Maadhimisho ya Mwaka wa Imani Jimbo Katoliki Zanzibar!
Jimbo Katoliki la Zanzibar limeadhimisha Jubilei ya Miaka 150 tangu imani Katoliki
iingie katika visiwa hivyo. Adhimisho hili limefanyika Jumamosi, tarehe19 Oktoba 2013.
Tukio hili la kihistoria limeanza kusherehekewa kwa kufunguliwa rasmi shule iliyoanzishwa
na Jimbo: Francis Maria Paul Libermann School.
Padri Francis Maria Paul Libermann
ni mwasisi wa Shirika la Mapadri Mapadri wa Roho Mtakatifu (The Spiritans) ambao walihusika
na upandaji wa mbegu ya imani katika visiwa hivi. Pd. Francis alifanya jitihada za
pekee kuwakomboa watumwa, na kuwapatia elimu, kwani aliamini kwamba “Elimu ni ufunguo
wa maisha, kumwezesha mtu kupata uhuru wa kweli.”
Mgeni rasmi katika Jubilei
hii na ufunguzi wa shule na mahafari kwa wanafunzi wa chekechea, msingi na sekondari
alikuwa ni Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, askofu mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.
Katika nasaha zake alisisitiza juu ya umuhimu wa elimu. Kwani elimu si tu inamkomboa
mwanadamu kutoka katika ujinga na imani potofu, lakini pia ni kiungo thabiti cha upendo,
amani ustawi na mshikamano katika jamii. Kardinali Pengo asisitiza kuwa elimu inafukuza
dhana ya kudhaniana vibaya, inafukuza chuki kati ya watu, inafukuza uadui; kwani yenyewe
ni nuru kati ya wanajamii.
Askofu Augustino Ndeliakyama Shao katika adhimisho
hili, alisisitiza umuhimu wa elimu. Alitanabaisha kwamba, Kanisa linatoa elimu si
kwa lengo la kidini, lakini kwa lengo la kumnyanyua mwanadamu toka katika tope la
ujinga, ambalo ni adui mkubwa wa maendeleo ya watu. Alimshukuru Mwadhama Kardinali
Pengo kwa kutenga muda wake na kushirikiana nao katika tukio hilo adhimu.
Shule
ya Francis Maria Paul Libermann, ipo katika Shehia ya Tomondo, Wilaya ya Magharibi,
Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, kiasi cha kilomita 10 kusini mwa Mji Mkongwe Zanzibar.
Inajumuisha shule ya chekechea, shule ya msingi na shule ya sekondari (kidato 1-4).
Ilianza kujengwa mwaka 1994.
Shule hii ina changamoto mbalimbali, hasa upatikanaji
wa idadi ya kutosha ya wanafunzi kwa madarasa yote, tatizo la kulipa ada kwa wakati,
upatikanaji wa walimu wa kutosha na wenye sifa sitahiki, majirani wanaozunguka shule
kutoelewa malengo ya shule hiyo na hivyo kutokuwa tayari kuwapeleka watoto wao hapo
shuleni kupata elimu na umuhimu wa kuwepo kwa amani.
Sherehe ilihudhuriwa na
mapadri, watawa na wazazi wa wanafunzi na ilipambwa na shamrashamra mbalimbali ikiwemo
kubariki jiwe na msingi na udungo wa shule hiyo, pamoja na shangwe mbalimbali za kitamaduni
zilizofanywa na wanafunzi wenyewe: utenzi, nyimbo za kiswahili na kifaransa na ngoma.
Ngoma ya kibati yenye asili ya kisiwa cha Pemba ilitia fora.
Mwishoni, Mwadhama
aliwaahidi kurudi tena pamoja na maaskofu wote, au angalau wa metropolitani ya Dar
es Salaam, kuja kumshukuru Mungu pamoja nao, kwani Zanzibar ndilo lango la imani ya
Afrika Mashariki yote, Jubilei yao, ni jubilei ya Afrika’ Mashariki nzima.