Baba Mtakatifu Ijumaa hii (04/10/2013), amefanya ziara ya kichungaji kwenye mji wa
asili wa Mtakatifu Francisko wa Assisi na kuadhimisha pamoja na maelfu ya waumini
na wahujaji maadhimisho ya Sikukuu ya Mtakatifu Francisko inayosheherekewa kila tarehe
nne ya mwezi Oktoba. Itakumbukwa kwamba Mtakatifu Francisko wa Assisi ndiye mtakatifu
Msimamizi wa Italia.
Alipowasili mjini Assisi Papa alipokelewa na rais wa
Senate ya Italia, mh. Pietro Grasso, na rais wa kanda ya Umbria, Mh. Catiuscia Marini.
Alishuka kwenye ndege akiwa amejibebea begi lake leusi mkononi huku maelfu ya waumini
na mahujaji wakipiga kelele za furaha wakisema: Viva il Papa. Naye Papa alirudisha
salamu hizo kwa tabasamu na ishara za kuwabariki wote waliokuwa wakimkaribisha.
Wengi
wa wahujaji wamesafiri kutoka mbali na wamekesha usiku kucha nje ya viwanja vya kanisa
kuu la Mtakatifu Francisko na madhabahu ya Mtakatifu Maria, malkia wa Malaika, huku
wakingojea kwa hamu na gamu kukutana naye Papa Francisko.
Baada ya salamu hizo
Papa alielekea moja kwa moja kwa miguu kwenye kituo cha watoto na vijana walemavu
cha Seraphicum ambako aliongea nao huku akiwakumbatia na kuwabusu kwa mapendo na maneno
ya kuwatia moyo. Kwenye kuta za nje za kituo hicho cha watoto kulikuwa kumeandikwa
maneno haya: “Papa Francisko, myenyekevu kati ya wanyenyekevu” na “Unamgusa Mungu
aliye Hai, unaishi ukiabudu”
Kituo cha Seraphicum kilianzishwa na mwenyeheri
Ludovik da Casoria mnamo tarehe 17 mwezi Septemba mwaka 1871, kama kumbukumbu ya makovu
au stigmata ambayo Yesu alimshirikisha mtumishi wake Francis wa Assisi, kama ishara
ya mateso ya Yesu ambayo wanashirikishwa pia walemavu. Kwa sasa hivi kituo hicho kina
jumla ya walemavu 60 wanaotunzwa humo.
Alipowasili kwenye kituo cha Seraphicum
Baba Mtakatifu alipokelewa na mwakilishi wake nchini Italia, Mons. Adriano Bernadini,
na Askofu wa Assisi, Mons. Domenico Sorrentino. Papa aliandamana na Markadinali nane,
washauri wake aliowateua hivi karibuni kwa ajili ya kutekeleza marekebisho ndani ya
utendaji kazi wa vatikani, na kwa ajili ya kuboresha uongozi wa Kanisa pote ulimwenguni.
Papa
alipokuwa anasalimiana na watoto na vijana wa Seraphicum wauguzi wengine walibeba
juu kwa juu bango lenye maandishi: Francisko, jenga nyumba yangu- maneno ambayo yanasemekana
kusemwa na Yesu mwenyewe kama mwaliko kwa Mtakatifu Francisko, aliyeacha vyote na
kumfuata Kristo baada ya kuyasikia, alipokuwa akisali kwenye kanisa la Mtakatifu Dominiko,
zaidi ya miaka mia nane iliyopita.