2013-10-24 14:51:03

Familia inapaswa kuwa ni sehemu ya sera na mikakati ya kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiroho ili iweze kutekeleza dhamana yake!


Kardinali George Pell, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Sydney, Australia, hapo tarehe 23 Oktoba 2013 amefungua rasmi mkutano wa Baraza la Kipapa la Familia kwa Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican. Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia alizungumzia kuhusu mwono, changamoto, matarajio na mikakati ya Baraza lake kwa siku za usoni.

Anasema, Familia ina hazina kubwa katika maendeleo na mwanadamu: kiroho na kimwili, lakini pia familia zinakabiliwa na changamoto mbali mbali katika maisha na utume wake. Kuna mmong'onyoko mkubwa wa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, hali ambayo inachangia kusambaratisha familia nyingi duniani. Ubinafsi na kilio cha haki msingi za binadamu zinazosigana na utu wema ni kati ya changamoto kubwa kwa familia katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na tekenolojia.

Ni matumaini ya Baraza la Kipapa kwamba, familia itaendelea kuwa ni kiini cha mikakati na sera makini za kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiroho. Kanisa kwa upande wake, litaendelea kutangaza Injili ya familia, kwani ni sehemu ya vinasaba vya maisha ya mwanadamu. Wazazi walioachana na kuoa au kuoana ni changamoto katika malezi na makuzi ya watoto.

Wajumbe pamoja na mambo mengine wamekazia umuhimu wa familia za Kikristo kutoa ushuhuda makini katika maisha na vipaumbele vyao, kwa kuungana na Kristo kwa njia ya tafakari ya Neno la Mungu, maisha ya Kisakramenti, Sala na Matendo ya huruma. Baraza la Kipapa la Familia litaendelea kuhimiza utekelezaji wa katiba ya Familia Kimataifa sanjari na kuangalia haki zake za kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.