2013-10-23 08:55:03

Familia imara ni nguzo msingi za Kanisa


Padre Raymond Saba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano na Radio Vatican anabainisha kwamba, Kanisa limeendelea kuwekeza katika taasisi ya Familia kwa kutambua kwamba: Familia ni Kanisa dogo la nyumbani, chemchemi ya imani, matumaini na mapendo, changamoto endelevu ya kujenga na kuimarisha familia ili ziweze kutekeleza wajibu wake barabara ndani ya Jamii na Kanisa. RealAudioMP3

Anasema, Kanisa imara na thabiti linajengeka katika msingi wa familia bora inayoonesha upendo kati ya Baba, Mama na Watoto ambao kimsingi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Familia ni chemchemi ya miito mbali mbali ndani ya Kanisa kiasi kwamba, hata wito wa familia yenyewe unapata chimbuko lake ndani ya familia. Familia zinapaswa kuimarishwa ili kulifahamu Fumbo la Utatu Mtakatifu; kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa, Kusali na kuwa kweli ni kielelezo cha maadili na utu wema katika Jamii inayowazunguka.

Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Familia zinachangamotishwa kuwashirikisha majirani zao imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, kama njia ya ushuhuda wa imani tendaji. Familia itambue kwamba, ni Kanisa dogo la nyumbani, nguzo thabiti ya malezi na makuzi ya: imani, maadili na utu wema.

Padre Raymond Saba ambaye ameteuliwa hivi karibuni na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kuwa Katibu mkuu mpya, kuchukua nafasi ya Padre Anthony Makunde aliyemaliza muda wake wa uongozi, anawaalika wanafamilia kuhakikisha kwamba, wanashirikishana imani yao kuanzia katika familia. Baba, Mama na Watoto wasaidiane kusoma na kulitafakari Neno la Mungu kwa pamoja; wasali na kuonjeshana tone la upendo, huruma na msamaha; familia kwa pamoja ijitahidi kushiriki katika maadhimisho mbali mbali ya Sakramenti za Kanisa kwa njia ya ushiriki mkamilifu.

Padre Saba anasema, ikiwa kama familia zitatekeleza wajibu huu msingi kwa hakika familia za Kikristo zitakuwa ni shule ya sala, amani, upendo, mshikamano na uaminifu kama alivyokumbusha Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alipotembelea nchini Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.