2013-10-21 14:53:22

Boresheni huduma kwa wananchi, msiridhike na ubora wa majengo!


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa majengo mazuri ya ofisi za Halmashauri mbali mbali nchini ni muhimu lakini muhimu zaidi ni wafanyakazi na watumishi wa halmashauri hizo kuwa waaminifu na waandilifu katika utumishi wa umma. Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa ni wajibu wa watumishi wa halmashauri nchini kupunguza manung’uniko na malalamiko ya wananchi kwa kutimiza ipasavyo wajibu wao wa kutumikia wananchi.

Rais Kikwete ameyasema hayo Jumapili, Oktoba 20, 2013, wakati alipoweka jiwe la msingi kwenye Ujenzi wa Jengo la Halmashauri ya Mji wa Njombe kwenye eneo la Mji Mwema, nje kidogo ya mji wa Njombe. Rais Kikwete ambaye yuko katika ziara ya siku saba ya kikazi katika Mkoa wa Njombe amewaambia wananchi na viongozi waliohudhuria sherehe hizo ya kuweka jiwe la msingi:

“Nawapongezeni kwa kujenga jengo zuri na jipya kama hili. Linaongeza heshima kwa mji wa Njombe ambao ni makao makuu ya Mkoa wa Njombe. Lakini ubora wa jengo pekee hautoshi kwa utumishi bora wa wananchi,” amesema Rais Kikwete na kuongeza: “Ubora wa utumishi wa wananchi utapatikana tu endapo watumishi wa halmashauri hii na nyingine zote nchini watakaofikia kiwango cha kufanya kazi kwa uaminifu, uadilifu,wenye tija na matunda ya dhahiri kwa wananchi.”

Rais Kikwete amesema kuwa moja ya wajibu mkubwa wa watumishi wa halmashauri na wa umma kwa jumla nchini ni kupunguza malalamiko na manung’uniko ya wananchi kwa kuboresha kiwango cha ubora wa utumishi wao.








All the contents on this site are copyrighted ©.