2013-10-24 10:20:55

Jumuiya ya Kimataifa haina budi kusimama kidete katika utekelezaji wa rufuku ya silaha za mahangamizi!


Askofu mkuu Francis Chullikatt, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa, hivi karibuni wakati alipokuwa anachangia hoja kuhusu upigaji rufuku wa silaha za kinyuklia duniani, kwenye Mkutano wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa anasema, umefika wakati kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, silaha za maangamizi zinapigwa rufuku.

Anasema, hivi karibuni, Jumuiya ya Kimataifa imeonesha ujasiri wa pekee na wa kihistoria kwa kupitisha azimio kuhusu uteketezaji wa silaha za kemikali nchini Syria. Lakini jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, kuna baadhi ya mataifa makubwa duniani yanakwamisha jitihada hizi za Umoja wa Mataifa katika kudhibiti na kufutilia mbali utengenezaji, usambazaji na matumizi ya silaha za Kinyuklia. Ni jambo la aibu kwa baadhi ya nchi kushutumu matumizi ya silaha za maangamizi, lakini kwa Jumuiya ya Kimataifa inapojadili kuhusu silaha za Kinyuklia, wanafunga kauli!

Umefika wakati kwa Jumuiya ya Kimataifa kuzungumza na kutenda kwa mshikamano ili kukomesha utengenezaji, usambazaji na matumizi ya silaha za maangamizi duniani. Katika ulimwengu huu ambao umegeuka kuwa kama kijiji, Jumuiya ya Kimataifa haiwezi kuendelea kuenzi utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya mamillioni ya watu duniani kutokana na vita.

Kuna haja ya kufutilia mbali falsafa ya vita vinavyosababisha majanga na badala yake kuanza mchakato wa kupembua mahitaji msingi ya binadamu, ili yaweze kushughulikiwa ipasavyo!







All the contents on this site are copyrighted ©.