2013-10-04 11:02:57

Papa awasili Assis.


Baba Mtakatifu Ijumaa hii (04/10/2013), amefanya ziara ya kichungaji kwenye mji wa asili wa Mtakatifu Francisko wa Assisi na kuadhimisha pamoja na maelfu ya waumini na wahujaji maadhimisho ya Sikukuu ya Mtakatifu Francisko inayosheherekewa kila tarehe nne ya mwezi Oktoba. Itakumbukwa kwamba Mtakatifu Francisko wa Assisi ndiye mtakatifu Msimamizi wa Italia.

Alipowasili mjini Assisi Papa alipokelewa na rais wa Senate ya Italia, mh. Pietro Grasso, na rais wa kanda ya Umbria, Mh. Catiuscia Marini. Alishuka kwenye ndege akiwa amejibebea begi lake leusi mkononi huku maelfu ya waumini na mahujaji wakipiga kelele za furaha wakisema: Viva il Papa. Naye Papa alirudisha salamu hizo kwa tabasamu na ishara za kuwabariki wote waliokuwa wakimkaribisha.

Wengi wa wahujaji wamesafiri kutoka mbali na wamekesha usiku kucha nje ya viwanja vya kanisa kuu la Mtakatifu Francisko na madhabahu ya Mtakatifu Maria, malkia wa Malaika, huku wakingojea kwa hamu na gamu kukutana naye Papa Francisko.

Baada ya salamu hizo Papa alielekea moja kwa moja kwa miguu kwenye kituo cha watoto na vijana walemavu cha Seraphicum ambako aliongea nao huku akiwakumbatia na kuwabusu kwa mapendo na maneno ya kuwatia moyo. Kwenye kuta za nje za kituo hicho cha watoto kulikuwa kumeandikwa maneno haya: “Papa Francisko, myenyekevu kati ya wanyenyekevu” na “Unamgusa Mungu aliye Hai, unaishi ukiabudu”

Kituo cha Seraphicum kilianzishwa na mwenyeheri Ludovik da Casoria mnamo tarehe 17 mwezi Septemba mwaka 1871, kama kumbukumbu ya makovu au stigmata ambayo Yesu alimshirikisha mtumishi wake Francis wa Assisi, kama ishara ya mateso ya Yesu ambayo wanashirikishwa pia walemavu. Kwa sasa hivi kituo hicho kina jumla ya walemavu 60 wanaotunzwa humo.

Alipowasili kwenye kituo cha Seraphicum Baba Mtakatifu alipokelewa na mwakilishi wake nchini Italia, Mons. Adriano Bernadini, na Askofu wa Assisi, Mons. Domenico Sorrentino. Papa aliandamana na Markadinali nane, washauri wake aliowateua hivi karibuni kwa ajili ya kutekeleza marekebisho ndani ya utendaji kazi wa vatikani, na kwa ajili ya kuboresha uongozi wa Kanisa pote ulimwenguni.

Papa alipokuwa anasalimiana na watoto na vijana wa Seraphicum wauguzi wengine walibeba juu kwa juu bango lenye maandishi: Francisko, jenga nyumba yangu- maneno ambayo yanasemekana kusemwa na Yesu mwenyewe kama mwaliko kwa Mtakatifu Francisko, aliyeacha vyote na kumfuata Kristo baada ya kuyasikia, alipokuwa akisali kwenye kanisa la Mtakatifu Dominiko, zaidi ya miaka mia nane iliyopita.











All the contents on this site are copyrighted ©.