Maendeleo ya kiuchumi yatoe kipaumbele cha kwanza kwa binadamu!
Askofu mkuu Justin Welby wa Kanisa kuu la Cantebury ambaye pia ni kiongozi mkuu wa
Kanisa la Kiangalikani duniani anasema kwamba, mfumo bora wa uchumi na biashara hauna
budi kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu.
Askofu mkuu
Welby ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa anazungumza na wawakilishi kutoka katika
sekta ya uchumi na biashara nchini Uingereza.
Anasema, mikakati ya uchumi
na maendeleo haina budi kuwa ni sehemu ya mchakato unaopania kuhudumia mafao ya wengi
ndani ya Jamii. Wachumi na wafanyabiashara wanapaswa kutekeleza nyajibu zao ndani
ya Jamii kwa kuzingatia sheria, kanuni, maadili na utu wema; utu na heshima ya mwanadamu
vikipewa msukumo wa pekee, jambo ambalo ni kinyume kabisa na mwelekeo wa wachumi na
wafanyabiashara wengi wanaotafuta faida kubwa hata kwa gharama na mateso ya wananchi
wengi.
Ulimwengu unaendelea kushuhudia mashindano ya utajiri wa mali na vitu,
lakini ni watu wachache sana wanaothubutu kuwaonjesha jirani zao rasilimali na utajiri
waliopewa kama zawadi na Mwenyezi Mungu. Viongozi wengi wa kijamii wanamwelekeo wa
kutaka kujilimbikizia mali na utajiri kwa ajili ya mafao yao binafsi, bila kuzingatia
kanuni ya mshikamano na utu wa mwanadamu.
Changamoto kama hii pia imetolewa
na Askofu mkuu Vincent Gerard Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza,
aliyewachangamotisha wachumi na wafanyabiashara kutoa msukumo wa pekee katika kanuni
ya mshikamano unaopania kumletea mwanadamu maendeleo endelevu katika masuala ya uchumi
na biashara.
Mshikamano wa dhati ni kielelezo cha uwajibikaji unaotekelezwa
ndani ya Jamii na kama sehemu ya mchakato wa uzalishaji wa utajiri kwa njia ya uwajibikaji
mpana. Jamii inayosimikwa katika tunu hizi msingi anasema Askofu mkuu Welby inakuza
na kupanua mwelekeo wa uchumi na biashara na kwamba, mwanadamu ataheshimiwa. Changamoto
hizi zimeendelea kutolewa na Askofu mkuu Welby katika masuala ya biashara, uchumi
na maendeleo kwa kuzingatia: sheria, kanuni na maadili mema.
Mchakato huu
uwawezeshe wafanyabiashara wenye uwezo kusaidia juhudi za wafanyabiashara wadogo kutaka
kujikwamua kutoka katika athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Familia zinaweza kujiunga
na kuunda vyama vya ushirika kama mbinu ya kupambana na myumbo wa uchumi kimataifa
unaoendelea kusababisha majanga makubwa kwa familia sehemu mbali mbali za dunia. Wafanyabiashara
wanaweza kuwasaidia kwa njia ya mikopo yenye riba ndogo, wakisukumwa zaidi na kanuni
ya auni, mshikamano na upendo. Sera na Mikakati ya kiuchumi haina budi kuwalenga wanyonge
zaidi katika Jamii, ili nao waweze kuchangia katika ustawi na maendeleo yao.
Askofu
mkuu Welby anakiri kuwa, hakuna majibu ya mkato katika kutafuta suluhu ya mikopo inayotolewa
na Mabenki, lakini mikakati hii inapaswa kuongozwa na kanuni kwamba, shughuli za uchumi
na biashara hazina budi kuelekezwa kwa ajili ya kuhudumia Jamii na wala si kwa ajili
ya kuwakandamiza na kuwanyonya watu kutokana na umaskini wao!