2013-10-22 12:39:49

Mwenyezi Mungu anapenda kuponya madonda ya dhambi na mauti!


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, siku ya jumanne, tarehe 22 Oktoba 2013 amekazia mambo makuu matatu: tafakari ya kina, ukaribu kwa Mwenyezi Mungu na utashi wa kutaka kutekeleza mapenzi ya Mungu. Haya ni mambo muhimu sana yanayoweza kumsaidia mwamini kulifahamu Fumbo la Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, haiwezekani kwa mwamini kulifahamu Fumbo la Mungu kwa kutumia juhudi za akili yake kwani Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo amejichanganya katika maisha ya mwanadamu, ili aweze kuwaponya madonda yao ya ndani, kama alivyofanya Yesu mwenyewe.

Fumbo la Mungu ni jambo linaloendelea kumshangaza mwanadamu katika hija ya maisha yake ya imani ndiyo maana Mtakatifu Paulo anajitaabisha kuwafafanulia waamini kuhusu Fumbo la Ukombozi lililotekelezwa na Mungu, linaloweza kufahamika kwa njia ya tafakari ya kina. Haya ndiyo yaliyojionesha hata katika historia ya Kanisa. Waamini wanapaswa kulitafakari, kulisali na kulimwilisha katika uhalisia wa maisha yao.

Kwa vile mwanadamu anaendelea kutopea katika dimbwi la dhambi, Mwenyezi Mungu kwa huruma na upendo wake, ameamua kujinyenyekesha na kujishusha ili aweze kuwa karibu kabisa na binadamu na hatimaye kumkomboa kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Huyu ndiye Mungu ambaye yuko karibu katika historia na hija ya maisha ya mwanadamu, kama inavyojionesha katika historia ya ukombozi. Amekuwa ni jirani yake ili aweze kumkomboa na wala si kwa shuruti wala mikwara!

Baba Mtakatifu anasema, pale dhambi ilipoongezeka maradufu, hapo pia neema na baraka za Mungu zimejionesha kwa kiasi kikubwa, ili kuweza kuponya madonda ya dhambi kwa njia ya upendo na neema zake. Ndiyo maana Yesu alionesha upendeleo wa pekee kwa wadhambi ili kuwaonjesha huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka, akitambua kwamba, wao kama wagonjwa walikuwa na uhitaji mkubwa wa tabibu ambaye ndiye Yesu Kristo.

Hii ni changamoto kwa waamini kuendelea kumtegemea Mwenyezi Mungu katika maisha na vipaumbele vyao, kwani Yeye ni mwingi wa huruma na upendo.







All the contents on this site are copyrighted ©.