2013-10-27 11:32:56

Ubinafsi ukizidi, familia inakosa mwelekeo wa furaha yake, Familia inayoishi imani ni mwanga na chumvi ya dunia!


Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya 30 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa ni mwaliko kwa waamini kufanya tafakari ya kina kuhusu mambo msingi yanayopaswa kuzingatiwa na Familia za Kikristo. Kwanza kabisa, familia zinapaswa kuwa ni mahali pa sala, kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa wema, ukarimu na huruma yake katika maisha yao, daima wakionesha moyo wa unyenyekevu, huku wakitambua udhaifu wao wa kibinadamu, na hivyo kuhitaji kuonjeshwa upendo na huruma ya Mungu.

Huu ndio mwelekeo uliooneshwa na mtoza ushuru anayepongezwa na Yesu katika Injili, kinyume kabisa cha Farisayo iliyejikuza kupita kiasi. Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili tarehe 27 Oktoba 2013 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa ajili ya Familia.

Baba Mtakatifu anazichangamotisha familia za Kikristo kusali kwa unyenyekevu kwa kutambua kwamba, wanahitaji kuonja uwepo wa Mungu kati yao. Familia zijifunze kusali sala za kawaida, kutafakari Neno la Mungu kusali Rozari takatifu pamoja na kuombeana.

Familia ni mahali pa kuhifadhia imani baada ya mapambano makali katika maisha kama alivyofanya Mtakatifu Paulo, aliyejitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu na kushuhudia imani kwa maisha yake, kiasi hata cha kuhatarisha uhai wake, akaguswa na kuchangamotishwa na watu wa tamaduni mbali mbali, lakini akasimamama kidete kutangaza kweli za Kiinjili bila woga! Hii ndiyo imani ambayo Mtakatifu Paulo aliyoipokea na kuirithisha kwa watu wa mataifa, kiasi cha kupambana na kinzani nyingi.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuhakikisha kwamba, wanatunza imani yao kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya ushuhuda wa maisha, ukarimu na mshikamano wa dhati. Familia za Kikristo zitambue wajibu wake wa kimissionari katika uhalisia wa maisha yake ya kila siku, ili kweli ziweze kuwa ni mwanga na chumvi ya dunia.

Baba Mtakatifu anazichangamotisha Familia za Kikristo kuhakikisha kwamba, zinafurahia imani, kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye chemchemi ya furaha na amani ya kweli; anasikiliza wanyonge wanapomkimbilia kwa moyo wa unyenyekevu na kwamba, daima yuko karibu nao! Furaha ya kweli inapata chimbuko lake si kwa vitu anavyomiliki mtu, bali kutoka katika undani wa moyo wa mtu mwenyewe na uwepo wa Mungu katika maisha yake.

Hizi ni Familia zinazoonja upendo wa Mungu unaowawajibisha kuwa wakarimu kwa jirani zao; uwepo wa Mungu unaowajengea huruma na heshima kwa wote. Ubinafsi ukikithiri, familia itakosa mwelekeo na furaha ya kweli itatoweka kama umande wa asubuhi. Lakini familia inayoishi furaha ya imani ni mwanga na chumvi ya dunia, changamoto kwa familia kuiga mfano wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Mwishoni, Baba Mtakatifu katika mahubiri yake, amewatakia wote furaha na amani inayobubujika kutoka kwa Kristo!







All the contents on this site are copyrighted ©.