Rais Kikwete asema "Dhambi ya ubaguzi itasababisha kupotea kwa amani na utulivu"
Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania katika hotuba yake kwenye sherehe ya kilele cha mbio
za Mwenge wa uhuru, Kumbu kumbu ya miaka 14 tangu alipofariki dunia Baba wa Taifa
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere sanjari na Wiki ya Vijana Kitaifa, Mkoani Iringa,
tarehe 14 Oktoba 2013, amewaambia watanzania kwamba, dhambi kubwa ya kubaguana inaweza
kusababisha amani na utulivu kutoweka nchini Tanzania, lakini zaidi, jitaabishe kusoma
mwenyewe!
Niruhusuni nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema,
kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kukutana tena mwaka huu kuadhimisha Kilele cha
Mbio za Mwenge wa Uhuru, kumbukumbu ya Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere
na Wiki ya Vijana. Namshukuru sana Mkuu wa Mkoa wa Iringa, na viongozi wenzake pamoja
na wananchi wa Iringa kwa kutupokea vizuri na ukarimu wenu. Pia nawapongeza kwa kukubali
kuwa wenyeji wa maadhimisho haya. Kazi ya kuandaa sherehe kubwa kama hizi siyo jambo
jepesi hata kidogo. Bahati nzuri mambo yamefana sana kama tunavyoshuhudia sote. Hongereni
sana.
Pongezi Wizara
Ndugu wananchi; Niruhusuni pia nitoe
pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Dkt. Fenella Mukangara, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni
na Michezo na Mheshimiwa Zainab Omary, Waziri wa Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana,
Wanawake na Watoto wa Zanzibar kwa uongozi wao makini wa shughuli za Mbio za Mwenge.
Kama tujuavyo shughuli za Mbio za Mwenge husimamiwa na Wizara zetu hizi mbili. Tunawapongeza
kwa kazi nzuri waifanyayo. Ni ukweli ulio wazi kuwa kila mwaka tunashuhudia mambo
yakiwa bora zaidi kuliko mwaka uliopita. Mcheza kwao hutunzwa. Hongereni sana.
Pamoja na Mawaziri napenda kuwatambua viongozi na wafanyakazi wote wa Wizara zetu
mbili waliohusika na Mbio za Mwenge kwa kazi yao nzuri tunayojivunia sote. Aidha,
nawapongeza Wakuu wa Mikoa na Wilaya, viongozi na watumishi wa Serikali zetu mbili
na wajumbe wote wa kamati mbalimbali walioshiriki katika kuratibu Mbio za Mwenge wa
Uhuru mwaka huu. Wamefanya kazi nzuri inayostahili kupongezwa na kila mmoja wetu.
Kwa namna ya pekee nawapongeza ndugu Juma Ali Sumai, kiongozi wa Mbio za Mwenge
na Wakimbiza Mwenge wenzake kwa kutimiza kwa ufanisi wa hali ya juu jukumu kubwa na
zito la kukimbiza Mwenge wa Uhuru nchi nzima. Nawapa pole nyingi kwa changamoto mbalimbali
walizokumbana nazo katika safari ya kilomita nyingi. Kazi hiyo wameimaliza salama
na leo wameukabidhi Mwenge ukiwa salama. Nawapongeza sana kwa kuufikisha ujumbe wa
Mwenge kwa uhodari mkubwa.
Waheshimiwa Mawaziri; Ndugu wananchi; Nafurahi
kusikia kuwa kama ilivyokuwa miaka iliyopita, mwaka huu watu walijitokeza kwa wingi
kila mahali Mwenge wa Uhuru ulipopita. Pia nimeambiwa ujumbe wa Mwenge ulifikishwa
kwa ufasaha na kwamba umepokelewa vizuri. Miradi mingi ya maendeleo imezinduliwa na
kuwekewa mawe ya msingi.
Napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza kwa dhati
kabisa wananchi wa Tanzania kwa ushiriki wao mzuri katika Mbio za Mwenge. Ushiriki
wao ni kielelezo tosha cha kutambua umuhimu wa Mwenge wa Uhuru na cha moyo wa uzalendo
kwa nchi yetu na kuwaenzi waasisi wa taifa letu. Kwa niaba ya Serikali nawahakikishia
kuwa tutaendelea kuwahimiza viongozi wa ngazi mbalimbali kuhakikisha kuwa miradi yote
iliyozinduliwa na kuwekewa mawe ya msingi wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru inaendelea
kutekelezwa kama ilivyokusudiwa.
Kwa namna ya pekee nawapongeza waandishi
na vyombo vya habari kwa kuwa nasi bega kwa bega kuhamasisha watu na kueneza ujumbe
wa Mwenge. Mchango wao umesaidia sana kufanikisha malengo ya Mbio za Mwenge kwani
siku zote wapotoshaji hawakosekani.
Kumbukumbu ya Baba wa Taifa
Ndugu
Wananchi; Kama mjuavyo siku ya kilele cha Mbio za Mwenge pia ni siku ya kuadhimisha
kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa letu la Tanzania kilichotokea miaka 14 iliyopita.
Ni siku ambayo tunawajibika kukumbuka mema mengi aliyoifanyia nchi yetu, mafundisho
yake na urithi aliotuachia. Nia yetu ni kutaka watu wasimsahau kiongozi wetu huyu
maalum na muhimu sana katika historia ya nchi yetu.
Miongoni mwa mambo ya
kukumbuka hasa wakati huu wa Mchakato wa Katiba Mpya ni (jambo la busara kutumia
muda wetu) kujikumbusha mawazo ya Mwalimu kuhusu umoja wa nchi yetu pamoja na Muungano
wa Zanzibar na Tanganyika. Hotuba zake na maandishi yake kuhusu mambo hayo yana mafundisho
mengi mazuri ambayo tukiyaelewa vyema na kuyazingatia yatatusaidia sana katika mjadala
na ukamilishaji wa mchakato wa Katiba mpya.
Mimi naamini fikra za Mwalimu
na mtazamo wake kuhusu umoja wetu na Muungano bado vina maana hata leo. Tujiepushe
na kuyapuuza tusije tukawa na Katiba itakayolibomoa taifa badala ya kulijenga. Ninaposema
hivyo sipendi nieleweke kuwa sitaki mabadiliko ila napenda tuwe makini katika kufanya
mabadiliko. Nataka tufanye mabadiliko yatakayotupeleka mbele na siyo kuturudisha
nyuma.
Ndugu wananchi; Pamoja na kuadhimisha siku ya kifo cha Baba wa
Taifa (Mwalimu Julius Nyerere), nadhani ni vyema pia tukawa tunaikumbuka siku ya kuzaliwa
kwake yaani tarehe 13 Aprili (1922). Nisingependa kujiingiza katika mjadala wa siku
ipi bora zaidi kwani zote ni siku muhimu katika historia ya maisha ya mwanadamu. Tofauti
yake ni kuwa siku ya kuzaliwa ni ya furaha na siku ya kufa ni ya majonzi. Kama tutakubaliana
tuikumbuke na siku yake ya kuzaliwa pengine siku hiyo tungeiita Nyerere Day. Tuiadhimishe
siku hiyo kusheherekea maisha yake kwa kujadili kazi zake na kufanya shughuli mbalimbali
kuenzi mambo mema aliyosimamia na kuifanyia nchi yetu na dunia kwa ujumla.
Kauli
Mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2013
Ndugu Wananchi; Kama alivyoeleza
Mheshimiwa Waziri kila mwaka Mbio za Mwenge wa Uhuru huwa na ujumbe maalum unaobebwa
na kauli mbiu ya mwaka huo. Mwaka huu ujumbe ulikuwa “Watanzania ni Wamoja: Tusigawanywe
kwa Msingi wa Tofauti Zetu za Dini, Itikadi, Rangi na Rasilimali”. Ujumbe huu ni
muafaka kabisa hasa ukikumbuka misukosuko na majaribu makubwa nchi yetu iliyopitia
mwaka huu. Hivyo kutumia Mbio za Mwenge wa Uhuru kukumbushana haja na hoja za kuziba
nyufa zilizoanza kujitokeza ni jambo la busara sana. Ni jambo la kuungwa mkono na
kila mwananchi na hasa kila mzalendo.
Bahati nzuri upepo huo mbaya umepita
na tuombe usirudi tena. Hivi sasa hali ni shwari na Watanzania tunaendelea kushirikiana
vizuri bila ya kubaguana kwa dini zetu, vyama vya siasa na kadhalika kama tulivyozoea
kuishi miaka yote. Waliotaka kutufarakanisha hawakufanikiwa lakini, lazima tuwe makini
kwani wanaweza kujaribu tena kutugawa ama kwa yale yale au mambo mengine.
Ndugu
wananchi; Kwa kweli nafarijika sana kuona Watanzania wakiendelea kukataa ushawishi
na uchochezi wa kugawanywa kwa misingi ya dini au mambo mengine. Ndugu zangu naomba
tuendelee hivyo na hayo ndiyo mafundisho mema na urithi aliotuachia Baba wa Taifa
tunayemkumbuka leo. Tukigawanyika, nchi yetu itavurugika na sote tutakuwa tumeharibikiwa.
Dhambi kubwa ya kubaguana kwa misingi yo yote ile ni kupotea kwa amani na utulivu.
Bila amani, hatuwezi kuishi kwa furaha katika nchi yetu hii nzuri. Bila amani, jamii
haiwezi kujishughulisha kwa ukamilifu na shughuli za kujiletea maendeleo. Amani ikituponyoka
nchi yetu itayumba na hakuna atakayebaki salama.
Napenda kuwahakikishia wananchi
wenzangu wote, kuwa sisi Serikalini tutaendelea kufanya kila tuwezavyo kujenga, kulinda
na kudumisha umoja na mshikamano wetu ambao ndio msingi mkuu wa kuwepo kwa amani na
utulivu nchini. Tutaendelea kukemea kwa nguvu zetu na uwezo wetu wote vitendo vinavyosababisha
mmomonyoko wa umoja na mshikamano wetu. Serikali haitasita kuchukua hatua za kisheria
dhidi ya mtu au kikundi cha watu watakaojihusisha na vitendo vya kuvuruga amani ya
nchi yetu. Naomba Watanzania wenzangu mtuelewe hivyo. Napenda kusisitiza na kuwasihi
kuwa tuendelee kuaminiana, kuheshimiana na kuvumiliana pamoja na tofauti zetu.
Mapambano
Dhidi ya UKIMWI
Ndugu wananchi; Pamoja na ujumbe huu maridhawa ambao
kimsingi ndiyo ujumbe mkuu wa Mbio za Mwenge tangu kuasisiwa kwake, mwaka huu wananchi
waliendelea kuhimizwa kuendeleza mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI, rushwa na dawa
za kulevya. Tangu ugonjwa wa UKIMWI uingie nchini kwetu mwaka 1983, inakadiriwa kuwa
zaidi ya ndugu zetu milioni 2 wamepoteza maisha kutokana na maradhi haya. Hali kadhalika
zaidi ya watoto milioni 1.3 wamekuwa yatima na watu zaidi ya milioni 1.5 wanaishi
na VVU hivi sasa. Bahati mbaya karibu asilimia 65 ya hao ni wanawake.
Kitaifa,
takwimu zinaonesha kuwa maambukizi ya UKIMWI yanazidi kupungua kutoka asilimia saba
mwaka 2005 hadi asilimia 5.7 mwaka 2010 na kufikia asilimia 5.1 mwaka 2012. Hapa Iringa
napo maambukizi yamekuwa yanapungua ingawaje bado yapo juu na kwamba ni Mkoa wa pili
nchini kuwa na kiwango cha juu cha maambukizi. Takwimu zinaonesha kuwa kiwango cha
maambukizi Mkoa wa Iringa ni asilimia 9.1, wanaume asilimia 6.9 na wanawake asilimia
10.9. Mkoa wa Njombe ndiyo unaoongoza ukiwa na asilimia 14.8.
Kwa sababu
ya maradhi haya idadi ya watoto yatima ni kubwa katika mkoa huu (inakadiriwa kuwa
waliopo ni 3400). Inahuzunisha sana kusikia au kuona baadhi ya watoto hawa wamelazimika
kukatisha masomo yao baada ya wazazi wao kufariki ili kuwalea wadogo zao. Kwa ajili
hiyo, wamelazimika kufanya kazi zisizostahili kufanywa na watu wa umri wao. Wapo
pia wazee ambao kwa umri wao wanahitaji kulelewa lakini wamebaki peke yao na wakati
mwingine wanalazimika kulea watoto walioachwa na watoto wao.
Ndugu wananchi; Nilishaagiza
viongozi siku za nyuma na leo narudia tena kuwa, tuwatambue watoto yatima kisha tutengeneze
mipango thabiti ya kuwasaidia. Lengo letu hapa ni kutaka tuwawezesha kupata fursa
ya kukua na kuishi kama watoto wengine. Jambo moja muhimu nililolisisitiza ni kuwa
tuhakikishe kuwa vijana hawa wanapata elimu ambayo ndiyo ufunguo wa maisha yao.
Ndugu
wananchi; Tuongeze ari, nguvu na kasi ya kupambana na gonjwa hili hatari.
Ni kweli tunapata mafanikio lakini hayatoshi. Kiwango bado ni cha juu mno. Nawaomba
viongozi wa Serikali, dini, asasi za kijamii, wanasiasa na wananchi tuendelee kuhamasisha
jamii kujiepusha na ugonjwa huu. Tuwahimize watu wajitokeze kupima wajue mustakabali
wao, waepuke ngono nzembe na hasa hasa wawe na subira na waaminifu kwa ndoa zao au
wapenzi wao. Sisi katika Serikali tutaendelea kutimiza wajibu wetu wa kuelimisha
na kuhakikisha kuwa dawa za kufubaza vijijidudu vya UKIMWI zinapatikana bure kwa waathirika
waliofikia hatua ya kutumia dawa hizo.
Natoa wito kwa wananchi wa
Mkoa wa Iringa kuongeza juhudi maradufu kutokana na ukweli kwamba kiwango cha maambukizi
kiko juu mno. Watu waendelee kujitokeza kwa wingi kupima kwa hiari ili kujua afya
zao. Katika zoezi la kupima kwa hiari hapa Iringa, watu 388,071 wamejitokeza kupima.
Jambo hili ni jema sana. Napenda pia kuchukua fursa hii kuwasihi akina mama wajawazito
wawe mstari wa mbele kupima VVU ili wale walioathirika waitumie ipasavyo huduma ya
kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Huduma hii inamfanya mtoto
anayezaliwa na mama aliyeathirika kuwa salama. Huduma hii ipo kote nchini na inatolewa
katika hospitali zote za Serikali.
Ndugu wananchi; Ombi langu
maalum kwa wanaume, kote nchini ambao bado hawajafanyiwa tohara wajitokeze kwa wingi
kufanya hivyo. Madaktari wanasema kuwa mwanaume aliyefanyiwa tohara anapunguza kwa
kiasi kikubwa hatari ya kuambukizwa VVU wakati wa kujamiiana. Naomba ieleweke kuwa
sisemi mtu akifanyiwa tohara hapati UKIMWI. La hasha. Ninachosema ni kwamba ukimlinganisha
na yule ambaye hakufanya hivyo, uwezekano wa kuambukizwa unapungua. Wanasema asiye
na tohara ana uwezekano mkubwa zaidi wa kupata michubuko ambayo hurahisisha virusi
kuingia kwenye mwili wake. Narudia kusisitiza mtu akipata tohara asidhani yuko salama
kabisa. Watu wote lazima wachukue tahadhari stahiki.
Ndugu wananchi; Ombi
langu la pili ni kwa watu wanaotumia dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI wasiache kuzitumia.
Wakiacha kwa sababu yo yote ile wanavipa vijidudu nafasi kujiimarisha na hivyo kuhatarisha
maisha yao. Ombi langu la tatu ni kwa jamii kuendelea kuwasaidia na kuwahudumia wenzetu
ambao wameathirika badala ya kuwanyanyapaa na kuwatenga. Na, muhimu zaidi tuwasaidie
watoto yatima na wazee ambao wameachwa bila msaada wowote.
Nawataka
viongozi wote katika ngazi mbalimbali washiriki kwa ukamilifu katika mapambano dhidi
ya maradhi ya UKIMWI. Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Afya na TACAIDS waendelee kuongoza
mapambano hayo bila kuchoka. Mimi bado naamini Tanzania bila UKIMWI inawezekana iwapo
tutazingatia masharti ya kuepuka ugonjwa huu na kuwahudumia ipasavyo walioathirika.
Ushindi hauko mbali sana.
Mapambano dhidi ya Rushwa
Ndugu wananchi;
Mwaka huu, katika Mbio za Mwenge wa Uhuru wananchi waliendelea kukumbushwa wajibu
wao katika kupambana na rushwa, kwa kauli mbiu isemayo “chukua hatua dhidi ya rushwa
sasa”. Ujumbe huu unakwenda sambamba na juhudi za serikali za kupambana na rushwa
nchini. Tunafahamu kuwa rushwa ni adui wa haki na kikwazo kikubwa cha maendeleo
ya jamii na taifa. Nchi ikiwa imegubikwa na vitendo vya rushwa itakosa maendeleo
stahiki na watu watadhulumiwa haki zao.
Hizo ndizo sababu kuu zilizoifanya
serikali yetu ichukie rushwa na kuchukua hatua za kupambana na uovu huu, tangu nchi
yetu ilipopata uhuru mpaka sasa. Kazi hiyo ngumu na yenye changamoto nyingi inaongozwa
na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU). Serikali imechukua na itaendelea
kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha chombo hiki ili kiweze kutimiza majukumu
yake kwa ufanisi zaidi. Matokeo yake TAKUKURU sasa ina mtandao mpana zaidi. Ina ofisi
kila Mkoa na kila Wilaya, watumishi wameongezeka na vitendea kazi pia.
Nafurahi kuona kuwa mafanikio ya kutia moyo yanaendelea kupatikana ingawaje kazi iliyo
mbele yetu bado ni kubwa. Sote tunasoma na kusikia kupitia vyombo vya habari taarifa
za watumishi wa serikali, taasisi za umma pamoja na watu wengine wanavyokamatwa na
TAKUKURU kwa kujihusisha na vitendo vya rushwa. Tangu mwaka 2006, kesi 63 zinazohusu
rushwa kubwa zimefikishwa Mahakamani. Baadhi zimeisha na wahusika waliopatikana na
hatia wameadhibiwa kwa mujibu wa sheria. Zipo pia tulizoshindwa, ni sawa katika nchi
inayoheshimu utawala wa sheria. Nyingine zinaendelea. Vile vile juhudi za TAKUKURU
zimeokoa fedha nyingi za umma. Kwa mfano, kwa kipindi cha miaka mitatu, yaani kati
ya 2010 hadi 2013, zaidi ya shilingi bilioni 28 zimeokolewa ambazo zingeweza kunufaisha
watu wachache wanaoendeleza vitendo vya rushwa badala ya taifa.
Naomba
wananchi waendelee kutoa taarifa zitakazosaidia kuwatambua na kuwakamata watoaji na
wapokeaji rushwa. Tukumbuke kuwa mafanikio katika mapambano haya hayategemei Serikali
au TAKUKURU peke yake. Ni mapambano ambayo jamii ikijihusisha kwa ukamilifu ushindi
mkubwa utapatikana. Yanatuhusu sote kwani tukishinda, matunda yake yatawafaidisha
watu wote. Pia, napenda kutumia nafasi hii kutoa wito kwa taasisi na idara zote za
serikali zinazohusika moja kwa moja katika vita dhidi ya rushwa zitimize ipasavyo
wajibu wake. Aidha pakiwepo na ushirikiano mzuri na mshikamano wa dhati miongoni mwetu
kwa hakika ushindi utapatikana. Tukifanya hivyo nina imani tutapata mafanikio makubwa
zaidi tena kwa haraka.
Dawa za Kulevya
Ndugu Wananchi;
Tatizo la biashara na matumzi ya dawa za kulevya limeendelea kuwa moja ya changamoto
kubwa zinazolikabili taifa letu. Serikali imeendelea kufanya jitihada kubwa kupambana
na changamoto hiyo. Yapo mafanikio yanayopatikana lakini bado tuna kazi kubwa ya kufanya
mbele yetu. Ukubwa wa kazi hiyo unaletwa na ule ukweli kwamba watu wanaohusika ni
wengi na wanazidi kuongezeka kila kukicha kwa tamaa ya kupata utajiri wa haraka.
Isitoshe wakati wote washiriki wake wanabuni mbinu mpya za kusafirisha, kusambaza
na kuuza dawa hizo haramu. Pia ni kazi hatari kwani wapambanaji kupoteza maisha si
jambo la ajabu.
Pamoja na changamoto hizo, kwa vile matumizi ya dawa za kulevya
yana athari mbaya kwa watu wanaotumia na jamii kwa ujumla, Serikali haitachoka kufanya
kila tuwezalo kupambana na uhalifu huu mpaka ushindi upatikane. Wakibadili mbinu
na sisi tutabadili maarifa ya uchunguzi na utambuzi mpaka tuwapate. Tutawahami ipasavyo
watu wanaojitolea muhanga kupambana na uovu huu. Mafanikio yanaendelea kupatikana.
Kwa mfano, kuanzia Januari hadi Septemba, mwaka huu (2013) watu 2000 (wafanya biashara
na watumiaji wa dawa za kulevya) wamekamatwa na aina mbalimbali ya dawa za kulevya
ikiwa ni pamoja na kilo 681 za dawa hatari ya heroine, zimekamatwa.
Watu hao
kama wasingekamatwa wangeendelea kuuza na kusambaza dawa za kulevya na kuathiri maelfu
ya watu na hasa vijana ambao ni nguvu kazi muhimu ya taifa letu na warithi wa jamii
na taifa wa kesho. Inatia uchungu sana kuona kuwa tegemeo letu hilo linaangamizwa
na watu wachache wenye uroho usio na kifani wa kujipatia utajiri wa haraka, tena kwa
gharama yoyote ile.
Ndugu wananchi; Kwa niaba yenu, napenda kutumia
nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa viongozi na wafanyakazi wote wa Tume ya
Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya na vyombo vingine vya dola kwa kazi kubwa
na nzuri inayoendelea kufanyika ya kukabiliana na tatizo hili. Katika mapambano
yetu tunashirikiana na nchi na taasisi za nchi mbalimbali duniani. Hivyo basi nazipongeza
kwa dhati nchi na taasisi hizo rafiki kwa ushirikiano wao ambao umetusaidia kupata
mafanikio haya kiasi tunayojivunia leo. Naomba ushirikiano huu uendelee kwani umetusaidia
kwa namna nyingi na umekuwa wa manufaa makubwa.
Ndugu wananchi; Nilishawahi
kusema siku za nyuma kuwa ni makusudio yangu na ya serikali kuanzisha chombo chenye
uwezo na nguvu kubwa zaidi ya kupambana na tatizo la dawa za kulevya nchini. Mchakato
wa kuunda chombo hicho umeanza na unaendelea vizuri. Hivi sasa tunayo Tume ya Kuratibu
Udhibiti wa Dawa za Kulevya. Chombo hicho kipya kitakuwa na nguvu kubwa zaidi kuliko
Tume na hata kuliko kikosi kazi cha vyombo vyote vya dola nilichokiunda kuipa Tume
meno.
Ndugu wananchi; Ili juhudi hizo zifanikiwe na ushindi upatikane itategemea
sana msaada, ushirikiano na ushiriki wa wananchi. Nawaomba sana ndugu zangu wananchi
wenzangu mshirikiane na vyombo vya dola katika kupambana na usafirishaji, uuzaji na
usambazaji wa dawa za kulevya. Baadhi yenu mnawajua watu wanaojihusisha na biashara
hii haramu. Watajeni washughulikiwe ipasavyo.
Wiki ya Vijana
Ndugu wananchi; Kama nilivyosema awali leo pia tunaadhimisha wiki ya vijana. Nimepata
fursa ya kutembelea mabanda ya maonesho ya vijana ili kuona shughuli wanazozifanya.
Nimefurahi na kufarijika sana na kile nilichokiona. Vijana wanafanya kazi nzuri na
kwa kweli ni uamuzi wa busara kuwashirikisha katika sherehe hizi kwani wanapata fursa
ya kuonesha kazi wanazozifanya katika kuboresha maisha yao na kuleta maendeleo ya
taifa. Hii pia ni nafasi nzuri kwa vijana kukutana, kufahamiana na kubadilishana mawazo,
ujuzi na taarifa muhimu zinazohusu maisha na maendeleo yao. Kwa kuzingatia umuhimu
na faida ya maonesho haya, ni vyema kuangalia uwezekano wa maadhimisho ya Wiki ya
Vijana yakafanyika katika ngazi ya Mikoa na kuhitimishwa Kitaifa kama tulivyofanya
leo.
Ndugu wananchi; Mimi na wenzangu Serikalini tunatambua na kuthamini
sana nafasi na mchango wa vijana katika kuchochea maendeleo ya nchi yetu. Ndio maana
Serikali inawekeza sana katika elimu na mafunzo yao. Ndiyo maana pia Serikali imeamua
katika mwaka huu wa fedha kuongeza uwezo wa bajeti ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni
na Michezo ili iweze kuwahudumia vijana vizuri zaidi. Tutaendelea kuongeza bajeti
hiyo ili Wizara iweze kuwaongezea vijana mitaji ya biashara kupitia Mfuko wa Taifa
wa Maendeleo ya Vijana.
Nimefurahi kumsikia Mheshimiwa Waziri akiahidi hapa
kwamba baadhi ya vijana walioshiriki katika maonesho niliyoyaona leo watafikiriwa
kupewa mikopo kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa. Nawasihi vijana watakaopata mikopo
kupitia Mfuko huu pamoja na mifuko mingine ya uwezeshaji wahakikishe wanaitumia vizuri
kwa malengo yaliyokusudiwa na kuirejesha kwa wakati ili wengine nao wapate.
Maendeleo
ya Mkoa wa Iringa
Ndugu wananchi; Jana jioni nilipokea taarifa
ya maendeleo ya Mkoa wa Iringa kutoka kwa Mkuu wa Mkoa, Dokta Christine Ishengoma.
Natoa pongezi nyingi kwa wananchi wa Iringa kwa juhudi zenu na mafanikio mnayoyapata
katika kujiletea maendeleo. Mkoa umeendelea kuwa wa kutegemewa katika kulipatia taifa
chakula hasa mahindi na sasa mwelekeo ni mzuri kwa mazao ya chai, mpunga, mboga na
matunda. Nawaomba muendelee na juhudi zenu. Ongezeni maarifa na matumizi ya zana za
kisasa na pembejeo za kilimo ili tija iongezeke mpate mavuno mengi zaidi. Mtatosheleza
mahitaji yenu na mtapata ziada kubwa itakayotumika kwingineko nchini na hata kuuzwa
nje ya nchi. Sisi katika Serikali tutaendelea kuwasaidia kwa upande wa upatikanaji
wa pembejeo, zana za kilimo, masoko, huduma mbalimbali zikiwemo za ugani, fedha na
kadhalika. Mkoa wa Iringa utanufaika kupitia Mpango wetu wa Matokeo Makubwa Sasa (Big
Result Now) na SAGCOT.
Ndugu wananchi; Serikali itaendelea kununua mahindi
ya wakulima kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula. Hata hivyo ni vyema nikaeleza
wazi kuwa Hifadhi ya Taifa ya Chakula haitanunua mahindi yote yaliyovunwa nchini.
Ukomo wetu kwa sasa ni tani 250,000 lakini tunaendelea kupanua uwezo wa maghala hadi
kufikia tani 400,000 ifikapo mwaka 2015. Tayari Hifadhi ya Taifa wameshanunua tani
209,000 hivyo bado tani 41,000. Hivyo nashauri wenzetu wa sekta binafsi nao wajitokeze
kununua mahindi ya wakulima.
Kwa kuwa hakuna kizuizi cha kuuza nje wanaweza
kufanya hivyo wakipenda. Hata hivyo, sisi tungependa kwanza wauze hapa nchini. Naomba
ieleweke kuwa hatutawauzia watu akiba yetu ya mahindi katika Hifadhi ya Taifa ya
Chakula kwa ajili ya kuuza nje.
Ndugu wananchi; Pamoja na kuendeleza
kilimo katika Mkoa wa Iringa, tutaendelea kuboresha barabara, na huduma za umeme,
maji, elimu na afya. Ninyi ni mashahidi kwamba utekelezaji wa ahadi ya kujenga barabara
ya lami kutoka Iringa hadi Dodoma unakwenda vizuri na ukarabati wa barabara ya Morogoro
– Tunduma kupitia Iringa na Mbeya umekamilika. Tunajipanga kutekeleza ahadi zetu
kwa baadhi ya barabara za Mkoa huu.
Kwa upande wa umeme vijijini tunaendelea
kuvipatia umeme vijiji 38 vya Mkoa huu na wakati huo huo tunajiandaa kuvipatia umeme
vijiji vingine 86. Tutaendelea kuongeza upatikanaji wa maji vijijini na mijini. Aidha,
tumeanza kutekeleza mkakati kabambe wa kuboresha elimu kwa shabaha ya kutoa fursa
ya elimu kwa vijana wetu wengi na kuongeza kiwango cha ufaulu. Haya yote tunayafanya
chini ya mkakati mpya wa kupata Matokeo Makubwa Sasa. Tutaongeza mara dufu juhudi
za kuboresha huduma ya afya.
Hitimisho
Ndugu wananchi; Kabla
ya kumaliza hotuba yangu niwakumbushe Watanzania wenzangu kuwa mwaka ujao ni wa aina
yake katika nchi yetu. Kwanza tunasherehekea miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar,
pili, tunasherehekea miaka 50 ya Muungano. Na tatu, kama mambo yatakwenda sawa tutapata
Katiba Mpya. Niwaombe Watanzania wenzangu tujiandae vyema kufanikisha mambo yetu hayo
matatu ya kihistoria. Naomba nimalize kwa kuwashukuru tena wananchi na viongozi wa
Mkoa wa Iringa kwa kufanikisha sherehe hii muhimu. Nawashukuru pia wadau mbalimbali
ambao wamechangia kwa hali na mali kufanya sherehe hizi zifanikiwe na kufana sana
kama hivi. Napenda kutumia nafasi hii pia kuwatakiwa ndugu zetu Waislamu na Watanzania
wenzangu wote heri ya Sikukuu ya Idd El Hajj.
Baada ya kusema hayo sasa natamka
rasmi kwamba shughuli za Mbio za Mwenge wa Uhuru, kumbukumbu ya Baba wa taifa Mwalimu
Julius Kambarage Nyerere na Wiki ya Vijana kwa mwaka 2013 zimefikia kilele chake.
Asante sana kwa kunisikiliza.