2013-11-02 11:51:34

Hali bado ni tete nchini Msumbiji!


Rais Armando Guebuza wa Msumbiji ameonesha utashi wa kisiasa wa kutaka kufanya majadiliano ya kina na Chama cha Upinzani cha RENAMO kinachoongozwa na Bwana Alfonso Dhlakama ambaye hivi karibuni ameanza tena harakati za kutaka kurudi msituni ili kuanzisha mapambano ya silaha, hali inayotishia amani na usalama nchini Msumbiji kwa sasa.

Rais Guebuza anasema, licha ya tofauti za kijeshi zilizopo, lakini Serikali ya Msumbiji bado iko wazi kwa kufanya majadiliano ili kudumisha haki, amani, utulivu, usalama na kwa ajili ya mafao ya wananchi wa Msumbiji. Chama cha RENAMO katika mikutano miwili iliyoandaliwa na Serikali kilishindwa kupeleka wajumbe kwa madai ya kwamba, kinataka watazamaji kutoka Jumuiya ya Kimataifa kushiriki.

Itakumbukwa kwamba, Msumbiji ilijipatia uhuru wake kutoka kwa Wareno kunako Mwaka 1975, lakini ikajikuta ikiingia katika vita ya wenyewe kwa wenyewe iliyositishwa kunako mwaka 1992 kutokana na juhudi zilizofanywa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, Mkataba wa amani ukatiwa mkwaju baina ya pande hizi mbili zilizokuwa zinapomana nguvu kwa njia ya mtutu wa bunduki. Rais Geubuza anasema, RENAMO itashindwa kutambulika Kikatiba ikiwa kama itaendelea kukiuka sheria na kanuni za nchi kuwasilisha madai na maoni yake.







All the contents on this site are copyrighted ©.