaminifu.

Mtakatifu Paulo anawaandikia Warumi akisema, kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyochini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kuwatenga na upendo wa Mungu, ulio katika Kristo Yesu, Bwana wao! Upendo wa Mungu ndicho kielelezo cha matumaini na imani ya Kikristo.

Hakuna jambo lolote linaloweza kuwatenga waamini kutoka katika upendo wa Kristo, aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya wokovu wa walimwengu, changamoto kwa waamini kumpokea kwa imani thabiti, ili kuendeleza mapambano ya maisha ya kila siku.

Baba Mtakatifu katika mahubiri yake anaendelea kusema kwamba, ni dhambi peke yake inayoweza kuharibu upendo wa Mungu, lakini utimilifu wa upendo wa Mungu kwa waja wake unajionesha kwa namna ya pekee kwa kukutana na hatimaye kuonana na Muingu uso kwa uso, kwani maisha adili hapa duniani yanafungua mlango wa matumaini ya maisha baada ya kifo.

Baba Mtakatifu anasema, waamini ambao wamejitahidi kuishi kikamilifu na kutekeleza wajibu wao barabara kwa ajili ya Kanisa, hapana shaka kwamba, wako mikononi mwa Mwenyezi Mungu, anayewapokea na kuwalinda; kielelezo cha heshima na uaminifu. Hili ndilo tuzo wanalostahili viongozi hawa wa Kanisa waliojitosa kimasomaso kwa ajili ya huduma kwa Mungu na jirani zao, sasa wako mikononi mwa Mwenyezi Mungu.

Wote wamehifadhiwa dhidi ya mauti; ni watu ambao wameyasimika maisha yao katika furaha na mahangaiko; katika matumaini na magumu ya maisha; huku wakiendelea kuwa waaminifu kwa Injili na ari ya kuokoa roho za watu, sanjari na kutunza mali ya Kundi walilokabidhiwa kwao na Mama Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, hata dhambi za waamini ziko mikononi mwa huruma ya Mungu inayofumbatwa katika upendo. Madonda matakatifu ya Yesu ni kielelezo cha huruma na tumaini la maisha ya uzima wa milele. Hili ni tuzo linalotolewa kwa wale wanaopokea Neno la Mungu, daima wakionesha unyenyekevu kwa Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu amewakumbuka Makardinali na Maaskofu waliojitoa bila ya kujibakiza katika wito na huduma kwa Kanisa; wakapenda kama Bwana harusi anavyompenda mwanamwali wake. Baba Mtakatifu amewaweka viongozi wote hawa chini ya maombezi ya Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu, ili waweze kuwasaidia kuona Ufalme wa mwanga na amani, mahali ambapo wenye haki waliojitahidi kuwa waamifu na mashahidi wa Injili wanapoishi.







All the contents on this site are copyrighted ©.