2013-10-25 09:51:30

Siku ya Mapadre nchini Marekani


Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, Jumapili tarehe 27 Oktoba 2013 linaadhimisha Siku ya Mapadre Marekani. Hii ni fursa maalum kwa waamini wa Parokia mbali mbali nchini Marekani kuweza kuunganika pamoja na Mapadre wao kwa: Ibada, Sala, tafakari na Majadiliano ya kina kuhusu maisha na utume wa Mapadre ndani ya Kanisa.

Miaka 10 iliyopita, Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani lilianzisha Siku ya Mapadre Kitaifa, kama njia ya waamini kuonesha moyo wa shukrani kwa huduma za maisha ya kiroho na kijamii inayotolewa na Mapadre katika maisha na utume wao nchini Marekani. Hii inatokana na ukweli kwamba, maisha na utume wa Mapadre unaangaliwa na vyombo vingi vya upashanaji habari "kwa jicho la makengeza".

Tukio hili ni muhimu sana hasa kwa wakati huu idadi ya miito ya Kipadre inapoendelea kupungua siku hadi siku. Nchini Marekani kuna Parokia 19,000 na kati ya hizi ni Parokia 4,000 tu ndizo ambazo zimebahatika kuwa na Padri. Kumbe, kuna baadhi ya Mapadre wanalazimika kuhudumia zaidi ya Parokia moja kutokana na uhaba wa Mapadre.







All the contents on this site are copyrighted ©.