2013-10-23 14:28:58

Bikira Maria ni mfano na kielelezo cha imani, upendo na mshimamano wa dhati na Kristo Yesu!


Bikira Maria mwenyeheri, kwa kipaji cha dhima na umama wa kimungu unaomwunganisha na Mwanae Mkombozi, na kwa neema zake za huduma zake za pekee ameunganika kwa undani na Kanisa. Mama wa Mungu ni kielelezo cha Kanisa, kwa habari ya imani, mapendo na umoja kamili na Kristo, kama alivyowahi kufundisha Mtakatifu Ambrosi.

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa katekesi yake, Jumatano, tarehe 23 Oktoba kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, kuhusu dhamana na nafasi ya Bikira Maria kama kielelezo na mfano wa Kanisa. Bikira Maria ni mfano na kielelezo cha imani inayoonesha mpango wa Mungu katika maisha yake, kiasi cha kumchagua kati ya wanawake wote kuwa ni Mama wa Mkombozi.

Ni mwanamke aliyejaa neema na ambaye alikubali mpango wa ukombozi uliotekelezwa na Mwenyezi Mungu katika maisha yake. Ukubali wa Maria ukamwezesha kuwa ni Mama wa Kristo, kielelezo cha hija ya imani iliyofanywa na waamini mbali mbali waliokuwa wanasubiri wokovu katika maisha yao. Bikira Maria ni kielelezo cha imani ya Kanisa katika Fumbo la Umwilisho, linaloonesha upendo wa Mungu usiokuwa na kifani kwa binadamu.

Bikira Maria aliweza kumwilisha imani yake katika uhalisia wa maisha ya kila siku, akajenga majadiliano ya kina kati yake na Mwenyezi Mungu kwa njia ya sala iliyomwezesha kudiriki kusimama chini ya Msalaba. Umama wake anasema Baba Mtakatifu unawakumbatia wanadamu wote katika Fumbo la Umwilisho. Ni mwanamke aliyejikita katika tafakari ya kina, mwanafunzi amini wa Kristo, changamoto kwa waamini kumwachia nafasi Bikira Maria ili aweze kuwaongoza katika imani kwa Kristo.

Bikira Maria alikuwa ni mfano wa huduma ya upendo unaojionesha kwa kumtembelea na kumhudumia binadamu yake Elizabeth aliyekuwa mjamzito. Ni Mama aliyeonesha ukarimu wa pekee kwa kumbeba tumboni mwake Neno wa Mungu aliyefanyika mwili kwa njia ya Roho Mtakatifu, aliyewakirimia watu furaha ya kweli. Bikira Maria anataka kuwapatia watu wote zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu ambayo ni Yesu Kristo.

Baba Mtakatifu anasema, Yesu anawakirimia waja wake: furaha, amani na upendo. Kanisa linatumwa na Kristo kwenda ulimwenguni kote ili kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Kila mwamini ni sehemu ya Kanisa, kumbe anao wajibu wa kuhakikisha kwamba, anampeka Yesu kwa watu wa mataifa, kwa kuwashirikisha na kuwaonjesha wengine tone la upendo unaoponya na kusamehe; upendo unaojitosa kimasomaso kwa ajili ya mafao ya wengi; upendo unaowaunganisha watu chini ya mchungaji mmoja ambaye ni Kristo mwenyewe, kwa kusaidiana na kutaabikiana.

Baba Mtakatifu anasema, Bikira Maria ni kielelezo cha umoja mkamilifu na Yesu Kristo kwa njia ya maisha na matendo yake. Bikira Maria alikuwa ni mwanamke wa sala na kazi, kiasi hata cha kudiriki kusimama chini ya Msalaba, hapo akajiunga na Mwanaye mpendwa Yesu Kristo, katika sadaka safi, isiyo na waa wala makunyanzi kwa ajili ya ukombozi wa binadamu. Akashiriki mateso ya Mwanaye kama njia ya kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yake; utii unaoshinda dhambi na mauti. Huu ni mwaliko kwa waamini kuungana na Yesu katika maisha yao, kwa kudumisha urafiki wa dhati hata katika ile Njia ya Msalaba.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuendelea kusali Rozari Takatifu kwa ajili ya kuombea amani duniani pamoja na tunu msingi za maisha ya Kiinjili kuweza tena kumwilisha katika uhalisia wa maisha ya waamini na watu wote wenye mapenzi mema. Amewapongeza waamini wote wanaoendelea kuadhimisha kwa ari na moyo mkuu Mwaka wa Imani sehemu mbali mbali za dunia.

Mwishoni anasema, kila mwamini anachangamotishwa na Mama Kanisa katika mwezi Oktoba kuwa ni mmissionari anayetumwa kutangaza Injili hadi miisho ya dunia, kwa kuwashirikisha jirani zake, upendo wa Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.