2013-10-23 14:42:41

Haki msingi za familia kimataifa!


Baraza la Kipapa la Familia kuanzia Alhamisi tarehe 24 Oktoba hadi tarehe 25 Oktoba 2013 linaendesha Kongamano la Kimataifa kuhusu haki ya familia, hasa wakati huu ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia unaposhuhudia athari za myumbo wa uchumi kimataifa pamoja na kumong'onyoka wa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Baraza la Kipapa la Familia wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, linapenda kuchukua nafasi hii kuwashirikisha wadau mbali mbali katika kongamano linalopania kuchambua kwa kina na mapana haki msingi za familia. Kongamano hili linakwenda sanjari na mkutano mkuu wa Baraza la Kipapa la Familia, utakaohitimishwa kwa kesha la Mwaka wa Imani kwa ajili ya familia; tukio ambalo litazishirikisha familia kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Muda huu ni kipindi cha sala na tafakari ya kina kuhusu haki msingi za familia katika ulimwengu mamboleo.

Licha ya viongozi wakuu kutoka Baraza la Kipapa la familia kushiriki katika kongamano hili, kutoka Barani Afrika ni Kardinali John Onaiyekani, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria. Kati ya mambo yatakayojadiliwa ni Katiba ya Familia Kimataifa na mielekeo mipya ya haki msingi za kifamilia.







All the contents on this site are copyrighted ©.