2013-10-24 10:47:27

Amani ya kudumu ni jambo muhimu sana huko Mashariki ya Kati!


Ujumbe wa Vatican unauangalia kwa matumaini makubwa mchakato wa kuanza tena kwa mazungumzo kati ya Israeli na Palestina kama njia ya kudumisha amani na usalama huko Mashariki ya Kati. NI matumaini ya ujumbe huu kwamba, mkutano wa pili wa Jumuiya ya Kimataifa kuhusu Syria, utasaidia upatikanaji wa amani ya kudumu nchini humo.

Hii inatokana na ukweli kwamba, mtutu wa bunduki unaporindima, wanaoathirika na kulipa kwa gharama ya maisha yao ni wananchi wa kawaida! Kumbe, kuna haja ya kuwa na suluhu la kisiasa itakayorudisha amani, usalama na utulivu huko Mashariki ya Kati sanjari na kuwasaidia wahamiaji na wakimbizi kwa hali na mali, kama sehemu ya mchakato unaopania kuwapatia wananchi wa eneo hili maendeleo endelevu.

Ni maoni ya Askofu mkuu Francis Chullikatt, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa alipokuwa anachangia mada hivi karibuni mada kuhusu hali ya usalama huko Mashariki ya Kati. Baba Mtakatifu Francisko ameendelea kukazia umuhimu wa usalama, amani na utulivu huko Mashariki ya Kati. Viongozi wa pande zinazohusika na mgogoro wa kivita nchini Syria hawana budi kuacha mapigano kama hatua muhimu itakayosaidia mchakato wa majadiliano yanayolenga upatikanaji wa suluhu ya kudumu nchini humo, katika mkutano wa Jumuiya ya Kimataifa unaotarajiwa kufanyika mjini Geneva, mwezi Novemba, 2013.

Askofu mkuu Chullikatt anasema kwamba, hadi sasa takwimu zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni nne ambao hawana makazi na wengine millioni mbili wameyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa mali na maisha yao. Hali hii tete inaweza kuhatarisha usalama na amani huko Mashariki ya Kati. Kanisa Katoliki kwa upande wake, litaendelea kutoa msaada wa hali na mali kwa waathirika wa mgogoro wa kivita nchini Syria bila ubaguzi wa kikabila wala kidini.

Anasema, inasikitisha kuona kwamba, kuna idadi kubwa ya Wakristo wanaolazimika kuyakimbia makazi na nchi zao kutokana na madhulumu ya kidini, hali ambayo inawalazimisha kuikimbia historia ya maisha yao kwa takribani miaka elfu mbili iliyopita, historia ambayo imejikita katika maisha na tamaduni za watu huko Mashariki ya Kati. Ni jambo lisilokubalika kuona kwamba, madhulumu ya kidini yanaendelea huko Mashariki kiasi cha kutishia amani na usalama wa Wakristo, kama ilivyotokea nchini Iraq.







All the contents on this site are copyrighted ©.