Miaka 25 ya Utawa na Upadre si haba kwa Waklaresiani nchini Tanzania
Hivi karibuni Padre George Nedumattan, Padre Bernard John pamoja na Padre Baskar Alamal
Raj kutoka Shirika la Waklaresiani wanaofanya utume wao Afrika Mashariki, hususan
nchini Tanzania na Uganda, wameadhimisha Jubilee ya Miaka 25 ya Upadre na Miaka 25
ya Maisha ya Kitawa kwa Padre Baskar Raj.
Hawa ni mapadre
ambao wamejitosa kutangaza Habari Njema ya Wokovu bila ya kujibakiza; wakawa tayari
kusimamia mafao ya wengi, wema, ukweli, utu na heshima ya binadamu. Kwa maneno na
maisha yao, wameendelea kutangaza Injili nchini India, Tanzania na Uganda.
Akitoa
neno la shukrani kabla ya Ibada ya Misa Takatifu iliyoadhimishwa kwenye Ukumbi wa
Kituo cha Familia Makoko, Jimbo Katoliki la Musoma, Padre Francis John, Mratibu mkuu
wa Shirika la Waklaresiani, Afrika Mashariki amesema kwamba, mapadre hao wametumia
muda wao mwingi kwa ajili ya kulea miito ya kipadre pamoja na shughuli za kichungaji
kwa Majimbo ya Musoma, Tanzania na Jinja, Uganda.
Familia ya Mungu, Jimbo
Katoliki Musoma, iliungana na Mapadre hawa kwa ajili ya kumwimbia Mungu utenzi wa
sifa na shukrani, wakiendelea kuwaombea mapadre hao neema, baraka na afya njema, ili
waweze kujitosa kimasomaso kwa ajili ya Mungu na jirani zao katika maisha ya kipadre
na kitawa.
Katika mahubiri yake, Padre Bernard John aliyewahi kuwa mkurugenzi
wa kituo cha familia cha Makoko, Jimbo Katoliki Musoma aliwataka waamini kujibidisha
kutenda mema kwa kuchuchumilia utakatifu wa maisha unaojionesha kwa namna ya pekee
kwa kuwahudumia wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kama Mapadre na watawa wa
Shirika la Waklaresiani, wanatumwa kuwahudumia ndugu zake Kristo, sehemu mbali mbali
za dunia.
Upadre na utawa ni wito wenye misalaba, neema na baraka. Katika maisha
na utume wao kama Wamissionari, wamewahi kuvamiwa na majambazi huko Morogoro; waliwahi
kutekwa nyara na kuibiwa wakiwa mpakani kati ya Tanzania na Kenya eneo la Namanga.
Baadhi yao wamewahi kupinduka na gari, lakini wakanusurika. Katika majanga yote haya
ya maisha, wameonja pia huruma, upendo na ulinzi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Leo
hii wanathubutu kusimama Altareni ili kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa shukrani
kwa Mungu, kwa viongozi wa Kanisa Afrika Mashariki na kwa Familia ya Mungu, mahali
pale ambapo wamehudumia kwa moyo wao wote! Wameonja na kushiriki “majanga” ya maisha
ya waamini katika Parokia mbali mbali wanazoendelea kuhudumia nchini Tanzania na Uganda.
Mapadre
hawa wanawaalika waamini kwa namna ya pekee, kuhakikisha kwamba, wanakuwa ni mwanga
unaobubujika kutoka kwa Kristo mwenyewe. Kila Mkristo anapaswa kukiri, kuadhimisha,
kuishi na kusali imani yake kwa njia ya matendo, ili wengi waweze kuguswa na kuvutwa
kumfahamu, kumpenda na kumtumikia Kristo, ili hatimaye, waweze kupata uzima wa milele.
Wamissionari
hawa wanaowamba waamini kuendelea kusali kwa ajili yao, ili waweze kutekeleza dhamana
na wajibu wa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Wanasema, wao
wataendelea kuwa ni wahudumu wa Neno la Mungu, waadhimishaji wa Mafumbo ya Kanisa
na matendo ya huruma, ili Injili ya Kristo iweze kuenea na kujikita katika mioyo ya
Familia ya Mungu Barani Afrika.
Jubilee ni kipindi cha shukrani na moyo wa
toba, hasa kwa yale ambayo wameshindwa kufanya kwa kuelemewa na mapungufu yao ya kibinadamu.
Wanawaalika waamini kuendelea kuwa na moyo mkuu na wenye fadhila, ukarimu, ili kuonesha
utukufu wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.
Wamissionari hao wanasema kwamba,
ushirikiano kati yao na waamini umewezesha kuleta mabadiliko makubwa katika sekta
ya elimu, afya na shughuli za kichungaji Jimboni Musoma na Jinja, kama sehemu ya mchakato
wa Uinjilishaji wa kina. Kama Shirika limeendelea kuona changamoto ya elimu na afya
kwa wananchi wa Jimbo la Musoma na Tanzania katika ujumla wake.
Wataaendelea
kuifanyia kazi changamoto hii kwa kujenga na kuboresha shule wanazomiliki na kuziendesha,
ili kuweza kukidhi matarajio ya Kanisa katika sekta ya elimu na afya. Jubilee hii
ilihudhuriwa na Mapadre wa CMF kutoka Jumuiya zake zilizoko Tanzania na Uganda.
Kutoka
Jimbo Katoliki la Musoma ni Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.