Dawa ya Reli ya kati Tanzania inachemshwa nchini China!
Kampuni ya ujenzi na uhandisi wa majengo ya “China Civil Engineering Construction
Corporation” (CCECC) imesema iko tayari kuja Tanzania na kujenga upya reli ya kati
ili iwe ya kisasa zaidi endapo wataombwa wafanye hivyo.
Hayo yamesemwa Ijumaa,
Oktoba 18, 2013 na Rais wa CCECC, Bw. Yuan Li alipofanya mazungumzo na Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda jijini Beijing, China. Waziri Mkuu alikuwa katika siku ya tatu ya ziara
yake ya kikazi ya siku tisa kwa mwaliko wa Serikali ya nchi hiyo.
Akizungumza
na Bw. Li pamoja na baadhi ya viongozi kutoka Tanzania alioambatana nao, Waziri Mkuu
alimweleza Bw. Li kwamba hivi sasa reli hiyo imechakaa hali inayofanya mizigo mingi
kutoka bandarini isafirishwe kwa barabara na hivyo kuongeza gharama kwa wasafirishaji.
Alisema
hali hiyo inachangia mzigo kwa Serikali kwani kumekuwa na uharibifu mkubwa wa barabara
kutokana na uzito wa magari yanayobeba mizigo kutoka bandari ya Dar es Salaam hadi
nchi jirani kwa sababu wanaitegemea sana bandari hiyo kwa kupokelea mizigo.
Alipoulizwa
ni uzito kiasi gani unaruhusiwa kwenye barabara za nchini China, Bw. Li alijibu ni
tani 25 (axle load) hali iliyomshtua Waziri Mkuu ambaye alilazimika kumweleza mgeni
wake kwamba barabara za Tanzania haziwezi kudumu kwa miaka mingi kwani hivi sasa zinaruhusu
magari yenye uzito wa tani 56 kupita kwenye barabara zake.
Alisema kutokuwepo
kwa usafiri madhubuti wa reli imekuwa ni kikwazo kikubwa cha usafiri kati ya Dar es
Salaam na Kigoma na Tabora hadi Mwanza lakni pia kutoka Tabora hadi Mpanda. “Kukamilika
kwa reli hii ambayo ni uti wa mgongo wa Taifa letu, kutasaidia hapo baadaye kufungua
milango na Burundi, Rwanda na DRC lakini pia tutaweza kupeleka mizigo hadi Uganda
kwa kupitia Mwanza,” alifafanua.
Kwa upande wake, Bw. Li alimweleza Waziri
Mkuu kuwa tayari wameanza mazungumzo na Wizara ya Uchukuzi na iwapo watafikia muafaka
wako tayari kuja kuijenga reli hiyo.
Akitoa mfano wa zoezi kama hilo, Bw. Li
alisema kutokana na mkopo wa benki ya Exim ya China, Septemba mwaka huu, wameanza
ujenzi wa reli kati ya Djibouti na Sudan Kusini pamoja na reli nyingine ya kuunganisha
Djibouti na Ethiopia ambapo zote mbili zinatarajiwa kukamilika baada ya miaka miwili.
“Hatuwezi
kufumua reli yote kwa mara moja. Ninachoona hapa, ujenzi wake itabidi uende kwa awamu
kwa sababu una gharama kubwa lakini kwa kuanzia tunaweza kuanza Dar es Salaam hadi
Morogoro, awamu ya pili tukatoka Morogoro hadi Dodoma na kuendelea ili usafiri wa
treni uwe ukiendelea wakati ujenzi wa reli nao ukiendelea,” alishauri.
Kampuni
ya CCECC ndiyo iliyojenga reli ya Tanzania hadi Zambia (TAZARA) yenye urefu wa kilometa
1,860 na madaraja 320. Ujenzi wake ulianza mwaka 1970 na kukamilika mwaka 1976.