2013-11-02 12:18:42

Utumwa mamboleo unadhalilisha: haki msingi, utu na heshima ya binadamu!


Baba Mtakatifu Francisko amekuwa akisikitishwa na kuguswa na mahangaiko ya watu sehemu mbali mbali za dunia, hasa wale wanaotumbukizwa katika utumwa mamboleo kutokana na kukithiri kwa biashara ya haramu ya binadamu. Baraza la Kipapa la taasisi za kisayansi na sayansi jamii, kwa kushirikiana na Shirikisho la Madaktari Wakatoliki Duniani wameanza semina ya kimataifa ya siku mbili, tarehe 2 Novemba na inahitimishwa tarehe 3 Novemba 2013 mjini Vatican.

Semina hii inawashirikisha wajumbe ishirini na wawili kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Hawa ni wadau wakuu katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu inayoendelea kushamiri sehemu mbali mbali za dunia. Mkutano huu unaoongozwa na kauli mbiu "Biashara haramu ya binadamu; utumwa mamboleo; udhalilishaji wa watu na Ujumbe kutoka kwa Kristo". Wajumbe wanapania kupembua hali hali ya biashara haramu ya binadamu ili kuibua mbinu mkakati wa kupambana na biashara hii kwa njia za kisayansi.

Askofu Marcelo Sanchez Sorondo anasema, biashara haramu ya binadamu ni vitendo vinavyokwenda kinyume kabisa cha utu na heshima ya binadamu na kwamba, vinakiuka haki msingi za binadamu. Hii ni biashara inayokuzwa na baadhi ya watu wenye uchu wa mali na utajiri wa haraka haraka. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanabainisha kwamba: utumwa, ukahaba na biashara ya wanawake na watoto ni matendo yanayodhalilisha utu na heshima ya binadamu na Muumba wake.

Taarifa ya Shirika la Kazi la Umoja wa Mataifa inaonesha kwamba, kati ya Mwaka 2002 hadi mwaka 2010, zaidi ya watu millioni 20.9 wamejikuta wakitumbukizwa kwenye kazi za shuruti. Kati yao wametelekezwa kwenye utalii wa ngono na biashara ya binadamu, kwa ajili ya kunyofolewa baadhi ya viungo vyao, vinavyotafutwa kwa udi na ubani katika masuala ya tiba sehemu mbali mbali za dunia.

Wachunguzi wa mambo wanasema kwamba, katika kipindi cha miaka kumi ijayo, biashara haramu ya binadamu itaweza kuvuka biashara ya dawa za kulevya na silaha duniani kutokana na faida kubwa inayopatikana kwenye biashara hii haramu ya binadamu. Biashara ya ngono ni tatizo linaloendelea kukua na kupanuka si tu kwa ajili ya nchi maskini duniani bali hata katika nchi tajiri na zilizoendelea zaidi.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema, kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya watu wanaotumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu, kwani hawa wanaamsha kwa mara nyingine tena madonda matakatifu ya Yesu. Utumwa mamboleo unadhalilisha: haki msingi, utu na heshima ya binadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.