Tamaa ya utajiri wa harakaharaka ni chanzo cha kukomaa kwa biashara haramu ya dawa
za kulevya!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema katika kipindi alichokaa ofisini na
kushughulikia suala la dawa za kulevya amebaini kuwa tatizo la biashara na matumizi
haramuya dawa hizo linakuzwa kwa kiasi kikubwa na hulka ya watu kutaka kupata utajiri
wa haraka.
Ametoa kauli hiyo Ijumaa, Oktoba 18, 2013 wakati akizungumza na
Watanzani waishio jijini Beijing, China alipokutana nao kwenye ubalozi wa Tanzania
nchini China. Waziri Mkuu alikuwa katika siku ya tatu ya ziara yake ya kikazi ya siku
tisa kwa mwaliko wa Serikali ya nchi hiyo.
Amesema wahusika wa biashara hiyo
wana siri kubwa na wanakula kiapo kwani wengi wao wako tayari kufa lakini hawako tayari
kuwataja wale waliowatuma kupeleka mizigo yao.
“Biashara hii imetawaliwa na
usiri mkubwa... watu hawako tayari kutajana. Wako radhi kufa. Changamoto tuliyonayo
ni kuangalia kwa namna gani tunaweza kupunguza shauku hii ya matumizi ya dawa za kulevya,”
alisema.
Waziri Mkuu alikuwa akijibu swali lililoulizwa na Bi. Fatma Matulanga
ambaye yuko masomoni nchini China kutaka kujua ni hatua gani ambazo Serikali imechukua
kuhusiana na suala la vijana 175 waliokamatwa nchini China yakiwemo makosa ya kukutwa
na dawa za kulevya ambayo adhabu yake ni kifo.
Alisema kama taratibu zinaruhusu,
maafisa walioko ubalozini wafanye jitihada ya kuonana na vijana hao na kuwasikiliza
ili waweze kuona namna gani ya kupata taarifa sahihi na kama wako tayari kuwataja
wale waliowatuma.
Awali, Waziri Mkuu alielezwa na Bi. Matulanga kwamba balozi
aliyekuwepo China, Bw. Philip Marmo aliahidi kutuma viongozi wa dini kwenye magereza
hayo ili wawasikilize vijana hao na kuona wanaweza vipi kuwasilisha taarifa zao Serikalini.
Alisema
Rais Jakaya Kikwete aliunda kikosi maalum cha kudhibiti dawa za kulevya ambacho kimekuwa
kikifanya kazi nzuri. Alitoa rai kuwa endapo kuna mtu ana taarifa zozote ama kuwafahamu
watu wanaojihusisha na biashara hiyo, apeleke taarifa kwenye kikosi hicho nao watafanya
uchunguzi wa kina ili kubaini ukweli na hatua stahiki zitachukuliwa.
Waziri
Mkuu alitumia fursa hiyo kuwaeleza Watanzania hao wa ughaibuni hatua mbalimbali za
kisiasa na kiuchumi ambazo nchi imepitia katika siku za hivi karibuni. Pia aliwagusia
kuhusu mchakato wa kupata Katiba mpya na hatua iliyofikiwa.