2013-10-21 09:31:52

Miaka 30 ya Kituo cha Televisheni cha Vatican si haba!


Kituo cha Televisheni cha Vatican, kinaadhimisha Miaka 30 tangu kilipozinduliwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, kama sehemu ya mchakato wa Mama Kanisa katika kutoa kipaumbele kwa mwanadamu aliyeumba kwa sura na mfano wa Mungu; umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea haki na amani, pamoja na kuwajengea watu matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi.

Kituo hiki kimeendelea kusoma alama za nyakati katika mabadiliko yanayojitokeza katika medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu; daima kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika uwajibikaji. Haya ni kati ya mambo ambayo yameendelea kufanyiwa kazi na Kituo cha Televisheni cha Vatican katika utekelezaji wa majukumu yake ya kutoa picha za televisheni kwa vituo mbali mbali vya televisheni duniani.

Hii ni sehemu ya ujumbe kutoka kwa Rais Giorgio Napolitano wa Italia kwenda kwa Monsinyo Dario Edoardo ViganĂ², mkurugenzi wa Kituo cha Televisheni cha Vatican katika maadhimisho ya Miaka 30 ya Kituo hicho. Sherehe hizi zimehudhuriwa na wadau mbali mbali katika sekta ya mawasiliano ya jamii ndani na nje ya Italia. Ilikuwa ni fursa kwa wadau hawa kufanya majadiliano ya kina kuhusu mada mbali mbali zinazogusa uwanja wa mawasiliano ya kijamii katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Vatican imekuwa ni mdau mkubwa wa mawasiliano ya jamii, kwani itakumbukwa kwamba, Gazeti la L'Osservatore Romano linalomilikiwa na kuendeshwa na Vatican limekwisha timiza miaka 150 tangu lilipoanzishwa na Radio Vatican hivi karibuni imeadhimisha Miaka 80 tangu ilipoanzishwa, matukio yote haya si haba anasema Rais Napolitano katika ulimwengu wa upashanaji habari.

Kituo cha Televisheni cha Vatican kimekuwa mstari wa mbele kwa kuonesha maisha na utume wa viongozi wakuu wa Kanisa walioko mjini Vatican; matukio ambayo yanatendeka kila kukicha. Ni kwa njia ya kituo hiki kwamba, mamillioni ya watu waliweza kumfahamu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili katika maisha na utume wake ndani ya Kanisa.

Ni kituo ambacho kimefuatilia kwa umakini mkubwa mikutano ya uchaguzi wa Mapapa katika kipindi cha miaka thelathini iliyopita, lakini kwa umahiri na ufanisi mkubwa wakati wa uchaguzi wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI na Papa Francisko.

Rais Giorgio Napolitano anakipongeza Kituo cha Televisheni cha Vatican kwa kusoma alama za nyakati na kwenda na wakati katika mabadiliko ya maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari duniani. Anawatakia kheri na baraka tele katika utume wao kwenye ulimwengu wa mawasiliano ya Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.