Tunakuletea Habari Njema ya furaha tunapotafakari pamoja Neno la Mungu katika sherehe
ya Watakatifu wote. Mama Kanisa akitaka kuhitimisha mwaka wa Kanisa kwa furaha anaona
ni vema awaoneshe watoto wake lengo la maisha ya Kikristu yaani ni kuelekea maisha
ya utakatifu, maisha ya milele mbinguni. Kumbe Mama Kanisa
amependa kila tarehe Mosi, Novemba ya kila mwaka, sherehe hii iadhimishwe katika Kanisa
zima la ulimwengu. Adhimisho hili ni mwaliko kwetu kuchuchumalia maisha yanayotimiza
mapenzi ya Mungu, maisha ya ufufuko ambayo Mtume Paulo anatuambia daima akisema basi
mkishafufuliwa mkayatazame yaliyo ya juu! Ni mwaliko wa kuwa Watakatifu. Mpendwa,
yafaa kutambua watakatifu ni akina nani? Watakatifu ni wale wanaokaa na Mungu katika
kiti chake cha enzi kadiri tusomavyo katika kitabu cha Ufunuo. Ni marafiki wa kweli
au tunaweza kusema ni marafiki wa dhati au wa kina. Ni wale ambao hula chakula pamoja
na mkuu wa familia, na hivi wanafurahi pamoja na Mungu Baba huko mbinguni. Ni
wale ambao wanasadiki katika Kristu na kuishi kadiri ya mafundisho yake, urafiki ambao
waliupata kwa njia ya ubatizo. Ni wale ambao Injili ilikuwa chakula chao cha kila
siku walipokuwa duniani na walijikabidhi katika mikono ya Mungu na kuwa mali yake.
Mpendwa mwana wa Mungu Watakatifu ni wale walioishi heri nane mafundisho ya Kristu
aliyoyatoa pale mlimani, Mt. 5:1-11 Ni wale ambao walitunza neema ya UTAKASO waliyoipokea
wakati wa Ubatizo. Ni wale ambao walimpenda Mungu kwa moyo wao wote, kwa akili yao
yote na kwa nguvu zao zote na kisha wakampenda jirani aliyeumbwa kwa sura na mfano
wa Mungu. Ni wale ambao katika ubinadamu wao walikubali mateso wakitambua na kujua
siri ya furaha watakayoipata milele, kama ambavyo Mtakatifu Paulo asemavyo: naona
kuwa mateso ya wakati huu wa sasa si kitu kamwe kama tukiyalinganisha n aule utukufu
utakaodhihirishwa kwetu! Rm 8:18 Sasa wanafurahia matunda ya msalaba wa Kristu. Kwa
kifupi ni wale walioshika vema amri kuu ya mapendo. Ili basi nasi tuweze kufikia
hali hiyo iliyo heri na furaha upeo, somo la kwanza linaweka mwaliko kwa watu wote
kuwa, ili mmoja aweze kupokea heri za milele yaani utakatifu, ni lazima kufua mavazi
katika Damu ya Mwanakondoo. Ni lazima kukinywea kikombe kimoja cha Damu Takatifu iliyo
thamani ya wokovu kwa wote. Ndiyo kusema ni kuishi kwa kutimiza mapenzi ya Mungu.
Kwa kufua mavazi katika Damu ya Mwanakondoo kunamwondoa mtu katika dhiki ya dhambi
na dhiki ya upungufu wa upendo mkamilifu. Mmoja ananyakuliwa toka taabu ya ulimwengu
geugeu na kuvikwa mavazi meupe ndiyo utakaso mkamilifu unaowezesha kuimba baraka na
utukufu na hekima na shukrani na heshima na uweza na nguvu zina Mungu wetu hata milele
na milele. Amina. Huu ni wimbo wa sifa kwa Mungu ambao unaweza kuimbwa na walio wake,
ndiyo watakatifu. Katika somo la Pili Mwinjili Yohane anasema utakatifu ni maisha
ambayo yanaanza katika ubatizo, na maisha haya ni fumbo lakini ambalo tunaweza kuliishi
kwa furaha. Maisha haya ni zawadi toka kwa Mungu ambayo lazima kuitunza. Katika hali
ya kawaida si rahisi kuuona utakatifu, lakini Yohane anasema si rahisi pia kupita
bila kusikika kwa sababu ni nguvu ya Mungu katikati ya maisha yetu. Anasonga mbele
akisema maisha ya utakatifu hayaendani na maisha ya wale waendao bado katika giza.
Ndiyo maana wakati wa Bwana, maadui wake hawakuweza kuona utakatifu na uchungaji
wake! Hivi leo wapo bado walio katika giza ambao kazi yao ni kupingana na watumishi
wa Kanisa na Kanisa zima kwa ujumla. Mwinjili Yohane, anazungumza juu ya ukweli
kwamba uko wazi sasa, na hivi Mungu hasubiri wakati ujao yaani wakati wa kufa kwetu
ili kufunua ukweli huo, bali anatupatia kweli huo sasa. Hata hivyo kukamilika kwa
maisha haya ni pale tutakapomwona Kristo uso kwa uso. Kwa kumwona uso kwa uso tutaweza
pia kutambua asili yetu katika ukamilifu wake. Katika Injili ya Mathayo tunapata
mafundisho ya Yesu mlimani yaani Heri Nane. Bwana anaonesha njia ya kufikia utakatifu,
njia ya kuishi mapenzi ya Mungu. Anaainisha namna ya kufika mbinguni, akisema, wanaheri
wale walio maskini wa roho maana ufalme wa mbinguni ni wao. Wanaheri wenye upole maana
watairithi nchi. Anazidi kukazia utakaso wa roho akisema heri wenye moyo safi maana
hao watamwona Mungu. Hizi ni baadhi ya heri nane za mlimani njia kamilifu ya kufikia
utakatifu. Kwa kuzitafakari heri nane tunaweza kusema mambo makuu mawili ni lazima
katika kufikia utakatifu. Jambo la kwanza ni kujitenga na chachu ya ulimwengu. Kumbuka
Bwana anasali na kusema tuko ulimwenguni lakini sisi si wa ulimwengu. Hii yamaanisha
kujitenga na kile kinachopingana na injili ya Bwana, na hivi kuwa maskini wa roho.
Kumbe Mkristo anapaswa ajisikie daima kinyume na mawimbi ya ulimwengu yanayopingana
na Injili. Jambo la pili ni lile la kupokea kikombe cha mateso daima na kulitangaza
jina la Bwana. Mateso haya hugeuka na kuwa furaha katika maisha ya mkristo sasa anapoishi
na baadaye. Mtakatifu lazima aoneshe sura ya Kristo mteswa na mwenye furaha kwa ajili
ya ukombozi wa ulimwengu. Mtakatifu ni lazima amwilishe Heri Nane katika maisha yake
na hivi zingae daima na kuwa kielelezo cha maisha ya upendo. Mpendwa, hiyo ndiyo
habari ya upendo mkamilifu utokao kwa Mungu kwa ajili ya watu wote, na sasa unaalikwa
kushiriki zawadi hii ya upendo bila kuchelewa tunapowashangilia watakatifu wa Mbinguni.
Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.