2013-10-04 11:00:35

Mafundisho ya Papa, kufanya upya Mji wa Assisi, Asema Meya Claudio Ricci


Kwenye ziara yake ya kichungaji mjini Assisi siku ya Ijumaa, Baba Mtakatifu Francisko alikaribishwa na maneno ya Meya wa Assisi, Bw. Claudio Ricci ambaye alisema kwamba maeneo aliyoishi Mtakatifu Francisko ni urithi kwa ajili ya majadiliano ya kibinadamu, na kwamba sasa mawe yaliyo hai yataanza kuishi maisha mapya kutokana na mwanga mpya unaomulikwa na ziara ya Papa Francisko mjini humo.
Meya Claudio Ricci amemshukuru Papa Francisko kwa kukitembelea kwanza kituo cha wallemavu cha Serafiko, huku akisema kwamba ni ishara kwamba Papa ameukumbatia moyo wa Kifrancisko, wa kuwajali na kuwaonyesha mapendo yaliyojaa huruma, watu walio wanyonge zaidi kwenye jamii; ishara pia ya Kanisa lililojaa mapendo na huruma, na moyo wa kushirikishana mapendo hayo.
Amesema Meya huyo kwamba siku ya ziara ya Papa Francisko mjini humo itabaki kama kumbukumbu hai kwani inawawezesha watu wengi kuelewa maana ya kujitoa bila ya kujibakisha kwa ajili ya hadi na heshima ya binadamu wengine.
Amemshukuru Papa pia kwa mafundisho yake ambayo yanaendelea kuwachangamotisha na kuwapa matumaini mapya yaliyojengwa juu ya unyenyekevu watu wengi kote duniani, huku akisema kwamba mji wa Assisi hautabaki ule wa zamani, kwani baada ya kuondoka mjini humo zawadi ya mafundisho yake Papa yataendelea kuupyaisha mji huo, upya ambao utakuwa kiini cha mazungumzo mapya ya jumuia ya kibinadamu.
Ni ziara ya kwanza ya kichungaji mjini Assisi inayofanywa na Papa ambaye amelichagua jina la Mtakatifu huyo wa Assisi na kuikumbatia roho ya mtakatifu huyo aliyeishi kwenye Karne ya 12 na13.











All the contents on this site are copyrighted ©.