2013-10-09 15:01:25

Papa Francisko afafanua kwa nini Kanisa ni Katoliki la ulimwengu


Katika katekesi yake ya kila Jumatano, kwa wiki hii Papa Francisko amezungumzia juu ya Kanisa na hasa akieleza maana ya Kanisa kuitwa Katoliki, kama tunavyokiri katika sala ya Nasadiki, Nasadiki katika kanisa moja takatifu Katoliki la ulimwengu.

Papa amesema neno Katoliki, awali ya yote linatokana na neno la Kigriki ' kath'olòn ' maana yake ni kulingana wote kwa ujumla.

Papa aliendelea na mafundisho yake, lakini kwanza alihoji, ina maana gani kusema kanisa katika ujumla wake(katoliki)’ au pia kwetu sisi ina maana gani kusema Kanisa ni la ulimwengu?

Papa Francisko alitoa ufafanuzi kwa kuelezea misingi mitatu ya kanisa kuwa la ulimwengu akisema, awali ya yote –tunasema Kanisa Katoliki ni kwa sababu ni mahali au jengo lililo mahali popote kwa ajili ya kutangaza imani kwa Yesu Kristu, aliye mletea wokovu binadamu, imani inayo tangazwa kwa watu wote bila ubaguzi. Kanisa ni mahali watu wote wanaalikwa kukutana na huruma ya Mungu, ambayo humbadili mtu, kwa kuwa ndani mwake yumo Kristu , zawadi ya kweli katika kuikiri imani , na ni utimilifu wa maisha ya kisakramenti na ukweli wa fumbo la mwili uliotolewa kwetu. Katika Kanisa , kila mmoja wetu ni muhimu kwa ajili ya imani, katika kuyaishi maisha ya Kikristu , katika kuwa watakatifu , na katika kutembea kila mahali na katika kila wakati.

Papa alieleza “Kanisa ni sawa na maisha ya familia, ambamo kila mmoja wetu huutolea uwepo wake kwa ajili wanafamilia, na ni mahali panapo ruhusu binadamu kukua, kukomaa na kuishi. Hakuna anayeweza kukua akiwa peke yake, au kutembea katika safari ya maisha akiwa peke au kujitenga mbali na wengine, bali sote hukua katika mjumuiko wa watu. Na ndivyo ilivyo kwa Kanisa. Katika Kanisa kwa pamoja tunasikiliza Neno la Mungu , tukiwa na uhakika kwamba ni ujumbe toka kwa Bwana alotupatia, ndani ya Kanisa tunaweza kukutana na Bwana katika Sakramenti alizotupatia kama madirisha yaliyo wazi kwa ajili ya kuupitisha mwanga wa Mungu, na miito, na pia ambamo tunaweza kuchota maisha ya Kimungu”.

“Katika Kanisa tunajifunza kuishi katika ushirika na kwamba upendo hutoka kwa Mungu. Mmoja wenu leo hii anaweza kuuliza kwa jinsi gani mimi ninaweza kuishi ndani ya kanisa? Je ni tu katika kushiriki maisha ya jamii au kwenda kanisani au kujifungia mwenyewe na matatizo yangu, au kujitenga mwenyewe na wengine? La sivyo , katika maana hii ya kwanza kwa nini Kanisa ni Katoliki,ni kwa sababu Kanisa Katoliki ni nyumbani kwa kila mtu, sisi sote ni wana wa Kanisa na wote ni wakazi wa nyumba hiyo Kanisa “.

Papa aliendelea kutaja maana ya pili ya Kanisa kuwa Katoliki akisema ni kikatoliki kwa sababu ni zima linalo endelea kuwepo duniani kote kwa ajili ya kutangaza injili kwa kila mwanamme na kila mwanamke . Kanisa sio kundi la wasomi , wala si kwa ajili ya watu wachache. Kanisa halina mpaka, ujumbe wake hupekwa kwa watu wote, jamii nzima ya wanadamu. Kila mtu anaweza kusema: Parokia yangu ni Katoliki , kwa kuwa hiyo ni sehemu ya Kanisa zima la ulimwengu , ambamo mna ukamilifu wa zawadi ya Kristo, imani, sakramenti na huduma katika ushirika na Askofu, na Papa, ni wazi kwa wote bila ubaguzi .

Mwisho, Kanisani Katoliki kwa sababu ni Nyumba ya Mapatano, ambamo na katika hali ya tamaduni na lugha huchanganyika pamoja na kuwa kitu kimoja chenye utajiri wa kipekee. Papa alieleza na kutoa mfano wa kinanda, ambamo vifungo vyake vinaposhikwashikwa kwa namna moja ya makubaliano na maelewano, hutoa muziki muzuri wa kuvutia kucheza pamoja.

Papa alieleza na kumtaka kila mmoja , kumwomba Bwana atufanye sisi sote kuwa wakatoliki, kama familia inavyokua pamoja katika imani na upendo, pia kuwavutia wengine katika umoja wa kanisa, na kupokea zawadi na sadaka ya kila mmoja, kwa ajili ya kumtukuza Mungu kwa pamoja kwa wema wake , neema zake na wokovu wake wa upendo.

Baada ya Katekesi, Papa alitoa salaam zake kwa makundi ya watu waliofika kumsikiliza.








All the contents on this site are copyrighted ©.