2013-10-22 10:05:59

Baraza la Maaskofu Katoliki Togo na changamoto zake!


Utume wa Mama Kanisa, ushuhuda amini wa imani na changamoto zinazolikabili Kanisa ni kati ya mada zilizochambuliwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Togo katika mkutano wake wa kawaida uliohitimishwa hivi katibuni huko Dapaong nchini Togo. Maaskofu wameangalia kwa ukaribu zaidi maisha ya waamini wa Kanisa Katoliki wanaounda walau asilimia ishirini ya idadi ya wananchi wote wa Togo na mchango wao katika ustawi na maendeleo endelevu nchini humo.

Maaskofu kwa pamoja wamekubaliana kufanya mabadiliko makubwa katika maisha ya Seminari, mahakama za Kanisa na Mafundisho ya Kanisa ili kuendana na hali halisi pamoja na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Maaskofu wamechambua kwa kina na mapana hali ya seminari kuu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Togo na umuhimu wake kama kisima cha majiundo makini ya maisha ya kipadre na kitawa nchini humo.

Maaskofu wameamua kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na Serikali, Wazazi na Walimu ili kuhakikisha kwamba, wanafunzi nchini Togo wanapata elimu bora wanapokua shuleni na kwamba, kuna haja kwa Kanisa kuchangia zaidi katika lengo hili. Maaskofu wanayashukuru kwa namna ya pekee, Mashirika ya kitawa yanayoendelea kutoa huduma makini katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu kwa wananchi wote wa Togo bila ubaguzi na kwamba, mikakati ya majiundo makini kwa vijana nchini humo ni jambo linalowagusa sana.

Askofu mkuu Brian Udaigwe, Balozi wa Vatican nchini Togo, alipata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Maaskofu Katoliki Togo. Katika mkutano huu, aliwasilisha pia hati zake za utambulisho kutoka Vatican kwa Rais Faure Gnassinbe wa Togo. kwa mara ya kwanza Askofu mkuu Brian aliweza kushiriki katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu na waamini wa Kanisa Katoliki nchini Togo. Amewapongeza kwa mwamko na ari kubwa katika maisha yao ya Kikristo.

Askofu mkuu Brain amekazia umuhimu kwa wananchi wa Togo kujikita tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili katika mchakato unaopania ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. Ni wajibu wa kila mdau kuhakikisha kwamba, anajenga na kuimarisha utawala wa sheria, umoja wa kitaifa; msamaha na upatanisho; mambo msingi katika ujenzi wa maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Baraza la Maaskofu Katoliki Togo linamshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwapatia mwakilishi atakayewaonjesha upendo na mshikamano wa Baba Mtakatifu kwa wananchi wa Togo, hasa wakati atakapokuwa anafanya hija za kichungaji kwenye Majimbo Katoliki nchini Togo.







All the contents on this site are copyrighted ©.