2013-10-30 09:24:32

ECOWAS inapania kuimarisha biashara na usalama!


Jumuiya ya uchumi Afrika Magharibi, ECOWAS katika mkutano wa viongozi wake wakuu, imejadili na kupitisha maazimio yanayolenga kuboresha shughuli za kiuchumi sanjari na usalama wa raia na mali zao. Viongozi hao katika mkutano wao uliofanyika mjini Dakar, Senegal, wamepitisha kwa kauli moja kodi ya pamoja katika bidhaa zinazosafrishwa katika nchi wanachama wa ECOWAS.

Kodi hii ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya ECOWAS tangu kuanzishwa kwake kunako mwaka 1975. Lengo ni kulinda biashara zinazozlishwa na nchi wanachama wa ECOWAS. Viongozi hao pia wamekubaliana kuendeleza majadiliano ya biashara kati ya ECOWAS na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya pamoja na kufanya marekebisho ya Itifaki iliyofikiwa mjini Cotonou, kunako mwaka 2000. ECOWAS inapania pamoja na mambo mengine kuanzisha sarafu ya pamoja, ikiwezekana ifikapo mwaka 2015.

ECOWAS kwa kushirikiana na wadau wengine, inapenda kuimarisha amani, utulivu na usalama kwa kudhibiti biashara haramu ya silaha na dawa za kulevya ambayo imekuwa ni chanzo cha majanga kwa nchi nyingi za Kiafrika. Changamoto nyingine iliyojadiliwa na viongozi hawa ni uharamia unaokwamisha mzunguko wa biashara Afrika Magharibi.







All the contents on this site are copyrighted ©.