Mwaka wa Imani: Kesha la Maadhimisho ya Siku ya Familia inayoishi imani!
Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi jioni tarehe 26 Oktoba 2013 katika kesha la Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani kwa ajili ya Familia, aliwaalika wanafamilia wote kushikamana kwa
pamoja wakiwa na moyo na roho moja, kwani Kristo ndiye anayewategemeza.
Uwanja
wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ulikuwa umesheheni umati wa watoto,
vijana na wazee walioungana na Baba Mtakatifu katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani,
tukio ambalo limeongozwa na kauli mbiu "Familia inaishi furaha ya imani". Baba Mtakatifu
anasema, amepata bahati ya kusikiliza kwa makini uzoefu, historia na mang'amuzi ambayo
wameyasimulia wakati wa mkesha huo.
Ameguswa na magumu, umaskini, magonjwa
na changamoto mbali mbali katika maisha ya kifamilia, lakini pamoja na mambo yote
haya, bado waamini wanaalikwa kumwilisha furaha ya imani kwa Kristo anayewaalika kumwendea,
ili aweze kuwapumzisha.
Hizi ni familia zinazoelemewa na mzigo wa ukosefu wa
fursa za ajira, ukosefu wa upendo wa dhati, tabasamu la kukata na shoka pamoja na
kushindwa kupokelewa. Hii ni mizigo ya ukimya unaozua wasi wasi na hofu ndani ya familia,
kwani bila upendo wa dhati wanandoa watashindwa kuvumilia magumu yanayojitokeza katika
sehemu za kazi. Baba Mtakatifu anawakumbuka wazee wanaoishi bila msaada; familia zinazoshindwa
kuhimili kishindo cha makali ya maisha kutokana na sera tenge za uchumi; familia zinazokabiliana
na magonjwa yanayohitaji huduma makini. Familia zote hizi anasema Baba Mtakatifu
zinakaribishwa na Yesu, ili zipate kupumzika kwani Yesu anazifahamu fika na kwamba,
anataka kuzikirimia furaha ya kweli inayobubujika kutoka kwake. Huu ndio ujumbe ambao
Baba Mtakatifu anawaalika Wanafamilia kuukumbatia na kuusambaza kwa jirani zao. Wanandoa
wanapaswa kuwa waaminifu katika taabu na raha, katika magonjwa na afya; wakipendana
na kuheshimiana siku zote za maisha yao.
Hii ni hija ya matumaini kwa wanandoa,
kwani hawatambui yale ambayo wanaweza kukumbana nayo katika safari ya maisha yao ya
ndoa, lakini kama ilivyokuwa kwa Abraham wanamtumainia Mwenyezi Mungu bila woga huku
wakiendelea kuwajibika mbele ya Mungu na Jamii inayowazunguka. Wanandoa wanapaswa
kutekeleza utume wao wa kuunda familia na kwamba, neema inayotolewa na Sakramenti
za Kanisa si kwa ajili ya kupamba ndoa, bali ni kwa ajili ya kuwaimarisha na kuwajalia
ushujaa ili kusonga mbele na kusali kwa pamoja kama Jumuiya katika safari inayodumu
maisha yao yote hadi pale kifo kitakapowatenganisha.
Baba Mtakatifu anabainisha
kwamba, wanandoa wanahitaji uwepo wa Yesu katika hija ya maisha yao, ili waweze kuwa
na imani, wapokeane, wathaminiane na kuheshimiana kwa kutambua kwamba, wao si wakamilifu.
Samahani, Naomba radhi na Asante ni maneno msingi katika kudumisha umoja, upendo na
mshikamano wa dhati ndani ya familia. Wanandoa wajifunze kusamehana kila siku ya maisha
yao.
Wajifunze kusali, kula na kupumzika kwa pamoja. Watekeleze matendo ya
huruma kwa kuwatembelea wagonjwa na wazee. Pale ambapo hakuna upendo, furaha na sherehe
vinatoweka kama ndoto ya mchana. Yesu ni Sakramenti ya furaha kwa njia ya Neno na
Mkate wa uzima anaowakarimia wafuasi wake, ili waweze kuwa na furaha timilifu.
Baba
Mtakatifu Francisko anawaalika wanafamilia kuiga mfano wa Familia Takatifu ya Yesu,
Maria na Yosefu iliyoonesha utii kwa sheria, wakaenda Hekaluni na kupokelewa na Mzee
Simeoni na Anna, waliobahatika kumwona Masiha aliyekuwa anasubiriwa na watu wengi.
Wazee hawa wawili ni kielelezo cha imani kama kumbu kumbu, mwaliko kwa vijana wa kizazi
kipya kuwasilikiza na kuwaheshimu wazee kwani wote wanategemeana.
Baba Mtakatifu
anasema, Familia takatifu ilitakatifuzwa kwa uwepo wa Yesu, hivyo wanafamilia hawana
budi kushikamana na kutembea pamoja na Yesu, huku wakitolea ushuhuda wa imani yao
na kwamba, Yesu anayo maneno ya uzima. Baba Mtakatifu amewashukuru na kuwatakia wanafamilia
wote jioni njema.