Askofu asiyesali na kulitafakari kwa kina Neno la Mungu, atamezwa na malimwengu!
Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 24 Oktoba 2013 majira ya jioni amewaweka
wakfu Maaskofu wakuu wawili watakaoshiriki katika utume wa: kufundisha, kuongoza na
kuwatakatifuza watu wa Mungu katika hija ya maisha yao hapa duniani. Hawa ni Askofu
mkuu Jean Marie Speich, Balozi wa Vatican nchini Ghana na Askofu mkuu Giampiero Gloder,
Rais wa taasisi ya elimu ya Kanisa.
Yesu Kristo mwanzoni mwa utume wake, aliwachagua
mitume kumi na wawili waliokuwa wamejazwa nguvu ya Roho Mtakatifu kwenda kutangaza
Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Mwishoni, hata mitume waliwaweka wakfu
wasaidizi wao ili kushiriki katika utume wa kutangaza Injili ya Kristo, Mapokeo ambayo
bado yanaendelea hadi leo hii.
Askofu anapozungukwa na Makleri wake, Yesu
Kristo, Kuhani mkuu yuko pamoja nao! Kristo kwa njia ya maisha na utume wa Askofu
anaendelea kutangaza Injili ya Wokovu; anaendelea kuwatakatifuza waamini kwa njia
ya Sakramenti za Kanisa. Kristo analijalia Kanisa lake waamini wapya wanaojenga na
kuimarisha Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Ni Kristo kwa njia ya unyenyekevu
na hekima ya Askofu anawaongoza watu wa Mungu katika hija ya maisha yao hapa duniani,
ili waweze kufikia furaha ya uzima wa milele!
Baba Mtakatifu anasema, Maaskofu
wapya waliowekwa wakfu wanaingizwa katika hurika wa Kiaskofu; wanapaswa kuheshimiwa
kama wahudumu wa Kanisa na wagawaji wa mafumbo matakatifu na kwamba, wanatakiwa kutolea
ushuhuda wa Injili na utume wa Roho Mtakatifu katika azma ya kutakatifuza. Ni viongozi
wanaopaswa kusikilizwa na kuheshimiwa kwa ajili ya Kristo.
Baba Mtakatifu amewaambia
Maaskofu wakuu Jean Marie e Giampiero kwamba, watafakari kwa kina kwamba, wamechaguliwa
kutoka kati ya watu kwa ajili ya mambo yanayomhusu Mungu. Uamskofu ni kielelezo cha
huduma na wala si heshima. Askofu anapaswa kuhudumia na wala si kutawala. Huduma kwa
familia ya Mungu ipewe kipaumbele cha kwanza.
Maaskofu wanatumwa kutangaza
Injili kwa wakati unaofaa na ule usiofaa! Wanapaswa kukemea na kuonya, kufundisha
na kutia moyo, daima wakijitahidi kuadhimisha Mafumbo matakatifu kama njia ya kupata
utimilifu wa utakatifu wa maisha. Askofu ajibidishe kulitafakari Neno la Mungu na
kusali, vinginevyo anaweza kumezwa na malimwengu! Kama walinzi na wagawaji wa Mafumbo
matakatifu na viongozi wa Familia ya Mungu, wanapaswa kuiga mfano wa Kristo mchungaji
mwema, anayewafahamu Kondoo wake, kiasi hata cha kuyamimina maisha yake, huu ndio
upendo unaobubujika kutoka kwa Askofu.
Baba Mtakatifu anawaalika Maaskofu wakuu
wapya kuwapenda wale wote ambao Mwenyezi Mungu amewakabidhi katika utume wao. Kwanza
kabisa Makleri kwani wao ndio wasaidizi na jirani zao wakuu. Maaskofu wajenge utamaduni
wa kuwasikiliza Makleri na kuwasaidia. Waoneshe upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii pamoja na kuwashirikisha waamini walei katika maisha na utume
wa Kanisa na kwamba, hawana budi kuwa karibu na waamini wao!
Baba Mtakatifu
anawaalika Maaskofu wakuu wapya kujenga na kuimarisha moyo wa majadiliano ya kidini
na kiekumene; kwa kushikamana na Maaskofu wengine wote, tayari kuyasaidia Makanisa
yanayohitaji. Maaskofu wachunge Kondoo wa Kristo mintarafu maongozi ya Roho Mtakatifu
kwa ajili ya Kanisa la Mungu. Wakeshe katika Fumbo la Utatu Mtakatifu; kwa kutambua
kwamba, wao ni: Waalimu, Makuhani na Wachungaji. wakumbuke kwamba, Roho Mtakatifu
anawainua katika unyonge wao kama binadamu.