2013-10-29 09:18:28

Watumiaji wa mitandao ya kijamii ni wadau wakuu katika utangazaji wa Injili! Millioni 10 si haba!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili iliyopita katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii, amewashukuru wafuasi wake ambao hadi kufikia tarehe 26 Oktoba 2013 imefikia watu millioni 10. Mtandao wa Khalifa wa Mtakatifu Petro unaojulikana kwa anuani ya @Pontifex umepata mafanikio makubwa katika ulimwengu wa watumiaji wa mitandao ya kijamii.

Hii ni idadi ya watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaomfuata Khalifa wa Mtakatifu Petro katika ukurasa wake wa twitter unaosomeka kwa lugha tisa kwa sasa. Hispania na Kiingereza kwa sasa ndizo lugha zinazoongoza kwa kuwa na wafuasi wengi kwenye mtandao huu. Huu ni ujumbe wa maneno machache tu yanayogusa moyo na akili ya mtu.

Alikuwa ni Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa Kumi na sita, alipozindua mtandao huu wa kijamii na katika kipindi cha mwezi mmoja akawa na wafuasi wapatao millioni moja. Ujumbe huu hutumwa pia na watumiaji wa mitandao hii ya kijamii kwa marafiki, ndugu na jamaa zao, kiasi kwamba, idadi ni kubwa na inakaidiriwa kwamba, watu wamefikia walau millioni 60, tofauti na wale wanaomfuata Baba Mtakatifu moja kwa moja katika mtandao wake.

Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii, limepokea ujumbe wa idadi kubwa ya watumiaji wa mitandao ya kijamii kwa moyo wa shukrani na matumaini makubwa. Monsinyo paul Tighe anapenda kutumia fursa hii kuwashuruku watumiaji wa mitandao ya kijamii wanaoendelea kumuunga mkono Khalifa wa Mtakatifu Petro katika kueneza Ujumbe wa Imani, Matumaini na Mapendo miongoni mwa Jamii ya Kimataifa.

Watumiaji hawa wa mitandao ya kijamii wamekuwa ni wadau wakuu katika Uenezaji wa Injili, dhamana kubwa aliyokabidhiwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Kwa njia ya mitandao ya kijamii, Baba Mtakatifu Francsiko kama alivyokuwa pia mtangulizi wake Papa mstaafu Benedikto XVI anajitahidi kuhakikisha kwamba, kila wakati anawalisha watu kwa Habari Njema ya Wokovu, licha ya tofauti ya imani na misimamo ya kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.