2013-10-17 11:06:18

Simameni kidete kulinda na kutetea masilahi ya wengi, haki na amani!


Viongozi wa Serikali nchini Tanzania wametakiwa kutotafuta masilahi yao binafsi kwa kupitia migogoro mbalimbali inayojitokeza kati ya wafugaji na wakulima, bali wanatakiwa kutafuta ufumbuzi na kumaliza migogoro ya kijamii ili amani na utulivu viendelee kutawala.

Kauli hiyo imetolewa Siku ya Jumatano na Imamu Hilali Abdula Azizi Yunus wa msikiti wa Bilali area C Dodoma alipokuwa akihutubia baada ya swala ya Eid-El-Hajj iliyofanyika viwanja vya Barafu mjini hapa.

Imamu huyo alisema kuwepo kwa migogoro hiyo siyo wakati wa kujitafutia masilahi, bali kinachotakiwa ni upatikanaji na ufumbuzi wa namna amani itakayotakiwa ipatikane kati ya pande zote mbili. Alisema kitendo cha kuendelea vurugu na serikali kukaa kimiya hali hiyo inatia wasiwasi kwa watanzania na kushuku kuwa pengine viongozi hao wa serikali wanapata masilahi kwa kupitia migogoro hiyo.

Alisema Serikali ina wajibu wa kutatua migogoro inayojitokeza nchini Tanzania kutokana na uwezo na nguvu iliyopo, hivyo hakuna sababu ya kusikia wananchi wanapigana na kuuwana kwa ajili ya malisho ya mifugo na maeneo ya kilimo. Watanzania hawaamini kwamba, serikali kama inaweza kushindwa kama ule mgogoro uliopo kati ya wafugaji na wakulima wilayani Mvomero ambao umekuwa ukichukuwa sura mpya kila unapotokea kwa muda mrefu sasa.

“Hivi kweli serikali ilivyo na nguvu imeshindwa kutatua hii migogoro ya wafugaji na wakulima ikiwemo ile ya wananchi pia kuchomewa nyumba zao na wengine kudaiwa kubakwa, hapa kuna maslahi ndani yake” alisema Imamu.

Wakati huo huo Shekhe wa Mkoa wa Dodoma Rajabu Shabani akihutubia baada ya swala hiyo kwenye msikiti wa Gadaff, amewataka viongozi wa kiasiasa nchini Tanzania kuacha kupeleka hisia zao kuhusu suala la marekebisho ya katiba mpya na badala yake wazingatie maoni ya Watanzania ambao walipelekewa kwa ajili ya kutoa mapendekezo ya namna wanavyotaka rasimu ya Katiba iwe.

Shekhe huyo alisema hata hivyo anategemea viongozi wa vyama vya siasa ambao wamekutana na Rais Jakaya Kikwete mapema Juma hili pia watafanya yale ambayo yatakuwa yana maslahi kwa Watanzania wote na siyo kwa upande wao na vyama vyao!








All the contents on this site are copyrighted ©.