Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 28 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji, ninapenda kukusalimu na kukualika katika kipindi cha tafakari
ya Neno la Mungu : masomo Dominika 28 ya mwaka C. Neno la Mungu latudai kuwa wenye
imani inayorudisha upendo na shukrani kwa Mwenyezi Mungu.
Katika somo la kwanza
tunamwona Naamani, jemedari mpagani mara baada ya kuponywa ukoma wake anarudisha tunda
la shukrani kwa Mungu kwa njia ya mtumishi wa Mungu. Naamani ni mfano bora katika
upagani wake wa kutoa shukrani kwa Mungu.
Basi wale wote waliowabatizwa wanadaiwa
zaidi kuliko mpagani huyu Naamani katika wajibu wa kumrudishia Mungu shukrani kwa
ajili ya ukombozi walioupokea kwa njia ya Damu Azizi ya Bwana pale msalabani. Katika
somo la II Mt. Paulo anamwasa Mtakatifu Timotheo, daima kuweka mawazo na kumbukumbu
zake zote katika Yesu Kristu mfufuka.
Akimwambia hilo anasema si wewe tu,
bali hata yeye mwenyewe ni mteswa wa Bwana na zaidi katika utume wake. Katika hilo
anasema Neno la Mungu ni hai halifungwi katika mateso hayo bali tunazidi kulichangamkia
ili liweze kupiga mbio na kufikia lengo lake la kuwaokoa watu. Anamkumbusha Mtakatifu
Timotheo ukuu wa Mungu akisema, hata sisi tusipoamini, upendo na uaminifu wa Mungu
hubaki palepale! Kumbe sasa mwaliko ni kustahimili katika mausia na mafundisho yake
Mungu ili kuweza kubaki naye daima, tukitumikia sas ana kisha kuurithi uzima wa milele.
Mpendwa
msikilizaji, Injili yaweka mbele yetu, Bwana wetu Yesu Kristo aliyeko katika hekaheka
na shughuli za kichungaji, yuko njiani akipita vijiji vya Samaria na Galilaya akielekea
Yerusalemu. Sote twatambua anaelekea Yerusalemu kufanya nini! Bwana akiwa katika utume
huo atakutana na watu 10 wenye ukoma. Watu hawa wanaonekana kuwa na mbegu ya imani
na hivi wanapaaza sauti na wanamwalika Bwana awahurumie na kuwaondoa katika shida
yao.
Bwana anawapokea na anawaambia nendeni mkajioneshe kwa makuhani. Bwana
anataka watu hawa wakutane na uso wa Mungu katika safari hiyo ya kwenda kujionesha
kwa makuhani. Wanakutana na Mungu ambaye haogopi sura zilizoharibiwa na ukoma ndio
dhambi bali Mungu anayezikumbatia sura hizo na kuzisikiliza toka moyoni mwake.
Mwinjili
anataka kutufundisha kuwa kupona ni tendo la safari ya kiimani, ni tendo la kukutana
na uso wa Mungu, na zaidi ya hayo, ni jambo linalojengwa katika upole na linataka
pia kushirikisha jumuiya ya watu, ndiyo maana ya kuwaambia waende wakajioneshe kwa
makuhani.
Mpendwa msikilizaji, mara kadhaa mantiki yetu ni kuwakwepa hawa walioharibiwa
na magonjwa na hivi kuwasukumiza pembezoni, basi leo Bwana anataka tukajenge mfumo
wa upendo unaokumbatia watoto wa Mungu pasipo ubaguzi kwa furaha na matumaini. Bwana
akisha kuwaambia waende wakajioneshe kwa makuhani wanaondoka na huko njiani wanatakasika.
Ujumbe mara moja ni kwamba kukutana na Bwana ni utakaso, ni kujikabidhi kwake ili
atende apendavyo na matokeo yake ni kuwa safi.
Baada ya tendo la kutakaswa
Bwana anakuja na hoja nyingine akitaka kujenga moyo wa shukrani katika kuishi imani
yetu, ndiyo kusema chochote tukipatacho tuseme asante kwa yule anayetupatia na zaidi
Mungu mgawaji wa mapaji yote. Ni katika mantiki hiyo Mwinjili anamweka Mkoma aliyetakasika
mbele yetu, akirudi kumshukuru Bwana. Na mtakasika huyu cha ajabu alikuwa Msamaria!
Wengine ambao pengine wangesadikika zaidi kuwa wa kwanza kutoa shukrani hawakuonekana!
Katika hili Bwana atajenga moyo wa shukrani lakini pia atajenga mantiki ya kuwainua
Wasamaria ambao walisadikika wazushi na wasio na akili, lakini sasa badala yake wanakuwa
mfano bora wa imani na shukrani kwa Mungu. Mpendwa shukrani haitegemei kumbe kabila
lako bali unyenyekevu wako ukijikabidhi mikononi mwa Bwana aliyekuondoa katika uvuli
wa mauti kwa njia ya ubatizo.
Tukisonga mbele katika tafakari tunaona kisha
tendo hilo la shukrani basi Bwana anasema inuka uende zako imani yako imekuponya.
Jambo la nguvu ambalo twapaswa kulishikilia pia katika fundisho la Bwana ni lile hasa
la kuguswa na sura ya Mungu na kuweza kuangaziwa ili kuweza kutoa shukrani kwake.
Katika siku zetu hizi suala la shukrani sasa linaanza kuwa adimu sana.
Kumbe
kumbuka shukrani na imani havitengani kabisa. Shukrani ya Msamaria inampa Bwana nguvu
ya kwenda kukabiliana kifo huko Yerusalemu. Ndiyo kusema haitoshi kusema Bwana utuhurumie
bali kuongeza Bwana tunakushukuru kwa zawadi ya Imani, kwa zawadi ya ndoa yetu, kwa
zawadi ya upadre, kwa zawadi ya utawa na karama nyingine zote tulizozipokea toka kwa
Mungu.
Nikutakie moyo wa shukrani daima ukiimba sifa za Bwana daima kwa utenzi
wa shukrani. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard
Tiganya C.PP.S.