2013-10-15 11:03:45

Siku ya Baba wa Taifa na changamoto kwa watanzania!


Serikali ya Tanzania itajenga kituo cha kuwaenzi waasisi wa taifa katika eneo la
Kiromo Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani ambapo tayari upembuzi
yakinifu umefanyika. Kauli hiyo ilitolewa Mjini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani katika mkutano wa
hadhara wa kuadhimisha miaka 14 ya kumbukumbu ya kifo cha Baba wa
taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere yaliyofanyika katika viwanja vya Nyerere Square.

Waziri Kombani alisema licha ya kupata eneo hilo tayari upembuzi
yakinifu umefanyika na athari za kimazingira ambapo pamoja na mambo mengine kituo hicho kitafanya kazi ya kuzifanya, kuhifadhi kumbukumbu, mali na vitu vyenye umuhimu wa kihistoria vya waasisi hao. Alisema kituo hicho pia kitaratibu shughuli zote zinazohusu waasisi ikiwemo kuhamasisha umma kuhusu utafiti, kuandaa machapisho mbalimbali yanayoelezrea michango na kazi mbalimbali walizowahi kufanya waasisi hao.

Waziri Kombani alisema umedhihirisha mataifa mengi duniani yana
utaratibu wa kisheria na kisera wa kuebnzi na kuhifadhi kumbukumbu za
viongozi wao mashuhuri. Alisema katika kufanikisha hilo serikali imeazimia kuweka utaratibu wa sheria wa namna ya kuendesha kusimamia na kuratibu shughuli za
kuwaenzi viongozi wakuu waasisi wa taifa kwa kuhifadhi vielelezo vya
kumbukumbu zao kwa manufaa ya taifa na vizazi vijavyo.

“Heshima, utu, amani na utulivu, demokrasia na maendeleo ya Mtanzania
ni urithi na utajiri wa taifa letu ambao umetokana na juhudi na
mchango mkubwa wa kujitoa mhanga kwa viongozi wetu hawa hivyo hakuna
budi kuyalinda kwa kuwaenzi” alisema

Alisema mwaka 2004 sheria ya kuwaenzi waasisi wa taifa namba 18 ya
mwaka 2004 ilipitishwa na bunge kwa lengo la kuweka utaratibu wa
kuendesha, kusimamia na kuratibu shughului za kuwaenzi waasisi wa
taifa Mwalimu Nyerere na hayati Abeid Aman Karume na kuhifadhi vitu na
kumbukumbu zao kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo. Aidha alisema serikali imefanikiwa kuzitambua taasisi , asasi zinazomiliki kumbukumbu, mali na vitu vyenye umuhimu wa kihistoria kitaifa ili kuhakikisha zinatunzwa vizuri kwa maslahi ya taifa.

Alibainisha kuwa serikali imeunda bodi ya udhamini wa mfuko wa
kuwaenzi waasisi wa taifa ambayo itakuwa na jukumu la kutafuta,
kukusanya na kusimamia fedha za mfuko huo.

Kwa upande wake, Balozi mstaafu Job Lusinde alisema Mwalimu Nyerere
alikuwa mwanasiasa mwenye kipaji cha pekee alimini kuwa siasa kwake ni
kuwatumikia watu waliokuamini na kukupa dhamana ya kuwaongoza. Alisema kutokana na msingi huo mwalimu alikuwa ni mwanasiasa mwenye
maono ya mbali hasa ukizingatia kuwa matukio ya watu aliokuwa
akiwaongoza yalimuumiza na aliguswa nayo kutoka moyoni akiamini,
kuhubiri na kuenenda katika umoja.








All the contents on this site are copyrighted ©.