Baada ya Miaka 10 ya maombi, Maaskofu Katoliki Zambia wapata kibali cha kuanzisha
Kituo cha Televisheni! Si haba!
Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia limeipongeza na kuishukuru Serikali ya Zambia kwa
kutoa kibali kwa Baraza la Maaskofu katoliki Zambia kufungua na kuendesha kituo cha
Televisheni kama sehemu ya mchakato wa utangazaji wa Injili kwa njia ya za mawasiliano
ya kijamii.
Tangu mwaka 2002, Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia kwa mara
ya kwanza liliomba kibali cha kuanzisha kituo cha Televisheni Kitaifa, lakini Serikali
ikawa kimya kwa miaka yote hii, lakini Maaskofu waliendelea kuvuta subira hadi pale
Serikali iliporidhia ombi lao hapo tarehe 18 Oktoba 2013.
Akizungumzia kuhusu
tukio hili Paadre Paul Samasumo, Msemaji mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia
anafafanua kwamba, wazo la kuanzisha Kituo cha Televisheni cha Kanisa ni changamoto
iliyotolewa na Mababa wa awamu ya kwanza ya Sinodi ya Afrika iliyofanyika kunako mwaka
1995 kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika njia za mawasiliano ya jamii kama vyombo
muhimu vya Uinjilishaji Barani Afrika. Mkazo ukawekwa kwenye vituo vya radio na televisheni
nchini Zambia.
Lengo lilikuwa ni kuhakikisha kwamba, Kanisa linashiriki kwa
hali na mali katika kurithisha tunu msingi za maisha ya Kiinjili, Kiutu na Kitamaduni
kwa watu wa nyakati hizi bila upendeleo kwa kuzingatia sheria, kanuni na maadili.
Wazo hili ni changamoto iliyotolewa pia na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, aliyelichangamotisha
Kanisa kuhakikisha kwamba, linasoma alama za nyakati kwa kujikita katika Uinjilishaji
wa vyombo vya mawasiliano ya jamii hata katika jukwaa hili jipya, linalohitaji pia
kuonja "cheche za Injili".
Kituo hiki cha Televisheni cha Baraza la Maaskofu
Katoliki Zambia, kinalenga kuwahudumia wananchi wote wa Zambia bila ubaguzi, kwa kuzingatia:
Maadili, Kanuni na Mafundisho Jamii ya Kanisa. Maaskofu wanatambua changamoto kubwa
zilizoko mbele yao katika kukiendesha, lakini ni muhimu kwa ajili ya ustawi na maendeleo
ya wananchi wa Zambia: kiroho na kimwili. Ni kituo ambacho kinalenga Familia nzima.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Zambia anasema Padre Paul Samasumo, litaendelea kugharimia vituo
vya Radio vilivyoanzishwa na Majimbo kama vile Kituo cha radio Lutanda kilichoko
Jimbo Katoliki la Chipata. Kituo cha Radio Sesheke kinatarajiwa kufunguliwa eneo la
Sesheke na kwamba, Radio Maria Zambia sasa inaweza kusikika nchi nzima.
Hiki
ni kituo ambacho kimeendelea kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha maisha ya sala,
tafakari ya Neno la Mungu na maisha ya kiroho. Kwa hakika anasema Padre Paul Samasumo
hii ni sauti ya Kikristo katika nyumba za wananchi wa Zambia, inayoleta mvuto na mguso
wa kusikiliza!