Kanisa halina budi kuwekeza katika mitandao ya kijamii kwa ajili ya mafao ya wengi!
Waziri wa habari nchini Nigeria Bwana Labaran Maku, amelishauri Kanisa Katoliki Nchini
Nigeria kuanza mchakato wa matumizi ya njia za mawasiliano ya Jamii katika azma ya
Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Mchakato huu
uliwezeshe Kanisa pia kuziinjilisha njia za mawasiliano ya kijamii kwani kwa kiasi
kikubwa zimekuwa ni sababu ya kumong'onyoka kwa misingi ya maadili na utu wema.
Ili
kutekeleza wajibu na dhamana hii nyeti, kuna haja kwa Kanisa nchini Nigeria kuwekeza
katika majiundo makini kwa Mapadre na Watawa watakaoweza kutumia mitandao hii kwa
umakini mkubwa kama sehemu ya Uinjilishaji, kwani kwa sasa kuna idadi kubwa ya vijana
wanaoperuzi kwenye mitandao na wakati mwingine wanaambulia mitandao inayowayumbisha
katika maisha yao kijamii na kimaadili.
Kanisa lijitahidi kuwa na mitandao
hii katika taasisi zake za elimu na huduma kwa jamii na wala zisiwe kwa ajili ya viongozi
wachache tu wa Kanisa. Kwa kuwekeza katika mitandao ya kijamii, idadi kubwa ya watu
wanaweza kupata fursa ya kusikia Habari Njema ya Wokovu ikitangazwa kwao! Hii ni kutokana
na huruma na upendo wa Mungu kwa watu wake kwamba, leo hii watu wanaweza kuwasiliana
kwa haraka na kwa upesi zaidi ikilinganishwa na miaka kadhaa iliyopita.
Mitandao
ya kijamii anasema Bwana Labaran Maku inaweza kutumika kusoma Biblia, kuhubiri na
kufundisha mambo msingi ya maisha. Ikiwa kama itatumika vyema, ulimwengu unaweza kuwa
ni mahali pazuri zaidi pa kuishi. Bwana Maku ameyasema hayo hivi karibuni wakati alipokuwa
anatoa mhadhara kwenye Seminari ya Kumbu kumbu ya Bigard iliyoko mjini Enugu, Nigeria,
kwa njia ya video.